Je utaweza kustahamili safari ya ndege ya saa 19?

Boeing 787-9 Dreamliner from Qantas

Chanzo cha picha, Getty Images

Shirika la ndege la nchini Australia la Qantas litafanya majaribio ya safari za saa 19 ili kuona kama abiria na wahudumu wanaweza kustahamili safari hizo za mbali.

Shirika hilo linataka kufanya safari za moja kwa moja kutoka jiji la Sydney kwenda London na kutoka Sydney kwenda New York kufikia 2022.

Safari hizo zikifanikiwa ndizo zitakuwa za mbali zaidi za moja kwa moja duniani.

Safari za majaribio zitaanza baadae mwaka huu, na ndege zitabeba abiria 40 ambao afya zao zitakuwa zikiangaliwa kwa muda wote wa safari.

Mkurugenzi mtendaji wa Qantas Alan Joyce amesema safari za moja kwa moja kutoka pwani ya mashariki ya Australia kwenda London na New York zinafungua "ukurasa wa mwisho wa safari za ndege".

"Safari za mbali sana za ndege zinaibua maswali mengi ya msingi juu ya afya na raha kwa abiria na wahudumu," Bw Joyce amesema.

Safari hizo mbili za London na New York zinatarajiwa kuwa na muda saa 19, kulingana na hali ya hewa.

Safari tatu za majaribio zitafanyika ambazo zitahusisha wafanyakazi wa shirika hilo tu - ambao wote watavalishwa vifaa maalumu vya kiteknolojia ambavyo vitakagua hali ya afya zao kwa muda wote wa safari.

Muda wa kulala, chakula na vinywaji vyote vitakaguliwa ili kuona athari za kiafya namna mwili utakavyoendana na mabadiliko.

Safari hizo zitatumia aina ya ndege za Boeing 787-9.

Baada ya majaribio, shirika hilo litafanya maamuzi ya kuanzisha safari hizo ama la mwishoni mwa mwaka huu.

Safari za mbali zaidi za ndege

Ndege
Presentational white space

Safari za mbali za ndege kwa sasa ni eneo ambalo mashirika makubwa ya ndege wanachuana katika kuhudumia wateja.

Shirika la Ndege la Singapore mwaka jana lilizindua safari ya saa 18 na dakika 25 kutoka Singapore mpaka New York, ambayo kwa sasa ndiyo safari ndefu zaidi ya ndege duniani.

Mwaka jana pia, Qantas ilizindua safari ya saa 17 kutoka Perth kwenda London, wakati Qatar inafanya safari ya saa 17 pia baina ya Auckland na Doha.