Mkataba wa nyuklia wa Iran: Ufaransa yaishutumu Marekani kwa kuiwekea vikwazo Iran

Chapa za kampuni za Airbus na Renault

Chanzo cha picha, Reuters/AFP

Maelezo ya picha, Kampuni mbili ambazo huenda zikaathiriwa vibaya na vikwazo vya Marekani

Ufaransa imesema kuwa haitokubali hatua ya Marekani kuziwekea vikwazo kampuni zinazofanya biashara na Iran.

Kitendo hicho cha Washington kinajiri kufuatia hatua ya rais Donald Trump kujiondoa katika makubaliano ya kihistoria ya kusitisha mpango wa kinyuklia wa Iran.

Waziri wa maswala ya kigeni nchini Ufaransa Jean-Yves Le Drian alisema kuwa kampuni za Ulaya hazifai kuathirika kutokana na uamuzi wa Marekani.

Marekani inasema kuwa kampuni zina miezi sita kusitisha biashara na hazitaruhusiwa kuandikisha kandarasi mpya la sivyo zikabiliwe na vikwazo.

Je bwana Le Drian amesema nini?

Katika mahojiano na gazeti la Le Perisien waziri huyo wa maswala ya kigeni alisema: Tunahisi kwamba hatua ya kupita mipaka ya vikwazo hivyo haitakubalika. Raia wa Ulaya hawafai kuathirika na hatua ya Marekani kujiondoa katika makubaliano ambayo wao wenyewe walishiriki.

Waziri wa maswala ya kigeni nchini Ufaransa Jean-Yves Le Drian

Chanzo cha picha, AFP

Maelezo ya picha, Bwana Le Drian alisema kuwa uamuzi wa washirika wengine katika makubaliano hayo lazima uheshimiwe

Alisema kuwa vikwazo hivyo vipya vitaathiri Marekani na Ulaya itaweka mikakati ya kulinda maslahi ya kampuni zake na kuanza kujadiliana na Washington kuhusu swala hilo.

Bwana Le Drian alisema kuwa uamuzi wa washirika wengine kuhusu makubaliano hayo ni lazima uheshimiwe.

Alisema kuwa athari za hatua hiyo ya Marekani tayari zimeanza kuhisiwa kutokana na kupanda kwa bei ya mafuta na hali ya wasiwasi ya kisiasa katika eneo la mashariki ya kati.

Ufaransa, Uingereza na Ujerumani zote zimesema kuwa zitafanya kazi na Iran ili kujaribu kuokoa makubaliano hayo.

Waziri wa uchumi nchini Ujerumani Peter Altmaier amesema kuwa atafanya kazi na kampuni zilizoathiriwa ili kujaribu kupunguza madhara mabaya ya uamuzi huo wa Marekani.

Marekani kuiwekea vikwazo Iran baada ya Trump kutangaza kujiondoa katika mkataba wa kinyuklia na taifa hilo

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Marekani kuiwekea vikwazo Iran baada ya Trump kutangaza kujiondoa katika mkataba wa kinyuklia na taifa hilo

Ni kampuni gani zitakazoathirika?

Baadhi ya kampuni za Ufaransa zimetia kandarasi zenye thamani ya mabilioni ya madola na Iran tangu mkaubaliano hayo ya kinyuklia yaafikiwe 2015.

Kampuni hizo zinashirikisha Airbus, kampuni ya mafuta ya Total na kampuni za magari zaRenault na Peugeot.

Zitalazimika kufunga uwekezaji wake kufikia mwezi Novemba la sivyo zikabiliwe na vikwazo.

Je ni hali gani ya kisiasa iliopo mashariki ya kati?

Mfano wa hivi karibuni ni vita kati ya Iran na Israel nchini Syria.

Israel imevishutumu vikosi vya Kikurdi kitengo cha majini cha Iran Revolutionary Guard Corps (IRGC) - kwa kurusha makombora 20 ya roketi nchini Israel siku ya Alhamisi

Israel ilisema kuwa wapiganaji wake baadaye walishambulia maeneo sabini ya kijeshi ya Iran nchini Syria .

Hatua ya Iran kupeleka wanajeshi wake nchini Syria kumsaidia rais Bashar al-Assad imeikasirisha Israel.