Wakristo na Waislamu waonyesha umoja Kibera Kenya

Waumini wanapaka msikiti rangi ya njano

Chanzo cha picha, Colour in Faith

Maelezo ya picha, Waumini wanapaka msikiti rangi ya njano
    • Author, Anthony Irungu
    • Nafasi, BBC Africa, Nairobi

Makanisa na misikiti katika kitongoji duni cha kibera jijini Nairobi yanapata umbo jipya, baada ya kupakwa rangi ya manjano kama ishara ya umoja na uwiano baina ya waislamu na wakristo.

Mradi huo unaoendelezwa katika kitongoji duni cha kibera mjini Nairobi, ambacho ndiyo mojawapo ya mtaa mkubwa wa mabanda barani Africa, unalenga kuangamiza dhana ya ubabe wa kidini, unaosababisha mivutano na ugaidi miongoni mwa vijana kwa misingi ya dini.

Mradi huo, colour-in-faith unatumia sanaa kubadilisha jamii, na lengo la waasisi ni kuusambaza kote nchini Kenya.

Kasisi Albert Loresha katika kanisa la ACK holy Trinity Parish Kibera

Chanzo cha picha, Colour in Faith

Maelezo ya picha, Kasisi Albert Loresha katika kanisa la ACK holy Trinity Parish Kibera

Kasisi Albert Loresha aliyeongoza zoezi la kupaka rangi anasema, ulikuwa wakati wa kufahamiana kati ya waislamu na wakristo, wakati wakipaka kuta za kanisa hilo rangi.

Kanisa la Kianglikana, lango lake na pia kuta, zimepakwa rangi ya manjano.

Kuta za msikiti pia zimepakwa rangi ya manjano, zoezi lililofanywa na wakristo.

Wakaazi wa Kibera wakishirikiana katika kupaka rangi mskiti Kibera kuonyesha umoja kati ya uislamu na ukristo

Chanzo cha picha, Colour in Faith

Maelezo ya picha, Wakaazi wa Kibera wakishirikiana katika kupaka rangi mskiti Kibera kuonyesha umoja kati ya uislamu na ukristo

Katika mtaa wa Kibera, umaskini ukosefu wa usalama na pia mivutano baina ya waumini wa dini tofauti hushuhudiwa mara kwa mara.

Kuna misikiti 14, na takriban kanisa mia saba.

Imamu Yusuf Nasur Abu Hamza, ''wakati mwingine waislamu huwa wanahisi kama wakristo wanapendelewa na serikali''.

Msimamizi wa mradi huu Nabila Alibhai anasema, kuwashawishi viongozi wa kidini kushiriki katika mradi huu, halijakuwa jambo rahisi, haswa kutokana na ukiritimba wa kamati za maeneo ya ibada.

Maelezo ya sauti, Wakristo na Waislamu waonyesha umoja Kibera Kenya