Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Sakata la Korosho: Je, shinikizo la kisiasa limemng'oa Hawa Ghasia Kamati ya Bajeti?
Maswali na mjadala umeibuka juu ya hatua ya kujiuzulu viongozi wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, mwenyekiti Hawa Ghasia na naibu wake Jitu Soni.
Ghasia ambaye ni mbunge wa Mtwara Vijijini na Soni mbunge wa Babati Vijini wote kupitia chama tawala CCM walitangaza uamuzi wao mbele ya wajumbe wa kamati hiyo jana Jumanne asubuhi jijini Dodoma bila kutoa sababu za kufikia maamuzi hayo tena kwa pamoja.
BBC ilifanya jitihada za kuzungumza na Bi Ghasia na kutaka atumiwe ujumbe mfupi ambao hata hivyo hakuujibu.
Katibu wa Bunge Stephen Kagaigai ameliambia gazeti la kila siku la Kingereza Tanzania The Citizen kuwa ofisi yake licha ya kupokea taarifa za kujiuzulu nyadhifa za wabunge hao lakini hawana taarifa juu ya sababu ya uamuzi huo.
Bi Ghasia hatahivyo hwa ufupi kabisa aliliambia Gazeti la Mwananchi kuwa,"Mimi nimejiuzulu kwa hiari yangu, sitaki kuzungumza na waandishi wa habari, 'full Stop'. Mbona nilivyochaguliwa hamkuja kunihoji nini malengo yangu lakini sasa nimemaliza mnataka kunihoji."
Kamati ya Bajeti ambayo inanguvu ya kikanuni kuibana serikali katika masuala ya kibajeti chini ya uongozi wa Bi Ghasia itakumbukwa kwa namna ilivyoibana serikali katika vipindi tofauti ikitaka mabadiliko ya kibajeti.
Mwezi Juni mwaka huu kamati hiyo iliongoza wabunge bila kujali tofauti zao za kisiasa katika kupinga mapendekezo ya serikali katika Sheria ya Fedha wa mwaka 2018 kwa kuchukua asilimia 100 ya tozo za mauzo ya korosho nje ya nchi (Export levy) kupelekwa mfuko mkuu wa fedha za serikali.
Awali, asilimia 65 ya tozo hiyo ilikuwa ianenda kwenye mfuko wa zao hilo na baadae kurejeshwa kwa wakulima kupitia pembejeo. Hoja ya wabunge wakiongozwa na kamati ya bajeti ilikuwa, hatua ya kuchukua fedha zote ingeleta athari kubwa kwa maendeleo ya zao hilo na wakulima wake.
Mjadala ukawa mkali lakini hoja ya serikali ikapita. Baadae, Rai John Magufuli akasema hakupendezwa na namna ya wabunge wa CCM hususani wa mikoa ya kusini kwa namna walivyolijadili suala hilo, na akatishia kuwa laiti wangeliandamana basi angetuma askari wawaadhibu.
Kutokana na mjadala wa korosho, wadadisi wa masuala ya kisiasa na baadhi ya wabunge wakausifu msimao wa Ghasia na kamati yake.
Akizungumzia juu ya kujiuzulu kwa Ghasia Mbunge wa Kigoma Mjini ACT Zitto kabwe kupitia ukurasa wake wa twitter alisema, "Nimesikitishwa sana na uamuzi Huu. Kamati ya Bajeti ya Hawa Ghasia ilikuwa imeanza kurejesha heshima ya Bunge. Ndio Siasa za zama hizi. Asante sana Hawa kwa kazi uliyofanya."
Je, kuna shinikizo la kisiasa?
Kuna ambao wanaamini kuwa viongozi hao wameshurutishwa kujiuzulu kutokana na msimamo wao imara juu ya sakata la korosho.
Gazeti la Mwananchi limedai kudokezwa na chanzo ambacho hawakukutaja jina kuwa uamozi wa Ghasia na Soni haukuwa wa hiyari. Huku mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema kupitia mtandao wake wa twitter pia ameashiria kuwa kulikuwa na shinikizo.
"Mkti Kamati ya Bajeti ya Bunge Hawa Ghasia /Makamu wake wamejiuzulu Uongozi kwa ridhaa yao ?ebu tuone huko mbele ya safari,pengine vichwa vya habari vitakuja kubadilika na kusema Hawa Ghasia na Makamu wake watakiwa kujiuzulu Uongozi Kamati ya Bajeti ya Bunge.Najaribu kuwaza tu," aliandika Lema.
Mwezi Machi 2017, mwenyekiti wa kamati ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira, Dk Dalali Kafumu na makamu wake, Vicky Kamata kwa pamoja walitangaza kujiuzulu nafasi zao.
Wawili hao hata hivyo hawakuficha sababu zao kwa kuweka wazi kuwa walichukua uamuzi huo kutokana na Serikali kuingilia majukumu yao katika utendaji kazi.
Baada ya kujiuzulu kwa Ghasia na Soni, , wajumbe wa kamati ya bajeti walimchagua mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene kuwa mwenyekiti na mbunge wa Maswa Magharibi, Mashimba Ndaki kuwa makamu, wote wawili ni kutoka upande wa CCM.