Moja kwa moja, Kuna dalili kwamba Iran inajaribu kufufua shughuli za nyuklia -JD Vance

''Ikiwa Iran itachukua hatua za kutengeneza upya silaha hizo, hali hiyo itakuwa changamoto kubwa kwetu'', anasema makamu wa rais wa Marekani.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Mariam mjahid

  1. Man United ilikataa kumsajili Osimhen 'kwasababu ya Afcon'

    Victor Osimhen alijiunga na klabu ya Galatasaray ya Uturuki kwa mkataba wa kudumu Julai mwaka jana, baada ya kusahauliwa na vilabu vya Premier League.

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Victor Osimhen alijiunga na klabu ya Galatasaray ya Uturuki kwa mkataba wa kudumu Julai mwaka jana, baada ya kusahauliwa na vilabu vya Premier League.

    Ratiba ya Kombe la mataifa Afrika (Afcon) ni moja ya sababu kuu zilizoifanya Manchester United kutofanya jaribio la kumsajili mshambuliaji Victor Osimhen, kwa mujibu wa aliyekuwa kocha wa timu ya kwanza wa klabu hiyo, Benni McCarthy.

    Osimhen, mshambuliaji wa Nigeria, alivutia vilabu vikubwa barani Ulaya baada ya kufunga mabao 26 ya ligi msimu wa 2022-23 na kuisaidia Napoli kutwaa ubingwa wa Italia kwa mara ya kwanza ndani ya miaka 33.

    McCarthy, aliyekuwa sehemu ya benchi la ufundi la Old Trafford chini ya aliyekuwa meneja Erik ten Hag, amesema alihusika katika mchakato wa kusaka washambuliaji na aliamini Osimhen “angefaa kikamilifu” ndani ya kikosi cha United.

    Hata hivyo, kufanyika kwa Afcon kila baada ya miaka miwili na mara nyingi katikati ya msimu wa soka Ulaya kuliifanya United kuelekeza macho kwa wachezaji wengine licha ya Osimhen kuwa “juu kabisa ya orodha” mwanzoni.

    “Ukitumia pauni milioni 100 kumsajili mchezaji, hutaki kumpoteza kwa mwezi mzima kutokana na Afcon,” McCarthy aliiambia BBC World Service.

    “Nadhani angefanikiwa sana pale. Lakini Afcon ilikuwa kikwazo kikubwa.

    “Kukosekana katika mechi nyingi muhimu, timu huathirika inapokosa mshambuliaji wake mkuu.

    “Hivyo uamuzi ukafanyika. Kwa kiasi kikubwa sana ilikuwa kwa sababu ya Afcon, na jina la Victor Osimhen likaondolewa kwenye orodha ya wachezaji waliokuwa wakivutia.”

    Badala yake, United ilimsajili Rasmus Højlund kutoka Atalanta kwa pauni milioni 72 Agosti 2023. Mshambuliaji huyo wa Denmark alifunga mabao 26 katika mechi 95 kabla ya kujiunga na Napoli kwa mkopo Septemba mwaka uliofuata.

    Osimhen, ambaye alitajwa kuwa Mwanasoka Bora wa Afrika mwaka 2023, aliondoka Napoli na kujiunga na Galatasaray kwa mkopo Septemba 2024, kabla ya kukamilisha uhamisho wa kudumu Julai mwaka uliofuata.

    McCarthy, ambaye sasa ni kocha mkuu wa timu ya soka ya Kenya, wenyeji wa Afcon 2027, anaamini mashindano hayo yanapaswa kuendelea kufanyika kila baada ya miaka miwili ili kuipa Afrika jukwaa la kuonesha vipaji vyake, lakini akasisitiza haja ya kupanga ratiba isiyogongana na mashindano ya vilabu.

    “Nafikiri Caf inapaswa kushirikiana vyema na Fifa na Uefa kupanga muda wa mashindano haya ili yasihatarishe taaluma za wachezaji,” alisema McCarthy mwenye umri wa miaka 48.

    “Yangeweza kufanyika wakati wa mapumziko rasmi ya ligi au dirisha la Juni–Julai baada ya msimu kumalizika.

    “Lakini pia hapo wachezaji hawapati mapumziko.

    “Kwa maoni yangu, hilo ndilo suluhisho bora, kwa sababu baadhi ya vilabu vinaepuka wachezaji wa Afrika kwa kuhofia kuwapoteza kwa mwezi mmoja wakati wa Afcon.

    “Naamini mashindano yabaki ya kila baada ya miaka miwili, lakini yafanyike wakati usiogongana na ratiba za vilabu.”

    Soma zaidi:

  2. Hezbollah: Shambulio dhidi ya Ali Khamenei ni “mstari mwekundu”

    F

    Chanzo cha picha, EPA

    Afisa mmoja wa Hezbollah nchini Lebanon amesema kundi hilo halitachukua hatua za kijeshi iwapo Marekani itafanya mashambulizi ya “kiwango cha chini” dhidi ya mfadhili wake mkuu, Iran. Hata hivyo, amesisitiza kuwa shambulio lolote litakalomlenga Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, litachukuliwa kuwa “mstari mwekundu”.

    Kauli hiyo inatolewa huku maafisa wa Lebanon wakieleza wasiwasi kwamba Hezbollah inaweza kujikuta ikihusishwa katika mzozo mpana wa kikanda endapo hatua ya Marekani dhidi ya Iran itachochea vita zaidi.

    Akizungumza na shirika la (AFP) kwa sharti la kutotajwa jina, afisa huyo alisema: “Iwapo mashambulizi yatakuwa ya kiwango cha chini, msimamo wa Hezbollah utasalia kuwa kutojihusisha kijeshi.”

    Iran ni mfadhili na mshirika mkuu wa Hezbollah, na kundi hilo limewahi kuonya hapo awali kuwa linaweza kuchukua hatua endapo Marekani itaishambulia Iran moja kwa moja.

    Wakati huo huo, Reuters liliripoti Jumanne (Februari 24), likinukuu maafisa wawili waandamizi wa serikali ya Lebanon ambao hawakutajwa majina, kwamba Israel ilituma ujumbe usio wa moja kwa moja kwa Beirut.

    Ujumbe huo ulionya kuwa iwapo Hezbollah itaingilia mzozo kati ya Marekani na Iran, Israel itajibu kwa mashambulizi makubwa dhidi ya Lebanon, yakilenga pia miundombinu ya kiraia, ikiwemo uwanja wa ndege.

    Unaweza kusoma pia:

  3. Mbegu za kiume huogelea kwa kasi zaidi majira ya joto - Utafiti

    g

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Ubora wa mbegu za kiume huwa wa juu zaidi kipindi cha majira ya joto na wa chini zaidi wakati wa majira ya baridi, kulingana na utafiti mpya.

    Watafiti kutoka Uingereza, Canada na Denmark walichambua sampuli za shahawa kutoka kwa wanaume 15,581 nchini Denmark na jimbo la Florida, wote wakiwa na umri kati ya miaka 18 na 45.

    Matokeo yao yanaonyesha kuwa uhamaji wa mbegu za kiume, yaani uwezo wa mbegu hizo kuogelea kwa ufanisi, ulikuwa wa juu zaidi mwezi Juni na Julai katika maeneo yote mawili ya utafiti.

    Kuelewa mabadiliko haya ya misimu kunaweza kusaidia kuboresha matibabu ya uzazi kwa kupanga vyema muda wa matibabu na vipimo vya uzazi, na hivyo kutoa mwongozo bora kwa wanandoa wanaotaka kupata mtoto.

    Utafiti huo, uliochapishwa katika jarida la Reproductive Biology and Endocrinology, unaonyesha kuwa viwango vya uhamaji wa mbegu za kiume hubaki sawa katika hali tofauti za tabianchi, lakini hubadilika kulingana na misimu.

    Viwango vilikuwa vya chini zaidi mwezi Desemba na Januari, hata katika jimbo la Florida ambako hali ya hewa hubaki ya joto mwaka mzima.

    Hata hivyo, wanasayansi hawakubaini mabadiliko katika jumla ya idadi ya mbegu za kiume (wingi wa mbegu katika shahawa) wala katika ujazo wa shahawa zinazotolewa wakati wa kumwaga, bila kujali msimu.

    Hii ina maana kuwa ingawa uwezo wa mbegu za kiume kuogelea hubadilika kulingana na msimu, muda wa mwaka hauathiri idadi ya mbegu zinazozalishwa.

    Matokeo haya yanaashiria kuwa mabadiliko ya misimu yanaweza kuathiri uwezo wa uzazi wa mwanaume zaidi ya tofauti za joto pekee.

    Kwa wastani, joto bora la korodani ambako mbegu za kiume huhifadhiwa linapaswa kuwa nyuzi joto mbili hadi nne chini ya joto la kawaida la mwili la nyuzi 37 za Selsiasi.

    Joto lililo juu au chini ya kiwango hicho linaweza kuathiri vibaya uhamaji wa mbegu za kiume, na hivyo kupunguza uwezo wa uzazi.

    Pia unaweza kusoma:

  4. Manchester United yapata faida, lakini deni lafikia pauni bilioni 1.3

    Manchester United wako nafasi ya nne katika klabu bingwa Ulaya

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Manchester United wako nafasi ya nne katika klabu bingwa Ulaya

    Afisa Mtendaji Mkuu wa Manchester United, Omar Berrada, amesema mageuzi yaliyofanywa nje ya uwanja sasa yanaanza kuzaa matunda kifedha, licha ya deni la klabu hiyo kupanda na kukaribia pauni bilioni 1.3.

    Kwa mujibu wa ripoti ya miezi sita iliyoishia Desemba 31, 2025, United imeandika faida ya uendeshaji ya pauni milioni 32.6, hatua kubwa ikilinganishwa na hasara ya pauni milioni 3.9 katika kipindi kama hicho mwaka uliopita.

    Hata hivyo, klabu hiyo iliongeza mkopo wa pauni milioni 25 kupitia mfumo wake wa mkopo wa muda, na kufanya jumla ya mkopo huo kufikia pauni milioni 295.7. Ukijumlisha deni la zamani lililotokana na ununuzi wa klabu na familia ya Glazer family pamoja na madeni ya zaidi ya pauni milioni 500 (hasa ada za uhamisho wa wachezaji ambazo bado hazijalipwa), United ilikuwa na jumla ya deni la pauni bilioni 1.29 mwishoni mwa mwaka jana.

    Gharama za kifedha zilishuka hadi pauni milioni 13.9 kutoka pauni milioni 37.6 mwaka uliotangulia nafuu kwa klabu hiyo.

    Mnamo Agosti 2025, mchambuzi wa masuala ya fedha za soka Swiss Ramble aliiweka Everton na Tottenham Hotspur juu ya United katika orodha ya klabu zenye madeni makubwa zaidi, ingawa klabu hizo zimekopa kwa ajili ya ujenzi wa viwanja vipya.

    United bado haijaweka wazi itakavyofadhili ujenzi wa uwanja wake mpya unaokadiriwa kugharimu zaidi ya pauni bilioni 2. Hali hiyo inaeleza kwa nini klabu hiyo ina shauku kubwa ya kurejea kwenye michuano ya UEFA Champions League baada ya kukosekana kwa misimu miwili.

    Mapato ya jumla yalifikia pauni milioni 190.3, huku mapato ya kibiashara yakishuka kwa asilimia 8 hadi pauni milioni 78.5. Kwa upande mwingine, matumizi ya mishahara yalipungua kwa asilimia 9 hadi pauni milioni 75.1.

    Ripoti hiyo haikugusia gharama za kumfuta kazi kocha mkuu Ruben Amorim, kwa kuwa uamuzi huo ulifanyika baada ya kipindi cha hesabu kumalizika.

    Berrada amesema: “Matokeo haya yanaonesha wazi athari chanya ya mageuzi yetu nje ya uwanja katika kupunguza gharama na kuongeza faida. Tunaendelea kuweka masuala ya soka mbele, huku tukisaka mafanikio makubwa kwa timu zetu za wanaume na wanawake.”

    Pia unaweza kusoma:

  5. Marekani yawekea Iran vikwazo vipya kabla ya duru ya mazungumzo kuanza

    G

    Chanzo cha picha, EPA

    Kabla ya kuanza kwa duru ya tatu ya mazungumzo kati ya Marekani na Iran, Washington imeitangazia Tehran vikwazo vipya vinavyolenga zaidi ya watu 30, taasisi na meli, kwa madai ya kuhusika katika “biashara haramu ya mafuta ya Iran” pamoja na “utengenezaji wa makombora ya masafa marefu na silaha za kisasa.”

    Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara ya Hazina ya Marekani, hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa “shinikizo la juu zaidi dhidi ya Iran,” unaolenga kudhoofisha vyanzo vya mapato na uwezo wa kijeshi wa taifa hilo.

    Vikwazo hivyo vinawalenga hasa wamiliki na waendeshaji wa meli zinazodaiwa kusafirisha mafuta ghafi ya Iran na bidhaa za petroli kwenda masoko ya kimataifa kinyume cha masharti ya kimataifa.

    Aidha, wizara hiyo imesema baadhi ya vikwazo vinahusu taasisi zinazofanya kazi kwa niaba ya Islamic Revolutionary Guard Corps (IRGC), Wizara ya Ulinzi ya Iran, pamoja na Kikosi cha Msaada wa Vikosi vya Silaha. Taasisi hizo zinadaiwa kuhusika katika usambazaji wa malighafi na mitambo nyeti inayotumika kurejesha na kuimarisha uwezo wa Iran wa kutengeneza makombora ya masafa marefu, silaha za kisasa za kawaida na ndege zisizo na rubani (droni).

    Katika taarifa yake, Waziri wa Hazina wa Marekani, Scott Bessent, aliwataja raia wanne wa Iran, Mohammad Abedini, Mehdi Zand, Mehrdad Jafari na Ebrahim Shariatzadeh, akidai kuwa walisafiri kwenda Urusi na Venezuela kutoa msaada wa kiufundi unaohusiana na teknolojia ya droni.

    Hatua hiyo inajiri katika kipindi ambacho juhudi za kidiplomasia kati ya pande hizo mbili zinaendelea, huku mvutano ukibaki juu kuhusu mpango wa nyuklia na shughuli za kijeshi za Iran.

    Soma Pia:

  6. Jordan yasema haitaruhusu anga yake kutumika na Marekani kwa "mvutano wa kikanda"

    .

    Chanzo cha picha, Anadolu via Getty

    Maelezo ya picha, Mfalme Abdallah wa Jordan

    Shirika la habari la serikali ya Jordan la Petra liliripoti Februari 24 kwamba Mfalme Abdullah II wa Jordan amesema kuwa nchi hiyo haitaruhusu ukiukaji wowote wa anga yake au matumizi yake katika mzozo wa kieneo, huku kukiwa na mvutano unaoongezeka kati ya Iran na Marekani.

    Mfalme Abdullah alisema katika mkutano na wajumbe wa Baraza la Chama cha Wanahabari wa Jordan: "Jordan haitaruhusu anga yake kukiukwa, na nchi hii haitakuwa eneo la vita."

    Aliongeza kuwa usalama wa Ufalme wa Yordani na usalama wa raia wake "ni muhimu zaidi."

    Mfalme wa Jordan alikariri kuwa mazungumzo na suluhisho la kisiasa ndio njia pekee ya kuzuia kuongezeka zaidi kwa mivutano ya kikanda.

    Matamshi yake yalirejelea kauli za awali za Waziri wa Mambo ya Nje wa Jordan Ayman Safadi, ambaye alisema Jordan itakabiliana na jaribio lolote la kukiuka anga yake.

    Serikali ya Jordan hapo awali ilikanusha shutuma kwamba Amman iliiruhusu Israel kutumia anga yake kushambulia vituo vya nyuklia vya Iran.

    Hapo awali BBC ilifahamu kuwa Uingereza haijairuhusu Marekani kutumia kambi zake za kijeshi kusaidia mashambulizi yanayoweza kutokea dhidi ya Iran.

    Marekani hapo awali imetumia kambi za Jeshi la Wanahewa la Uingereza huko Fairford huko Gloucestershire, kwenye ardhi ya Uingereza, na Diego Garcia, kwa operesheni katika Mashariki ya Kati.

    Diego Garcia ni kisiwa kikubwa zaidi katika Visiwa vya Chagos katika Bahari ya Hindi, ambapo kambi ya pamoja ya kijeshi ya Uingereza na Marekani iko.

  7. Marekani na Iran kufanya mazungumzo huku shinikizo la makubaliano ya nyuklia likiongezeka

    Duru ya mwisho ya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja ilifanyika katika makazi ya balozi wa Oman huko Geneva mnamo tarehe 17 Februari.

    Chanzo cha picha, EPA

    Maelezo ya picha, Duru ya mwisho ya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja ilifanyika katika makazi ya balozi wa Oman huko Geneva mnamo tarehe 17 Februari.

    Maafisa wa Marekani na Iran wanatarajiwa kukutana mjini Geneva leo Alhamisi kwa duru ya tatu ya mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja, wakati Rais Donald Trump akitishia kuishambulia Iran iwapo makubaliano ya nyuklia hayatapatikana.

    Mazungumzo hayo yanafanyika wakati Marekani ikiendelea na mkusanyiko mkubwa zaidi wa kijeshi katika Mashariki ya Kati tangu uvamizi ulioongozwa na Marekani wa Iraq mwaka 2003. Wakati huo huo, Iran imeapa kujibu kwa nguvu endapo itashambuliwa.

    Mazungumzo haya yanaonekana kama juhudi za mwisho kuzuia mgogoro wa kijeshi, ingawa uwezekano wa kufikiwa kwa makubaliano bado haujawa wazi. Ingawa Trump amesema anapendelea suluhisho la kidiplomasia, pia ameeleza kuwa anafikiria kufanya shambulio dogo la kijeshi ili kushinikiza viongozi wa Iran wakubali makubaliano.

    Hata hivyo, rais huyo hajaeleza kwa kina anachodai katika mazungumzo hayo, wala sababu ya kuchukua hatua za kijeshi sasa, miezi minane baada ya Marekani kushambulia vituo vya nyuklia vya Iran wakati wa vita kati ya Israel na Iran.

    Iran imekataa ombi la Marekani la kusitisha urutubishaji wa madini ya urani ndani ya mipaka yake. Hata hivyo, kumekuwepo na dalili kwamba iko tayari kutoa baadhi ya mapendekezo ya maelewano kuhusu mpango wake wa nyuklia.

    Kama ilivyokuwa katika duru mbili zilizopita zilizopatanishwa na Oman mapema mwezi huu, ujumbe wa Iran utaongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Abbas Araghchi. Kwa upande wa Marekani, watawakilishwa na mjumbe maalum Steve Witkoff pamoja na mkwe wa Trump, Jared Kushner.

    Katika wiki za karibuni, Marekani imetuma maelfu ya wanajeshi na kile Trump alichokiita “msafara mkubwa wa manowari” katika eneo hilo, ukiwemo meli mbili za kubeba ndege za kivita, meli nyingine za kijeshi, pamoja na ndege za kivita na za kuongeza mafuta angani.

    Kwa miongo kadhaa, Marekani na Israel zimeishutumu Iran kwa kujaribu kwa siri kutengeneza silaha ya nyuklia. Iran, hata hivyo, inasisitiza kuwa mpango wake ni wa matumizi ya amani tu, ingawa ndiyo nchi pekee isiyomiliki silaha za nyuklia ambayo imerutubisha urani kwa kiwango kinachokaribia kile cha kutengeneza silaha.

    Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, ameonya dhidi ya makubaliano yoyote yasiyojumuisha makombora ya masafa marefu ya Iran na makundi inayoyaunga mkono. Kwa muda mrefu, Netanyahu ameielezea Iran kama tishio kubwa kwa usalama wa Israel na chanzo cha kukosekana kwa utulivu katika eneo hilo.

    Wachambuzi wanaamini kuwa waziri mkuu huyo, ambaye alitembelea Ikulu ya Marekani mapema mwezi huu, huenda anasukuma ajenda ya kampeni yenye lengo la kuiondoa madarakani serikali ya Iran.

    Marekani ina hifadhi ya pili kwa ukubwa ya silaha za nyuklia duniani. Israel pia inaaminika kumiliki silaha za nyuklia, ingawa haithibitishi wala kukanusha rasmi.

    Kiongozi wa wachache katika bunge la Seneti Marekani, Chuck Schumer, alisema kwa ufupi: “Hili ni suala zito, na serikali inapaswa kueleza wazi msimamo wake kwa wananchi wa Marekani.”

    Soma zaidi:

  8. Kuna dalili kwamba Iran inajaribu kufufua shughuli za nyuklia -JD Vance

    Iran imekuwa ikisitiza mpango wake wa nyuklia ni wa amani

    Chanzo cha picha, NurPhoto via Getty Images

    Maelezo ya picha, Iran imekuwa ikisitiza mpango wake wa nyuklia ni wa amani

    “Hoja kuu ni wazi kabisa, Iran hairuhusiwi kumiliki silaha za nyuklia. Ikiwa itachukua hatua za kutengeneza upya silaha hizo, hali hiyo itakuwa changamoto kubwa kwetu. Kwa hakika, tumeshuhudia viashiria vinavyoonesha kuwa wanaelekea katika mkondo huo,” amesema JD Vance, Makamu wa Rais wa Marekani, kabla ya kuanza kwa duru mpya ya mazungumzo mjini Geneva.

    Makamu huyo wa Rais aliongeza: “Ndiyo sababu Rais ametuma wajumbe wa majadiliano ili kushughulikia suala hili. Kama alivyorudia mara kadhaa, anapendelea suluhu ipatikane kwa njia ya diplomasia; hata hivyo, bado kuna mbinu nyingine zinazoweza kuzingatiwa endapo itahitajika.”

    Katika saa zijazo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araqchi, anayeliongoza ujumbe wa kidiplomasia wa nchi yake, anatarajiwa kufanya mazungumzo na Steve Whittaker, mwakilishi maalum wa Donald Trump kwa Mashariki ya Kati, jijini Geneva, Uswisi, kwa upatanishi wa Oman.

    Soma Zaidi:

  9. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja ya tarehe 26/02/2026. Nakusihi ufuatilie hadi tamati.