Namna ya kukabiliana na mwezi Januari

Muda wa kusoma: Dakika 3

Baada ya Krismasi iliyo katika mwezi wenye matumizi ya kupita kiasi, kipindi kinachofuata ni Januari. Mwezi huu unafahamika na wengi kama wenye changamoto za ukosefu wa pesa labda pengine hilo huchochewa na watu kufanya matumizi mengi kipindi cha mwezi uliotangulia kiasi hata cha kuwa na madeni.

Ukweli ni kwamba usipokuwa makini unaweza kuona mwezi Januari kuwa mgumu kuliko yote, lakini kuna mawili matatu tuliyokusanya yanayoweza kuwa msaada mkubwa katika mwezi huu.

1. Tengeneza bajeti

Wengi hutengeneza bajeti lakini tatizo ni kwamba mara nyingi huwa haifwati.

Bajeti itakusaidia katika mwelekeo wa matumizi ya pesa zako na jinsi zinapaswa kutumika.

Pia inakuambia ni kiasi gani cha pesa ulicho nacho cha kutumia kila mwezi na pale ambapo unahitaji kupunguza ikiwa unatumia matumizi kupita kiasi.

2. Panga matumizi mapema kabla hujapata pesa

Kupanga matumizi yako mapema itakusaidia usipoteze pesa kwa mununuzi ambayo hujapangia.

Tabia ya kununua kitu kwasababu umekiona, ndio chanzo cha wengi kufanya matumizi ambayo hawakuyatarajia.

Itakuwa vyema ikiwa utafikiria kuhusu kuendesha fedha zako za kibinafsi kama biashara.

3. Usibane matumizi sana

Sababu moja ya watu kutengeneza bajeti ni kuhakikisha hawafanyi manunuzi nje ya bajeti.

Ukizuia matumizi yako kupita kiasi, utaasi tu na kununua vitu ambavyo haviko kwenye bajeti yako.

Badala yake, tumia mfumo wa 50/30/20. 50% ya mapato yako inapaswa kugharamia gharama/bili zako zinazohitajika au zisizobadilika

Asilimia 30 ya mapato yako yanapaswa kuwa ya vitu vya 'kujifurahisha' au matumizi yasiyo ya lazima, na 20% yawe ya malipo ya deni na akiba.

4. Fuatilia matumizi yako

Haiwezekani kuweka bajeti na kushikamana na malengo yako ya kifedha ikiwa hutafuatilia matumizi yako. Si lazima iwe kitu kigumu.

Unaweza kufuatilia matumizi yako kwa kalamu na karatasi ikiwa unafikiri utaandika kila kitu au unaweza kutumia programu inayosawazisha kila kitu kwenye akaunti yako ya benki na kufuatilia matumizi yako katika muda halisi.

5. Usikate tamaa kupanga bajeti ikiwa utakuwa na matumizi zaidi

Bajeti hutengenezwa lakini pia makosa hutokea. Ikiwa utafanya matumizi kupiti kiasi, haimaanishi kwamba huwezi kupanga na kufanya bajeti.

Unachoweza kufanya ni kuangalia, bajeti yako imezidi wapi na urekebishe wakati unaofuata.

Kwa mfano, ikiwa kukutana na marafiki kunakufanya uwe na matumizi kupita kiasi, unaweza kubadili mwenendo wako.

6. Hakikisha unapesa zinazoweza kukusaidia wakati wa dharura

Hakikisha unapesa zinazoweza kukusaidia wakati wa dharura kuanzia angalau miezi 3 hadi 6.

Hizi zitakusaidia ikiwa ghafla utapoteza kazi au utashindwa kufanya kazi. Utakuwa na pesa za kukusaidia kipindi unafikiria nini cha kufanya.

7. Kuwa na mpango wa kununua vitu ambavyo haviko kwenye orodha yako

Sote tuna hisi vibaya wakati umenunua bidhaa ambazo hazikuwa kwenye orodha yako, lakini ukitengeneza mpango wa kununua vitu ambavyo haviko kwenye orodha yako, utakuwa katika njia bora zaidi.

Jaribu mbinu ya kujipatia saa 48. Ukiona kitu ambacho hakipo kwenye orodha yako, jipe saa 48.

Ikiwa baada ya saa hizo utajiona bado unakihitaji, anza kufikiria namna ya kukipata. Lakini ikiwa utasahau kama wengine, hutakuwa na sababu ya kununua tena.

8. Hakikisha unawekeza

Ni vizuri pia kuwekeza kwa malengo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Malengo ya muda mfupi yanaweza kuwa yatakayo kuwezesha kununua vitu kama nyumba, gari na kadhalika.

Malengo ya muda mrefu kwa kawaida ni kuhusu kustaafu.

Usiwekeze bila kujua unachofanya

Leo ni rahisi zaidi kuliko hapo awali kuwekeza kwa kutumia simu au kompyuta yako, lakini isipokuwa kama unajua unajitosa katika kitu gani, usifanye hivyo.

Jifunze kadri uwezavyo kuhusu kuwekeza, kustahimili changamoto zinazoweza kutokea na kujiwekea ratiba.

Jua kile unachojihusisha nacho na kipi kibaya zaidi kinaweza kutokea. Zingatia ratiba, viwango vya riba na viwango vya chini vya uwekezaji.

Kuelewa jinsi ya kushughulikia fedha zako za kibinafsi ni ufunguo wa kutunza fedha zako.

Kuelewa jinsi mikopo inavyofanya kazi, jinsi ya kupanga bajeti, lini na jinsi ya kuwekeza, na jinsi ya kujua wakati unahitaji kupunguza matumizi kutakuwezesha kufikia malengo yako ya kifedha na kupata amani unapoelekea kustaafu.