Jitihada za uokoaji zinaendelea Ugiriki baada ya moto kuua watu 74, watu walikimbilia baharini

Jitihada za uokoaji zinaendelea huko nchini Ugiriki, ambako moto mkubwa uliwaka kuzunguka maeneo ya mji na vijiji karibu na mji mkuu Athens.
Wafanyakazi wa dharura waliokuwa wakifanya shughuli za uokoaji wanaelezea matukio ya uharibifu uliotokana na moto huo ikiwemo kuteketea kwa msitu pamoja na magari yaliyokuwa katika maeneo hayo.
Takribani watu 74 wamethibitishwa kufariki lakini idadi ya watu ambao waliopotea bado haijajulikana.

Chanzo cha picha, Kalogerikos Nikos


Chanzo cha picha, Getty Images
Katika kisa kimoja miili 26 iligunduliwa kwa pamoja ikiwa juu ya mwamba pembezoni mwa bahari katika eneo la Mati, moja kati ya miji iliyoathirika zaidi.
Wakazi wanasema walilazimika kukimbilia baharini kujiokoa walipoona wamezingirwa na moto huo.
Baadhi hawakuweza kufika baharini kwa wakati.
Mamlaka katika mji huo zina mashaka kuhusiana na chanzo cha moto huo na kwamba huenda umesababishwa makusudi.
Waziri mkuu wa Ugiriki Alex Tsipras amesema janga hilo limeathiri nchi nzima.
''Nchi inapitia katika wakati mgumu sana. Mamia ya watu wamefariki na hili linamuumiza kila mmoja haswa kwa familia zilizopoteza wapendwa wao. Leo Ugiriki inaomboleza, na kwa kumbukumbu ya wale wote waliofariki tunatangaza siku tatu za maombolezo.'' Alisema Tsipras.

Katika eneo la Neos Voutzas karibu na mji wa Mati, wakaazi walikua wakitizama mabaki ya nyumba zao.
Theofilaktos Logothetis ni mmoja wao na anasema alikua mmoja wa wale waliokua wa mwisho kabisa kutoka nyumbani kabla ya miale ya moto kufika kwa majirani zake.

Chanzo cha picha, EPA

''Moto ni kama ulikuwa unatukimbiza, aliyekua anaweza kuondoka kabla haujafika ilikua bahati. Mtu aliyekua kulia kwangu nilipokua nikiendesha kuelekea barabara kuu aliunguzwa mpaka akawa mkaa.''
Serikali ya Ugiriki inasema kuna uwezekano mkubwa watu wengi zaidi wakawa wamefariki katika kisa hicho ambacho kimeacha simanzi kwa nchi nzima.
Siku tatu za maombolezo zimetangazwa nchini humo.












