Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Bondia mashuhuri Tanzania Thomas Mashali afariki
Bondia mashuhuri nchini Tanzania Thomas Mashali amefariki dunia katika hali ya kutatanisha mtaa wa Kimara, Dar es Salaam.
Taarifa zinasema mwanamasumbwi huyo aliuawa na watu wasiojulikana.
Kwa mujibu wa gazeti la Mwananchi la Tanzania, Mashali alishiriki kwenye kongamano la ngumi na kuchangia mada ya mabondia kunyanyaswa na mapromota kwenye mapambano.
Mwaka jana alifanya mazoezi mtaa wa Jericho mjini Nairobi akiwa na mabondia wengine wawili wakielekea Ulaya.
Mashali alizaliwa Septemba 9, 1989.
Kabla ya kufariki alikua ameshinda mapigano 19, akapoteza 5 na kwenda sare 1 na KO 4.
Alijiunga na ndondi za kulipwa mwaka wa 2009 na katika pigano lake la kwanza mwaka huo Novemba 11 alimshinda kwa KO Hamadu Mwalimu ukumbi wa Manzese Texas, Dar es Salaam.
Katika pigano la pili Aprili 4, Mashali, ambaye alikua anapigana uzani wa super middle, alienda sare na Karama Nyilawila ukumbi wa DDC Magomeni, Dar.
Pigano lake la mwisho kabla hajafa ni Septemba 12 mwaka huu alipomshinda Shabani Kaoneka kwa pointi huko Bagamoyo.