Shule za kurekebisha tabia nchini Nigeria zatesa watu kama wanyama

Polisi nchini Nigeria wamegundua zaidi ya vijana 70 wakiwa wamefungwa katika shule binafsi ya kiislamu huko kaskazini mwa Nigeria.

Mamia ya vijana wametoroka katika shule mbalimbali za dini ya kiislamu katika siku za hivi karibuni.

Shule za bweni za kiislamu zinazojulikana kama Almajiris ni maarufu sana kwa waislamu wengi kaskazini mwa Nigeria.

Wazazi wanaowapeleka watoto wao katika shule hizo huwa wana matumaini ya kuwarekebisha tabia watoto wao kwa kupata elimu ya dini ya kiislamu.

Ingawa baadhi ya vijana waliookolewa katika vyuo hivyo wanadai kuteswa na kunyanyaswa kingono.

Rabiu Umar Galadima mwenye miaka 26 ni miongoni mwa vijana waliookolewa katika moja ya shule hizo huko mji wa Daura, eneo ambalo rais wa taifa hilo Muhammadu Buhari ametokea.

Galadima ameiambia BBC kuwa walikuwa wanatunzwa kama wanyama.

"Nilikuwa nachapwa fimbo 10 asubuhi, 10 mchana na jioni pia fimbo kumi, Nilikuwa nateswa, napigwa,nilikuwa kama mnyama",

Walimu wawili na mmiliki shule hiyo, mjini Daura, ambapo ndipo Rais Muhammadu Buhari amezaliwa, wamekamatwa.

Zaidi ya wanafunzi 300 waliandikishwa lakini wengi waliweza kutoroka kabla ya polisi kufika, mwandishi wa BBC Ishaq Khalid alisema.

Msemaji mkuu wa polisi kutoka Katsina aliiambia BBC kuwa matekwa hao walikuwa wakiandamana huku wengi wakiweza kutoka wakiwa bado na minyororo.

Shule hiyo imekuwa ikifanya kazi kwa miongo kadhaa kama sehemu ya mafunzo ya kitabu cha dini cha kiislam Quran na kufanya kazi na wanafunzi wenye matatizo ya kitabia.

Kumekuwa na ripoti nyingi za unyanyasaji katika shule za bweni za kiislam ndani ya kaskazini mwa Nigeria, huku wanafunzi muda mwingine wakilazimika kwenda mitaani na kuanza kuombaomba.

Unaweza pia kutazama: