Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kiongozi aliyekamatwa kwa kuhusishwa na kiapo cha Raila aachiliwa
Mbunge wa eneo bunge la Ruaraka nchini Kenya aliyehusishwa na kiapo cha kiongozi wa upinzani nchini humo Raila Odinga amewachiliwa kwa dhamana ya ksh.50,000 baada ya kulala katika seli za kituo cha polisi.
Tom Kajwang alifikishwa katika mahakama ya Milimani jijini Nairobi Alhamisi jioni ambapo alitarajiwa kukabiliwa na mashtaka yanayohusiana na kushiriki katika mkutano na kula kiapo kinyume na sheria.
Wabunge wa Nasa waliojaa katika mahakama hiyo walisema kuwa mashtaka aliyowekewa Kajwang ni bandia.
Kajwang alilala katika kituo cha polisi cha Kiambu baada ya kukamatwa siku ya Jumatano kwa kile maafisa wanasema ni jukumu lake katika sherehe ya kuapishwa kwa Raila Odinga kuwa 'rais wa wananchi'.
Mbunge huyo ambaye alisimama nyuma ya Raila wakati wa hafla hiyo iliofanyika katika uwanja wa Uhuru Park Jijini Nairobi alikamatwa katika mahakama ya Milimani jijini Nairobi na kupelekwa makao makuu ya ujasusi ili kuhojiwa.
Kesi yake itaendelea tarehe 6 wiki Ijayo.