Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Virusi vya Corona: Jinsi Iran inavyokabiliana na corona
Idadi ya maambukizi ya virusi vya corona nchini Iran inazidi kuongezeka huku watu wakiwa wanahoji namna ambavyo serikali inakabiliana na janga hili.
Lakini nini kinaendelea nchini humo kwa sasa.
Watu wangapi wameathirika na virusi hivyo?
Iran inaongoza kwa kuwa na vifo vingi vinavyotokana na corona, ukiachilia mbali China na idadi inadaiwa kuongezeka zaidi.
Kikosi cha Shirika la afya duniani (WHO) kitaenda Iran mwishoni mwa wiki hii kuangalia hali ilivyo na kutoa msaada.
Rais wa Iran Hassan Rouhani alisema kuwa hakuna haja ya kuweka miji au mitaa katika karantine.
Mjini Qom, ambao ndio kitovu cha mlipuko wa ugonjwa huo, maeneo ya mkusanyiko wa ibada bado yako wazi.
Kukamatwa kwa 'waeneza uvumi'
Shirika la habari la Iran na AFP yameripoti kwamba Polisi wa Iran wamewakamata watu 24 wanaoshukiwa kueneza uvumi kuhusu virusi vya Corona kwenye mtandao.
Mkuu wa jeshi la polisi la Irani Vahid Majid amesema watumiaji wa mtandao 118 walihojiwa na kuachiliwa baada ya kupewa onyo.
Je! Iran ina vifaa vya kutosha vya matibabu?
Shirika la afya duniani ,WHO inasambaza vifaa vya utambuzi na vifaa vya kinga kwa wafanyakazi wa afya nchini Iran.
Msemaji wa wizara ya afya ya Iran amesema WHO imesafirisha mizigo minne ya aina hiyo mpaka sasa.
Rais wa nchi hiyo wengi wana wasiwasi kuhusu ukosefu wa vifaa.
Msafirishaji wa vifaa hivyo nchini Irani, amesema kuwa hawezi kununua vifaa vya upimaji kwa sababu ya vikwazo vilivyowekwa na Marekani, kulingana na ripoti za nchini humo.
Ramin Fallah, mjumbe wa bodi ya Chama cha waagizaji wa vifaa vya matibabu alinukuliwa akiliambia shirika la habari la Iran kwamba, "Kampuni nyingi za kimataifa ziko tayari kuipatia Iran vifaa vya kupima virusi vya Corona, lakini tumeshindwa kuwatumia pesa,".
Marekani imedai kwamba vikwazo vyake vinazuia uwezo wa Iran kununua vifaa vya matibabu, ikiashiria msamaha wa bidhaa za kibinadamu.
Lakini Iran inasema kampuni zinaona ugumu wa kufanya malipo kwa sababu mabenki hayataki kuvunja sheria za Marekani ili kuepuka vikwazo.
Je! Kuhusu vifaa vya kufunika pua na mdomo?
Kama ilivyo katika nchi nyingine zilizo na milipuko ya virusi hivyo, Wairani wamekuwa wakijitokeza kwenye maduka ya dawa kununua vifaa hivyo pamoja na dawa za matibabu.
Bei ya bidhaa hizi, ambazo zinapatikana kwa uchache, zimepanda mara 10.
Watu wengi wamelalamika kwenye vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kwamba uhaba wa barakoa unatokana na kwamba mamilioni ya vifaa hivyo vilipelekwa China wiki chache zilizopita.
Kulingana na shirika la habari la Iran, nchi hiyo imetuma barakoa milioni tatu kwa China "kama ishara ya urafiki wa muda mrefu na wa jadi kati ya nchi hizo mbili".
Ripoti hizo pia zinaonesha kampuni za kichina zikinunua idadi kubwa ya vifaa hivyo kutoka Iran na kusababisha uhaba katika soko la nchi hiyo.
Serikali ya Iran sasa imesema imepiga marufuku usafirishaji wa barakoa kwa muda wa miezi mitatu huku ikiamuru viwanda vyake kuongeza uzalishaji.
Je! Watu wanaondoka nchini humo?
Iran haijapiga marufuku kuingia kwa wageni, lakini nchi kadhaa za jirani kama Uturuki, Pakistan na Iraq, zimefunga mipaka yao.
Uturuki na Falme za Kiarabu zimesimamisha ndege zote kutoka Iran.
Serikali ya Iran imesema ndege za kwenda China zilisimamishwa tarehe 2 Februari.
Lakini, rekodi za ndege zinaonesha kumekuwa na angalau ndege tisa kati ya Iran na China tangu wakati huo.