Rubani akiri kumuua mkewe baada ya kufichuliwa na teknolojia

Chanzo cha picha, Instagram/Babis Anagnostopoulos
Rubani mwenye umri wa miaka 33 raia wa Ugiriki amekiri kumuua mke wake raia wa Uingereza, polisi wamethibitisha.
Rubani huyo Babis Anagnostopoulos alikamatwa na polisi katika kisiwa cha Alonnisos, mara baada ya ibada ya kumbukizi ya maisha ya marehemu mkewe, bi Caroline Crouch.
Awali rubani huyo, alidai kuwa majambazi watatu walivamia nyumba yao jijini Athens na kumfunga kamba. Hata hivyo baada ya uchunguzi wa muda mrefu, polisi wanasema walibaini kuwa maelezo ya bwana huyo yalikuwa na walakini.
Polisi hawakupata ushahidi ama dalili ya kuthibitisha kuwa genge hilo la majambazi lilivamia nyumba yake na kumpiga na kisha kumkaba mkewe na kuiba Euro 15,000.

Chanzo cha picha, Alpha TV
Baada ya hapo polisi wakakagua vifaa mbalimbali vya teknolojia ili kuthibitisha maelezo ya rubani huyo. Saa ya Bi Caroline inayosoma mapigo ya moyo ilitoa ripoti ya namna gani mapigo yak e yalikuwa siku aliyofariki.
Mienendo ya mume katika siku ya mauaji pia ilifuatiliwa kupitia simu yake ya mkononi na mfumo wa kamera za nyumba yao pia zikaonesha walakini.
Japo rubani huyo alidai kuwa alifungwa mikono wakati mkewe akiuawa, polisi wanasema aliwkuwa akitumia simu yake.
Bi Caroline, 20, aliyeuawa akiwa na miaka 20 alizaliwa Uingereza na kuhamia Ugiriki akiwa mdogo pamoja na wazazi wake. Alikuwa akiishi na mumewe na mtoto mdogo jijini Athens alipouawa Mei 11.

Polisi awali walitangaza donge nono la Euro laki tatu kwa mtu ambaye angewabaini wauaji hao.
Siku tano baada ya kifo cha mkewe, rubani huyo alituma ujumbe katika mtandao wa kijamii wa Instagram uliombatana na picha ya mkewe siku ya harusi yao akisema: "Tutakuwa pamoja milele, Kwaheri mpenzi wangu."

Chanzo cha picha, Instagram/Babis Anagnostopoulos
Makachero walimchukua rubani hiyo siku ya Alhamisi baada ya kumbukizi ya maisha ya mkewe wakimwambia kuwa wamepata taarifa mpya na muhimu kuhusu kesi hiyo na kumtaka kwenda kumtambua mshukiwa mmoja.
Mara tu baada ya kufika Athens aliarifiwa kuwa yeye ndiye mshukiwa.
Alikiri kutenda mauaji hayo baada ya saa nane za mahijiano, waneleza polisi. Kuna ripoti kuwa aliwaeleza polisi kuwa walikuwa wakilumbana sana na mkewe katika siku za hivi karibuni.
Kesi iliyoitikisa Ugiriki
Mauaji hayo yamekuwa maarufu nchini Ugiriki. Awali yalizua mjadala juu ya usalama wa makazi ya watu, huku mume akidai ni genge la wageni ndio liliwashambulia.
Bwana mmoja raia wa Georgia alikamatwa katika siku za mwanzo za uchunguzi baada tu ya kuingia nchi jirani ya Bulgaria.

Chanzo cha picha, Alpha TV
Runinga ya Taifa ilikatiza matangazo mubashara ya kandanda ya Euro 2020 jana Alhamisi ili kuuhabarisha umma juu ya kukiri kwa rubani huyo kumuua mkewe.
Magari na watembea kwa miguu walisimama nje ya migahawa katika jiji la Athens ili kutazama taarifa hiyo ikitangazwa, kwa mujibu ripota wa BBC Kostas Koukoumakas.













