Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

'Urusi inakubaliana na wazo la kumaliza vita Ukraine'- Putin

Putin alikuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara ya mgeni wake kiongozi wa Belarus, Alexander Lukashenko, kuhusu pendekezo lililotolewa na Marekani la kusitisha mapigano kwa siku 30

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Lizzy Masinga & Dinah Gahamanyi & Mariam Mjahid

  1. Makamu wa Rais Zanzibar Othman Masoud, Lissu wazuiwa kuingia Angola

    Viongozi zaidi 40 kutoka nchi mbalimbali afrika akiwemo Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar, na mwenyekiti wa Chama cha upinzani cha ACT nchini Tanzania, Othman Masoud Othman wamezuiwa kuingia nchini Angola na mamlaka za Sereikali nchini humo.

    Taarifa iliyotolewa na chama cha ACT inasema, makamu huyo alizuiwa katika uwanja wa ndege pamoja na kiongozi mkuu wa chama hicho, Dorothy Semu.

    ‘Viongozi hao wanashikiliwa kwenye uwanja wa ndege wa Luanda na hati zao za kusafiria zinashikiliwa'. Ilisema sehemu ya taarifa ya chama hicho kilichotaka pia Ofisi ya Ubalozi wa Angola nchini Tanzania, kutoa maelezo ya kilichotokea.

    Viongozi wengine waliozuiwa ni Pamoja na rais wa zamani wa Botswana, Ian Khama, Waziri mkuu wa zamani wa Lesotho, mwenyekiti wa chama kikuu cha Upinzani Tanzania, CHADEMA, Tundu Lissu, Kiongozi wa upinzani Uganda, Robert Kyagulanyi (Bbobi Wine), na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna.

    Sifuna alithibitisha kupiti mtandao wake wa X, ‘ Tulialikwa na Rais wa UNITA, Adalberto Costa nchini Angola. Serikali imetuzuia kuingia’.

    Kwa upande wake Lissu aliandika ‘ kilichofanywa na mamlaka za uhamiaji za Angola hakikubaliki na kinapaswa kulaaniwa’.

    Viongozi hao walikuwa sehemu ya viongozi zaidi ya 40 walizuiliwa ambao waliwasili Angola kushiriki katika mazungumzo ya siku nne ya jukwaa la Demokrasia Afrika, yaliyoandaliwa na Taasisi ya The Brenthurst Foundation, ambayo yalikuwa yaanze leo Machi 13 mpaka 16.

    Mamlaka za Angola, hazijajitokeza kueleza kwa upande wao, licha ya jitihada za upande wa pili kutaka maelezo yao.

  2. 'Urusi inakubaliana kumaliza vita Ukraine kwa njia ya amani'- Putin

    Rais wa Urusi, Vladimir Putin anasema nchi yake inakubaliana na kusitisha mapigano na Ukraine lakini hatua hiyo inapaswa kuleta "amani ya kudumu na kuondoa sababu za msingi za mzozo huu."

    Putin alikuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara ya mgeni wake kiongozi wa Belarus, Alexander Lukashenko.

    Awali, Kremlin ilisema kuwa iko katika hatua za mwisho za operesheni ya kuiondoa Ukraine kutoka maeneo iliyoyateka huko Kursk.

    Mjumbe wa Donald Trump, Steve Witkoff, yuko Moscow akiwakilisha Marekani katika mazungumzo yake na Urusi kuhusu pendekezo la kusitisha mapigano kwa siku 30.

    "Nani atatoa amri ya kusitisha mapigano, na amri hizi zitakuwa na thamani gani?" anauliza Putin. akiongeza swali lingine nani ataamua ni wapi "ukiukaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano unawezekana kutokea" katika mpaka wa kilomita 2000, akimaanisha urefu wa mpaka kati ya Urusi na Ukraine.

    "Masuala haya yote yanahitaji kuchunguzwa kwa kina na pande zote mbili," anasema, akiongeza kuwa wazo la kusitisha mapigano ni "zuri na tunaliunga mkono kabisa lakini kuna masuala yanayohitaji kujadiliwa."

    Putin anasema anaamini kuwa "tunapaswa kujadiliana na wenzetu wa Marekani na washirika wetu" na "pengine" atafanya mazungumzo ya simu na Rais wa Marekani, Donald Trump.

    "Wazo lenyewe la kumaliza mgogoro huu kwa njia za amani, tunaliunga mkono."

  3. Ethiopia na Eritrea zinakaribia kuingia vitani, maafisa wa Tigray wanaonya

    Maadui wa muda mrefu, Ethiopia na Eritrea, wanaweza kuwa wanakaribia kuingia vita, maafisa katika eneo lenye machafuko la Ethiopia ambalo liko katikati ya mzozo huo wameonya.

    Hilo likitokea huenda likasababisha janga jingine la kibinadamu katika Pembe ya Afrika.

    Mapigano ya moja kwa moja kati ya majeshi mawili makubwa zaidi barani Afrika yangepaswa kuwa pigo la mwisho kwa maridhiano ya kihistoria ambayo yalimpa Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed, Tuzo ya Amani ya Nobel mwaka 2019, na yanaweza kuvutia mataifa mengine ya kikanda, wachambuzi wamesema.

    Vita hivyo pia vinaweza kuzua mgogoro mwingine katika eneo ambalo kupunguzwa kwa misaada kumeathiri juhudi za kusaidia mamilioni ya watu waliokumbwa na migogoro ya ndani nchini Sudan, Somalia, na Ethiopia.

    "Wakati wowote vita kati ya Ethiopia na Eritrea vinaweza kuanza," Jenerali Tsadkan Gebretensae, makamu wa rais katika serikali ya mpito ya Tigray, aliandika katika jarida, The Africa Report, siku ya Jumatatu.

    Vita vya wenyewe kwa wenyewe vya 2020-2022 huko Tigray kati ya Chama cha Ukombozi wa Watu wa Tigray (TPLF) na serikali kuu ya Ethiopia vilisababisha vifo vya mamia ya maelfu ya watu.

    Hofu ya kuzuka kwa vita vipya inahusiana na mgawanyiko wa TPLF mwaka jana, ambapo baadhi ya wanachama wake sasa wanatawala Tigray kwa baraka za serikali ya shirikisho ya Ethiopia, huku wengine wakipinga utawala huo.

    Siku ya Jumanne, kundi la waasi ambalo Tsadkan amelishutumu kwa kutafuta muungano na Eritrea, liliteka mji wa kaskazini wa Adigrat.

    Kwa upande wake, Getachew Reda, mkuu wa utawala wa mpito wa Tigray, aliomba msaada wa serikali dhidi ya waasi hao, ambao wanakanusha kuwa na uhusiano na Eritrea.

    "Kuna uhasama wa wazi kati ya Ethiopia na Eritrea," Getachew aliwaambia waandishi wa habari siku ya Jumatatu. "Kinachonitia wasiwasi ni kwamba watu wa Tigray wanaweza tena kuwa waathirika wa vita nyingine".

  4. Urusi yakataa mpango wa kusitisha mapigano kwa siku 30

    Urusi mekataa pendekezo la Marekani kuhusu usitishaji wa mapigano nchini Ukraine kwa muda wa siku 30.

    Mshauri wa mambo ya nje wa Rais Vladmir Putin, Yuri Ushakov amesema kukubali siku 30 za kusitisha mapigano ni suluhisho la muda mfupi

    Akiwa anaongea na vyombo vya habari vya Urusi asubuhi ya leo, Ushakov ameweka wazi msimamo wa Urusi kuhusu pendekezo la kusitisha mapigano kwa siku 30. Kwa ufupi, Ushakov amelipinga, akisema kuwa halitakuwa chochote zaidi ya kuwa la muda mfupi na litaipa fursa jeshi la Ukraine kujipanga upya.

    Ameongeza kuwa Urusi inatafuta "makubaliano ya amani ya muda mrefu nchini Ukraine ambayo yatazingatia maslahi na wasiwasi wa Moscow," na akaeleza kuwa "majadiliano ya kawaida ya maoni" kati ya Urusi na Marekani yanafanyika "kwa utulivu."

    Mjumbe wa Donald Trump, Steve Witkoff, amewasili Moscow tayari kwa mazungumzo na Urusi kuhusu kusitishwa kwa mapigano kwa muda nchini Ukraine, kwa mujibu wa ripoti ya CBS News, mshirika wa BBC nchini Marekani.

    Pamoja na kuwasili kwa mjumbe huyo, Ushakov pia amesema kuwa Marekani inaelewa kuwa uanachama wa Ukraine katika NATO hauwezekani.

    Kama balozi wa zamani wa Urusi nchini Marekani, Yuri Ushakov mwenye umri wa miaka 77, anaelewa vyema jinsi ya kuzungumza na Washington. Siku chache kabla ya uvamizi wa Urusi kwa Ukraine mnamo 2022, alishutumu utawala wa Biden kwa kudai kuwa wanajeshi wa Urusi walikuwa wanajiandaa kwenda vitani. Lakini siku chache tu baada ya Donald Trump kurejea Ikulu ya White House, alionekana kuwa mwepesi zaidi wa mazungumzo – na akaweka wazi kuwa Urusi iko tayari kwa mazungumzo iwapo Marekani itatuma "wawakilishi husika".

    Badala yake, Urusi imesema inataka mpango wa usitishaji wa mapigano wa kudumu ambao utajadili na kuzingatia maslahi ya Moscow. ikiwa ni pamoja na kuizuia Ukraine kuwa mwanachama wa muungano wa NATO.

    pia unaweza kusoma:

  5. SADC kuondoa Vikosi vyake DRC

    Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamekubaliana kusitisha zoezi la kutuma vikosi vya kijeshi nchini DR Congo katika mkutano uliofanyika leo Zimbabwe.

    Uamuzi huu unahitimisha operesheni ya Umoja wa SADC nchini DRC, iliyokuwa na lengo la kusaidia vikosi vya kijeshi vya Congo kudhibiti hali ya usalama katika mikoa ya Mashariki mwa nchi hiyo.

    Katika mkutano huo maalum ulioongozwa na Rais Emmeson Mnangagwa wa Zimbambwe, viongozi wa SADC walionyesha wasiwasi mkubwa kuhusu hali ya usalama inayozidi kuzorota katika mashariki mwa DRC licha yakuwepo kwa vikosi vya kijeshi vya SADC.

    Hali hii inajumuisha kutekwa kwa miji muhimu kama Goma na Bukavu, pamoja na kuzuiliwa kwa njia kuu za usambazaji wa misaada ya kibinadamu na kuwa vigumu kufikia wakimbizi wa ndani kwa ndani.

    Licha ya uamuzi wa kuondoa vikosi Congo, SADC imesisitiza itaendelea kusaidia serikali ya Jamuhuri ya Congo na kusisitiza kuwa suluhu ya kudumu inahitaji jopo pana la ushirikiano wa kisiasa na kidiplomasia, ambalo litahusisha pande zote, ikiwemo serikali, makundi yasiyo ya kiserikali, na wanamgambo wa M23.

    Kuondolewa kwa vikosi vya SADC kumejiri baada ya miaka mingi ya juhudi za kudumisha usalama, ingawa hali ya usalama haionekani kuboreka kwa haraka.

    Viongozi wa SADC pia walikumbuka na kutoa heshima kwa wanajeshi waliopoteza maisha wakiwa katika operesheni hiyo, wakituma risala za rambirambi na kuwatakia afueni y aharaka wanajeshi wanaouguza majeraha.

    Rais Félix Antoine Tshisekedi wa DRC alieleza shukrani za dhati kwa SADC kwa msaada wake wa muda mrefu katika kukabiliana na changamoto za usalama nchini mwake, huku akikaribisha uamuzi wa kuanza mchakato wa kuondoa vikosi.

    Aidha, kikao hicho cha SADC kilitambua uongozi bora wa Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania na Rais Emmerson Mnangagwa wa Zimbabwe, ambao walionekana kuwa na mchango mkubwa katika kuratibu ajenda ya amani na usalama katika eneo la SADC.

    Soma pia:

  6. Urusi yadai kuudhibiti mji muhimu wa Kursk huko Ukraine

    Saa chache baada ya ujumbe wa Marekani kutangaza unaelekea Moscow kujadili uwezekano wa kusitisha mapigano nchini Ukraine, Kremlin imedai imeutwaa tena mkoa wa Kursk ambao ulikuwa chini ya ulinzi wa wanajeshi wa Ukraine.

    Katika mapigano ambayo yamekuwa yakiendelea watu watatu wameuawa na 14 kujeruhiwa vibaya baada ya Urusi kuvamia eneo la Donetsk lililoko mashariki mwa Ukraine, Afisa wa mkoa huo Vadym Filashkin atoa taarifa hiyo.

    Kwa mujibu wa afisa huyo, zaidi ya makazi mia moja yameharibiwa vibaya.

    Katika eneo la kusini mwa Kherson, mzee wa miaka 68 ameuawa katika shambulizi la kombora lililotumwa na Urusi kugonga makazi ya watu.

    Huduma ya dharura ya serikali ya Ukraine DSNS inasema, maeneo ya makazi ya nje ya mkoa wa Kherson yalipata "shambulio kubwa" usiku wa kuamkia leo, na juhudi zake za kuzima moto uliosababishwa zilitatizwa na mashambulizi ya kufuatana.

    Wanajeshi wa Urusi wamedai wamedhibiti eneo la Sudzha, mji muhimu katika eneo la Kursk ambao umekuwa umekaliwa na wanajeshi wa Ukraine.

    Hata hivyo, BBC haijahakiki madai haya, na pia Ukraine haijazungumzia utekaji huo.

    Haya yanajiri baada ya Kremlin kuthibitisha kuwa Rais Vladimir Putin alitembelea eneo la Kursk nchini Urusi siku ya Jumatano, sehemu ambazo zimekuwa chini ya udhibiti wa Ukraine tangu uvamizi mwaka jana.

    Kufuatia ziara yake Kursk, vyombo vya habari vya Urusi viliripoti kuwa ilikuwa ni maagizo kutoka kwa Putin kwa wanajeshi wa Moscow wadhibiti eneo hilo haraka iwezekanavyo.

    Hatua hii ikiashiria dhamira ya Putin kuteka eneo hilo ili isitumike katika meza ya maridhiano na Ukraine muda utakapowadia.

    Haya yakijiri Putin na Kremlin pia hawajatoa hisia wala kujibu kuhusu mkutano wa Ukraine na Marekani ulioafikiana kuwe na usitishaji wa mapigano kwa muda wa mwezi mmoja.

    Mkuu wa majeshi wa Ukraine, Oleksandr Syrsky amefichua kuwa baadhi ya vikosi vyake vilikuwa vikijiondoa kutoka Kursk.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Tanzania kuongeza matumizi kwa 13% katika mwaka ujao wa fedha

    Tanzania inatarajia kuongeza matumizi kwa 13.4% katika mwaka wa kifedha kuanzia Julai, kulingana na rasimu ya bajeti inayolenga mahitaji ya malipo ya deni la nchi, gharama za uchaguzi mkuu ujao, na kusitishwa kwa msaada wa kigeni kutoka kwa Rais wa Marekani Donald Trump.

    Nchi hiyo ya Afrika Mashariki inatarajia kutumia shilingi trilioni 57.04 ($22 bilioni) katika miezi 12 kuanzia Julai, mwaka huu kutoka shilingi trilioni 50.29 mwaka wa fedha 2024/2025, kwa mujibu wa nyaraka ya bajeti iliyoonwa na Reuters.

    Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba alitoa taarifa iliyopewa jina "Rasimu ya Bajeti na Matumizi kwa Mwaka 2025/26" kwa kamati ya bunge siku ya Jumanne.

    Bajeti kamili ya mwaka ujao wa kifedha itasomwa mwezi Juni.

    Kati ya kiasi hicho cha jumla, serikali inatarajia kukusanya shilingi trilioni 40.97 kutoka kwenye vyanzo vya mapato ya ndani na kilichobaki kupitia deni la ndani na nje, kwa mujibu wa nyaraka hiyo.

    Tanzania inachukua hatua za kupunguza utegemezi wake kwenye vyanzo visivyo na uhakika vya mapato au deni lenye masharti yasiyofaa, nyaraka hiyo ilieleza.

    Kama baadhi ya nchi nyingine zinazoendelea, Tanzania pia imeathiriwa vibaya na kusitishwa kwa msaada kutoka kwa Rais wa Marekani Donald Trump kwa siku 90.

    Bajeti hiyo imezingatia, hati ilisema, "athari zinazoweza kutokea kutokana na mabadiliko ya sera kutoka kwa washirika wa maendeleo, hasa Marekani."

    Katika mwaka ujao wa kifedha, serikali itajikita katika kuongeza uzalishaji wa bidhaa na huduma za viwandani, na kukuza biashara na uwekezaji pamoja na mambo mengine, ilisema.

    "Vipaumbele maalum ni pamoja na kugharamia malipo ya deni la serikali, mishahara, uchaguzi mkuu wa 2025 na kukuza demokrasia nchini," Nchemba alisema kwenye hati hiyo.

    Tanzania inatarajia kufanya uchaguzi mkuu Oktoba ambapo wapiga kura watachagua rais mpya, wabunge na viongozi wa serikali za mitaa.

    Rais Samia Suluhu Hassan atagombea uchaguzi kwa muhula wa pili wa miaka mitano, baada ya kuingia madarakani mwaka 2021 kufuatia kifo cha mtangulizi wake.

    Soma pia;

  8. M23, Serikali ya DRC kukutanishwa rasmi wiki ijayo Angola

    Mazungumzo ya amani ya ana kwa ana baina ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na waasi wa M23 yanatarajiwa kuanza katika mji mkuu wa Angola, Luanda, tarehe 18 Machi, kwa mujibu wa raisi wa Angola katika taarifa iliyotolewa Jumatano.

    Nchi hiyo ya kusini mwa Afrika imekuwa ikijaribu kusimamia makubaliano ya amani ya kudumu na kupunguza mvutano kati ya Congo na jirani yake Rwanda, ambayo imekumbwa na tuhuma za kuunga mkono kundi la waasi.

    Hata hivyo Rwanda inakanusha tuhuma hizo.

    Angola ilitangaza Jumatano kuwa itajaribu kuweka mazingira ya mazungumzo ya moja kwa moja ana kwa ana.

    Serikali ya Congo imekataa mara kwa mara kushiriki katika mazungumzo na M23, ambapo siku ya Jumatano ilisema kuwa imepokea mwaliko wa Angola lakini haikuthibitisha ushiriki wake.

    Siku ya Jumatano, Tina Salama, msemaji wa Rais wa Congo Felix Tshisekedi, aliiambia Reuters kuwa serikali imepokea mwaliko kutoka Angola lakini haikuthibitisha ushiriki wake.

    Kiongozi wa M23, Bertrand Bisimwa, aliandika katika mtandao wa X akijivunia kumlazimisha Tshisekedi kukaa kwenye meza ya mazungumzo, alisema kuwa ni "uamuzi pekee w kiungwana kutatua mgogoro wa sasa" ambao umeongezeka kwa kiasi kikubwa tangu Januari.

    Waasi wamedhibiti miji miwili mikubwa ya mashariki mwa Congo tangu Januari, ikiwa ni ongezeko la mgogoro huo wa muda mrefu ulioanza kutokana na mchanganyiko wa mauaji ya kimbari ya 1994 ya Rwanda na harakati za kudhibiti rasilimali kubwa za madini ya Congo.

    Serikali ya Congo imesema watu wasiopungua 7,000 wamefariki katika mapigano tangu Januari.

    Zaidi ya watu 600,000 wamekimbia makazi yao kutokana na mapigano tangu Novemba, kwa mujibu wa ofisi ya masuala ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa.

    Nchi Jirani za DR Congo, ikiwa ni pamoja na Afrika Kusini, Burundi, na Uganda, wana wanajeshi mashariki mwa nchi hiyo, jambo linaloleta wasiwasi kuhusu vita kamili vya kikanda vinavyofanana na vita vya Congo vya miaka ya 1990 na mapema 2000 ambavyo viliua mamilioni ya watu.

    Soma pia;

  9. Wakaazi wa Italia wakesha baada ya mtetemeko wa ardhi kutokea

    Watu wengi ndani na viungani mwa mji wa Naples uliyoko Italia wamekesha usiku mzima kwa baridi na wengine katika magari baada ya zilizala ya ardhi kutetemesha makazi yao na kuharibu majengo.

    Wanasayansi wa tetemeko la ardhi kutoka Italia wamesema kuwa mtetemeko wa ukubwa wa 4.4 ulitokea saa 01:25 Alhamisi, kwa kina kifupi cha kilomita 3 (maili mbili), kando ya pwani kati ya Pozzuoli na Bagnoli.

    Mtetemeko huu ulisikika kote mjini Naples na kusababisha usumbufu mkubwa katika usambazaji wa umeme katika baadhi ya maeneo ya jiji hilo.

    Katika eneo la Bagnoli, karibu na kitovu cha mtetemeko, mwanamke aliokolewa kutoka kwa vifusi vya nyumba na sasa anatibu majeraha madogo.

    Naples inapatikana juu ya Campi Flegrei, bonde la volkano linalofanya eneo hili la kusini mwa Italia kuwa na hatari ya kutokea kwa matetemeko ya ardhi mara kwa mara.

    Ilifuatiwa na mitetemeko sita dhaifu zaidi.

    Watu walitoroka nyumba zao na kukusanyika katika mitaa ya Naples, wakiogopa tetemeko zaidi.

    Mnara wa kengele wa kanisa la mtaa uliharibiwa na magari kadhaa yalivunjwa vioo vyao vya mbele.

    Huko Pozzuoli, mkazi mmoja aliiambia TV ya Italia kwamba wakaazi walikuwa na wasiwasi kwamba mitetemeko ya miaka miwili iliyopita iliashiria "jambo tofauti na lililotokea hapo awali".

    Kando ya pwani, Meya wa Bacoli, Josi Gerardo Della Ragione, alisema umekuwa usiku mgumu, ingawa mji wake haujapata uharibifu.

    Waziri Mkuu Giorgia Meloni alikuwa akifuatilia hali hiyo kila mara na alikuwa akiwasiliana kwa karibu na wenzake, maafisa wake walisema.

    katika maenoe mengine Shule zilifungwa Alhamisi ili ukaguzi wa uthabiti wa jengo ufanyike kabla ya masomo kurejea.

    Pia unaweza kusoma:

  10. Usiku wa kwanza wa Duterte akiwa jela ni wakati muhimu kwa ICC

    Nje ya kizuizi cha Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), ambako rais wa zamani wa Ufilipino Rodrigo Duterte alipelekwa Jumatano, wafuasi wake walikusanyika, wakipeperusha bendera za taifa na kupiga kelele, "Mrudisheni!" huku akipitishwa kupitia milango ya chuma yenye nguvu kwa kasi.

    Muda mfupi kabla ya kutua nchini Uholanzi, mzee huyo mwenye umri wa miaka 79 bila kuomba msamaha alitetea "vita vyake vya umwagaji damu dhidi ya dawa za kulevya" ambavyo ICC inasema kuna "sababu nzuri" za kumfungulia mashtaka ya mauaji kama uhalifu dhidi ya ubinadamu.

    Wafanyabiashara wadogo wa madawa ya kulevya, watumiaji na wengine waliuawa bila kesi kwenye akiwa meya na, baadaye rais.

    Idadi rasmi inafikia 6,000, ingawa wanaharakati wanaamini kuwa idadi halisi inaweza kufikia makumi ya maelfu.

    Duterte alisema alipambana na wafanyabiashara wa dawa za kulevya ili kuondoa uhalifu wa mitaani nchini.

    Hata hivyo, mashirika ya kutetea haki za binadamu yanadai kuwa kampeni hiyo ilijaa dhuluma za polisi, zikiwalenga vijana kutoka jamii maskini wa mijini.

    Duterte ndiye mkuu wa zamani wa nchi ya Asia kushtakiwa na ICC - na mshukiwa wa kwanza kupelekwa The Hague katika kipindi cha miaka mitatu.

    Unaweza kusoma;

  11. Mzozo wa DRC: Wakuu wa nchi za SADC kukutana leo kwa mkutano maalumu

    Mkutano maalum wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) unakutana kwa njia ya video Alhamisi hii kujadili hali ya DR Congo.

    Mkutano huo, unaoongozwa na Rais Emmerson Mnangagwa wa Zimbabwe - ambaye kwa sasa ni mkuu wa SADC - unajadili suala la wanajeshi wa SADC waliotumwa katika ujumbe unaojulikana kama SAMIDRC, ambao wametumwa Goma.

    Mkutano wa leo unafuatia maazimio ya mikutano wa 'Organ Troika' - chombo kinachohusika na masuala ya siasa na usalama katika SADC - uliokutana Alhamisi iliyopita, chini ya uenyekiti wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, anayeongoza chombo hicho, kujadili suala la askari wa SADC nchini DRC

    Zaidi ya wanajeshi 1,000 wanaaminika kutumwa na Afrika Kusini, Malawi na Tanzania na wako katika kambi za Goma na vitongoji vyake huko Mubambiro, ambapo wanalindwa na kundi la waasi la M23.

    Wanajeshi hawa waliokuwa wametumwa na nchi hizi kusaidia jeshi la DR Congo, waliweka silaha chini baada ya kushindwa katika vita vya kuulinda mji wa Goma, ambao ulitekwa na M23 mwishoni mwa mwezi wa Januari.

    Tangu mji huo kutekwa, mustakabali wa askari hawa haueleweki.

    Mwezi uliopita, vuguvugu la M23 lilikubali kuiruhusu miili 14 ya Waafrika Kusini waliouawa katika mapigano hayo, pamoja na baadhi ya waliohitaji matibabu, kurejeshwa katika nchi zao kupitia Rwanda.

    Baadhi ya wanajeshi hawa bado wako ndani na karibu na Goma, wakilindwa na M23, kwa zaidi ya mwezi mmoja baada ya kushindwa vitani.

    Unaweza pia kusoma:

  12. Ujumbe wa Marekani waelekea Moscow kwa mazungumzo kuhusu Ukraine huku Putin akizuru Kursk

    Maafisa wa Marekani wanaelekea Urusi kujadili uwezekano wa kusitisha mapigano nchini Ukraine, kwa mujibu wa Rais Donald Trump.

    Habari hizi zinakuja baada ya maafisa wa Ukraine kukubaliana kusitisha mapigano kwa siku 30 kufuatia mkutano uliotarajiwa na maafisa wa Marekani nchini Saudi Arabia.

    Hapo awali, Waziri wa Mambo ya Nje Marco Rubio alisema kwamba "Jambo hili liko kwenye mikono ya [Urusi]" na kwamba Marekani inaamini kuwa njia pekee ya kumaliza mapigano hayo ni mazungumzo ya amani.

    Ziara ya Marekani inakuja huku Kremlin ikidai kuwa Rais Vladimir Putin alitembelea eneo la Kursk nchini Urusi, sehemu ambazo zimekuwa chini ya udhibiti wa Ukraine tangu uvamizi wa mwaka jana.

    Kufuatia mkutano wa Jeddah siku ya Jumanne, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alisema sasa ni juu ya Marekani kuishawishi Urusi kukubaliana na pendekezo hilo "chanya".

    Ikulu ya Kremlin imesema inachunguza mpango wa kusitisha mapigano, na kwamba mazungumzo ya simu kati ya Trump na Putin yanawezekana.

    Unaweza kusoma;

  13. Mtu aitwaye Bombshell aibua vita vikali vya urithi wa kisiasa nchini Zimbabwe

    Msafara mrefu wa mizinga ya jeshi ikipita kupitia mtaa mmoja wa Harare ulisababisha hofu - kwa muda mfupi, kwamba mapinduzi ya kijeshi yalikuwa yanakaribia kutokea nchini Zimbabwe.

    "Mambo yanakwenda vipi Zimbabwe?" aliandika mtu mmoja kwenye mitandao ya kijamii. Mwingine alisema: "Mara ya mwisho ilipotokea hivi, kulikuwa na mapinduzi."

    Msemaji wa serikali, Nick Mangwana, alikimbilia kuwatuliza hofu, akieleza kwamba mizinga ilikuwa katika mji mkuu asubuhi hiyo ya katikati ya mwezi Februari kama sehemu ya mazoezi ya kawaida"hakuna haja ya kuwa na wasiwasi kuhusu hilo."

    Hata hivyo, maneno na uvumi yaliendelea, yakionesha mengi kuhusu hali ya nchi.

    Kabla ya zoezi hilo la kijeshi, Rais Emmerson Mnangagwa alikumbana na ukosoaji mkali kwa mara ya kwanza tangu kuchukua madaraka mwaka 2017, kuhusu uongozi wake kutoka ndani ya chama chake cha Zanu-PF, huku kukiwa na wito wa kumtaka ajiuzulu.

    Madai haya yalikumbusha nyakati za awali kabla ya mapinduzi yaliyomng'oa mtangulizi wake, kiongozi wa muda mrefu Robert Mugabe.

    Mnangagwa alikamata madaraka mwaka 1980 kama shujaa wa mapinduzi aliyemaliza utawala wa mkoloni wa wachache weupe. Lakini kifo cha kisiasa cha Mugabe kilianza kutabiriwa wakati veterani wa vita vya uhuru vya miaka ya 1970 walipoondoa msaada wao kwake.

  14. Wakatoliki waaadhimisha kumbukumbu ya miaka 12 ya Papa kwa kumuombea apone

    Wakatoliki duniani kote wanaadhimisha kumbukumbu ya miaka 12 tangu Papa Francis kuchaguliwa kuwa papa kwa kumuombea apone.

    Francis, ambaye alichaguliwa tarehe 13 Machi 2013, amekuwa katika hospitali ya Gemelli ya Roma kwa karibu mwezi mmoja. Ametibiwa mara mbili homa ya mapafu na maambukizo mengine, na amepata matatizo ya kupumua mara kadhaa , ambayo yalizua wasiwasi juu ya maisha yake.

    Taarifa za hivi punde kutoka Vatican zimesema mzee huyo mwenye umri wa miaka 88 yuko imara baada ya picha ya X-ray ya kifua kuthibitisha "kuboreka" kwa hali yake katika siku za hivi karibuni.

    Lakini walisema hali yake bado ni tata na kwamba alihitaji matibabu zaidi hospitalini. Haijabainika ni lini ataruhusiwa kuondoka.

    "Hali ya kiafya ya Baba Mtakatifu imesalia kuwa shwari katika muktadha wa picha tata ya matibabu," ilisema taarifa iliyochapishwa na Vatican News.

    Kipimo cha "X-ray ya kifua kilichofanywa [siku ya Jumanne] kimethibitisha unafuu wake ulioonekana katika siku zilizopita," ilisema.

    "Hali ya kiafya ya Baba Mtakatifu imesalia kuwa shwari katika muktadha wa picha tata ya matibabu," ilisema taarifa iliyochapishwa na Vatican News.

    Unaweza pia kusoma:

  15. Iran yakataa mazungumzo ya nyuklia huku UAE ikipokea barua ya Trump

    Kiongozi mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei amekataa wazo la mazungumzo na Marekani kuhusu mpango wake wa nyuklia, huku Tehran ikithibitisha kupokea barua kutoka kwa Rais Donald Trump.

    Wiki iliyopita, Trump alisema barua hiyo ilipendekeza mazungumzo kuhusu makubaliano ambayo yataizuia Iran kupata silaha za nyuklia na kuepusha uwezekano wa kuchukuliwa kwa hatua za kijeshi dhidi yake.

    Ingawa Khamenei alisema hajaiona barua hiyo, ambayo iliwasilishwa na afisa kutoka Umoja wa Falme za Kiarabu, alipuuzilia mbali kuwa ni "udanganyifu wa maoni ya umma".

    "Tunapojua hawataiheshimu, kuna umuhimu gani wa kufanya mazungumzo?" aliuliza, akirejelea uamuzi wa Trump wa kuachana na mapatano ya nyuklia ya Iran ya mwaka 2015 katika muhula wake wa kwanza.

    Ameonya kuwa Iran italipiza kisasi endapo litatokea shambulio kwenye vituo vyake vya nyuklia.

    "Iran haitafuti vita, lakini ikiwa Wamarekani au mawakala wao watachukua hatua mbaya, jibu letu litakuwa la uhakika na la uhakika, na ambaye atapata madhara zaidi ni Marekani," amesema.

    Kiongozi huyo mkuu, ambaye ndiye mwenye uamuzi wa mwisho kuhusu masuala yote ya serikali, pia alisisitiza kwamba Iran "haipendezwi na silaha za nyuklia".

    Unaweza pia kusoma:

  16. Hujambo na karibu kwa matangazo haya ya mubashara ya Jumatano tarere 13.03.2025, tukikuletea habari za kikanda na kimataifa