Mambo matano ambayo huenda hukuyajua kuhusu Hijja

Waislamu kutoka kote ulimwenguni wanafanya ibada wakisoma Quran Tukufu, na kuzunguka Kaaba ili kutimiza Hija yao huko Makka, Saudi Arabia.

Chanzo cha picha, Getty Images

Muda wa kusoma: Dakika 4

Hijja ni ibada takatifu kwa waumini wa dini ya Kiislamu na takriban watu milioni mbili huzuru mji mtakatifu wa Makka nchini Saudi Arabia kila mwaka kufanya ibada ya Hajj.

Ni moja ya nguzo tano za dini ya Kiislamu na kila Muumini aliye na uwezo anatarajiwa kuitimiza kwenda kuhiji walau mara moja katika kipindi cha maisha yake.

Hijja ni wapo ya mikusanyiko mikubwa ya kila mwaka duniani inayovutia waumini kutoka pembe zote za ulimwengu. Makka ndio mahali alipozaliwa Mtume Muhammad (SAW) na eneo ambalo alipokea ufunuo wa kwanza wa Kitabu Takatifu, Quran.

Pia ndiko kunapopatikana Kaaba, jengo lenye umbo la mchemraba lililofunikwa kwa kitambaa cheusi ambalo liko katikati ya Masjid al-Haram, linalojulikana pia kama Msikiti Mtakatifu au Msikiti Mkubwa wa Makka, ambao unachukuliwa kuwa mahali patakatifu zaidi katika Uislamu.

Yajue mambo matano ya kipekee kuhusu ibada ya Hijja ambayo huenda hukuyajua.

Kaaba - Urithi wa Nabii Ibrahim

Pia unaweza kusoma:

Ibada ya Hija ya kila mwaka ni moja ya nguzo za Uislamu, yenye kuhusishwa na Mtume Muhammad (SAW), mwanzilishi wa dini hiyo.

Mahujaji hufanya ibada ya Tawaf ambayo ni kuzunguka Kaaba, eneo takatifu zaidi katika Uislamu, huko Masjid al-Haram.

Chanzo cha picha, EPA

Maelezo ya picha, Zaidi ya mahujaji milioni 1.8 walikwenda kuhiji mnamo 2024, kulingana na Data Saudi - jukwaa la kuwasilisha na kuchambua data za kiuchumi na kijamii Saudi Arabia.

Hata hivyo, ibada hiyo ilianzia wakati wa Nabii Ibrahim, ambaye inaaminika ndio chanzo cha jengo la Kaaba, kulingana na Imani ya Kiisilamu.

Tamaduni za Hijja zinaadhimisha kipindi ambapo nusra Nabii Ibrahim amchinje mwanawe akimtii Mwenyezi Mungu - kitendo cha kujitolea ambacho kilimalizika kwa Mungu kuingilia kati.

Nabii Ibrahim, anayejulikana kama Abrahamu katika Ukristo na Uyahudi, pia ni kiungo muhimu katika imani hizo zote mbili.

Hakuna kutengwa kwa misingi ya kijinsia

Tunisian prospective pilgrims wait for boarding to the flight for Hajj

Chanzo cha picha, Yassine Gaidi/Anadolu Agency

Maelezo ya picha, Wakati wa ibada ya Hijja, wanaume na wanawake hufanya ibada inayofanana, kwa wakati mmoja na mahali sawa, mara nyingi huwa kando na kando tu.

Tofauti na ibada zingine za Waislamu ambapo kila jinsia hufanya ibada ikiwa sehemu yake kama vile kutumia milango tofauti au kusali kwenye maeneo tofauti msikitini, hakuna ubaguzi wa kijinsia kati ya wanaume na wanawake wakati wa ibada ya Hijja.

Mavazi ya kipekee

Mahujaji wanaofanya ibada ya Hijja hufuata miongozo maalum ya mavazi ambayo yanaonyesha usawa wa kiroho na unyenyekevu.

Muslims perform Umrah in Mecca, Saudi Arabia - 27 Jan 2023

Chanzo cha picha, EPA

Maelezo ya picha, Mahujaji wa kike hawavai mavazi meupe kama ilivyo kwa mahujaji wa kiume

Mahujaji wa kiume huvaa vazi jeupe, lisilo na mshono, linaloitwa Ihram, kuashiria usawa wa waumini wote, bila kujali hali ya kijamii au kiuchumi.

Mahujaji wa kike hawavai mavazi meupe kama ya wanaume, lakini wanaweza kuvaa mavazi yoyote yasiyowabana, ya kawaida tu ambayo yanawastiri.

Wanapaswa kufunika vichwa vyao kwa hijab, lakini nyuso zao zinapaswa kusalia wazi wakati wa Hijja.

Kupanda mlima

Mojawapo ya ibada maarufu za Hijja ni Tawaf, ambapo mahujaji huzunguka Kaaba mara saba - mwanzoni na mwisho wa ibada ya Hijja.

Lakini je! ulijua kuwa ibada nyingine muhimu inajumuisha kutembea kati ya vilima viwili?

Sehemu ya ibada ya Hijja ni pamoja na kuzuru na kutembea mara saba kati ya vilima vya Safa na Marwah, vilivyo ndani ya Masjid al-Haram.

Inachukuliwa kuwa kitendo cha kukumbuka changamoto na uvumilivu wa Hajar, mke wa Nabii Ibrahim, ambaye alikimbia kati ya vilima hivyo viwili akitafuta maji kwa ajili ya mtoto wake mchanga.

Kilele cha Mlima Arafat

Wakati Kaaba ndio msingi wa ibada ya Hijja, kilele chake hufanyika huko Mlima Arafat, bonde la jangwa lililo nje ya Makka.

A Muslim woman prays on Mount Arafat during the Hajj 2023 pilgrimage, southeast of Mecca, Saudi Arabia, 27 June 2023.

Chanzo cha picha, EPA

Maelezo ya picha, Mahujaji hukusanyika kwenye maeneo tambarare ya Mlima Arafat kwa siku kufanya sala

Hapa, umati mkubwa wa waumini hukusanyika kuanzia jua linachomoza hadi linapotua huku wakifanya sala, kutafakari, na kusoma tena na tena Quran.

Maeneo haya takatifu yana umuhimu mkubwa katika Uislamu. Kulingana na imani ya Kiisilamu ni mahali ambapo Mtume Muhammad alitoa mahubiri yake ya mwisho.