Vita vya Ukraine: Zelensky asema Urusi imezidisha mashambulizi ya droni ndani ya wiki moja

Chanzo cha picha, Getty Images
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema Urusi imeongeza kasi ya mashambulizi dhidi ya nchi yake, ikitumia takriban droni 1,600 za mashambulizi, mabomu yaliyoongozwa karibu 1,100 na makombora matatu ndani ya wiki moja.
Zelensky amesema Moscow inalenga kuzidiwa kwa mifumo ya ulinzi wa anga ya Ukraine kupitia mashambulizi makubwa ya mfululizo, akisisitiza kuwa uwasilishaji wa makombora ya ulinzi kila siku bado ni wa muhimu. Ameongeza kuwa shinikizo la kimataifa dhidi ya Urusi haipaswi kulegezwa, akionya kuwa kupunguzwa kwa vikwazo kunaipa Urusi nafasi ya kuongeza fedha za kuendesha vita.
Wakati huohuo, Wizara ya Ulinzi ya Urusi imesema imeidungua jumla ya droni 215 za Ukraine katika usiku wa Ijumaa kuamkia Jumamosi, katika maeneo mbalimbali ya Urusi pamoja na Bahari ya Azov na Bahari Nyeusi.
Kwa mujibu wa wizara hiyo, droni hizo zilidunguliwa katika mikoa ya Belgorod, Bryansk, Voronezh, Kaluga, Kursk, Novgorod, Oryol, Pskov, Rostov, Smolensk, Tver na Tula, pamoja na mkoa wa Moscow, Krasnodar Krai, Crimea iliyounganishwa na Urusi, Bahari ya Azov na Bahari Nyeusi.
Soma zaidi:













