Uvamizi wa Lebanon: Je! Jeshi la Lebanon liko wapi wakati Israel inavamia?

    • Author, Carine Torbey
    • Nafasi, BBC News
    • Akiripoti kutoka, Beirut
  • Muda wa kusoma: Dakika 5
A Lebanese army soldier gestures at the scene of a reported pager explosion in Saida in southern Lebanon on 18 September 2024

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Askari wa jeshi la Lebanon baada ya tukio la mlipuko wa vifaa vya mawasiliano huko Saida kusini mwa Lebanon 18 Septemba 2024.

Mgogoro wa sasa kati ya Israel na kundi la wanamgambo la Hezbollah unatokana na mambo mawili makubwa, ambayo yamedumu kwa zaidi ya miongo minne.

Israel inasema inataka kuisambaratisha Hezbollah kwani ni tishio kwake, huku Hezbollah ikiendelea kushambulia maeneo ya Israel katika juhudi za kuliangamiza taifa la Israel.

Kwa muda wa miezi 11 iliyopita, mashambulizi ya kila siku mpakani mwa nchi hizo mbili yameongeza mvutano huo wa muda mrefu.

Israel sasa imefanya uvamizi nchini Lebanon kwa mara ya kwanza tangu 2006. Wengi wanauliza; jeshi la Lebanon liko wapi wakati haya yote yakitokea, na linafanya nini kuzuia mzozo mkubwa zaidi!

Pia unaweza kusoma

Nani anailinda Lebanon?

Lebanese army forces prepare to destroy in a controlled explosion a communication device found on the ground in southern Lebanon, between the villages of Burj al Muluk and Klayaa, on 19 September 2024, after hundreds of pagers and walkie-talkies used by Hezbollah exploded across Lebanon in unprecedented attacks that spanned two days

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Vikosi vya jeshi la Lebanon vinajitayarisha kulipua kifaa cha mawasiliano kilichopatikana kusini mwa Lebanon siku mbili baada ya maelfu ya vifaa hivyo kulipuka

Jeshi la Lebanon halijashiriki katika mapigano ya Israel na Hezbollah – kundi ambalo linatajwa kuwa la kigaidi na Marekani, Uingereza na nchi nyingine za Ulaya na Kiarabu. Kinadharia, ni kazi ya jeshi kupambana na adui wa taifa na Israel ni adui rasmi wa Lebanon. Lakini jeshi la Lebanon linakosa zana na silaha zinazohitajika kwa makabiliano hayo.

Jeshi la Israel lina vifaa vya kutosha na linaungwa mkono na madola ya Magharibi – kifedha, kidiplomasia na katika suala la silaha.

Vilevile, kuna imani iliyoenea inayoungwa mkono na kauli kutoka kwa maafisa kadhaa wa ngazi za juu wa zamani, wakiishutumu Marekani kwa kuzuia serikali ya Lebanon kupata silaha za kisasa ambazo zinaweza kuwa tishio kwa Israel.

Mgogoro mkubwa wa kiuchumi - uliochochewa na mlipuko mbaya wa ghala la mbolea huko Beirut 2020 - umefanya mambo kuwa mabaya zaidi kwa jeshi la Lebanon. Ukosefu wa fedha umeathiri wafanyakazi wake na mahitaji yake ya kimsingi ya kiutendaji, kama vile mafuta.

Soldiers secure the area after leaders of the Popular Front for the Liberation of Palestine group are reported killed by an Israeli airstrike in the Kola area of Beirut, Lebanon on 30 September 2024

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Wanajeshi wakilinda eneo hili baada ya viongozi wa kundi la Popular Front for the Liberation of Palestine kuripotiwa kuuawa na mashambulizi ya anga ya Israel mjini Beirut.

Michango kwa jeshi la Lebanon

La kushangaza zaidi, Marekani, ambayo inachukuliwa na Hezbollah kama adui yake mkubwa, ndiyo mfadhili mkuu wa jeshi la Lebanon. Washington imechangia mishahara midogo ya wanajeshi wa Lebanon.

Na misaada yake ni magari, vifaa na silaha za kawaida na sio msaada mkubwa ukilinganisha na misaada inayotoa kwa Israel.

Lakini baadhi ya wachunguzi wa mambo wanaeleza kuwa udhaifu wa jeshi la Lebanon dhidi ya Israel ni sawa na udhaifu wa majeshi mengine katika eneo hilo.

"Si jeshi la Lebanon wala jeshi lolote la nchi ya Kiarabu lenye uwezo wa kukabiliana na Israel," anasema Jenerali Mounir Shehade, mratibu wa zamani wa serikali ya Lebanon katika Kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini Lebanon (Unifil).

"Njia pekee ya kupambana na Israel ni kupitia vita vya kuvizia, kama inavyotokea Gaza."

Lebanese army soldiers talk while standing guard at the entrance of a hospital in Beirut on 17 September 2024 (AFP via Getty Images)

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Wanajeshi wa jeshi la Lebanon wakilinda lango la hospitali moja mjini Beirut siku ambayo vifaa vya mawasiliano vililipuka na kuua makumi ya watu na kujeruhi maelfu.

Khalil El Helou, jenerali mstaafu katika jeshi la Lebanon anasema "jukumu la jeshi la Lebanon ni kudumisha utulivu wa ndani, na leo hii hali ya ndani ni tete.

Kuhamishwa kwa wafuasi nusu milioni wa Hezbollah kwenda maeneo ambayo hayaungi mkono Hezbollah kunaweza kuleta msuguano ambao unaweza kuibua machafuko na pengine vita vya wenyewe kwa wenyewe," anasema.

Kufuatia kuuawa kwa kiongozi wa Hezbollah Hassan Nasrallah na Israel, jeshi la Lebanon lilisambaa kwa wingi katika maeneo mengi yanayoonekana kuwa "nyeti" ambapo kulikuwa na uwezekano mkubwa wa kutokea mvutano kati ya makundi tofauti nchini humo.

Pia ilitoa taarifa Jumapili iliyopita ikiwataka "raia kudumisha umoja wa kitaifa," ikisisitiza kuwa inaendelea kuchukua hatua za kulinda amani ya raia nchini humo.

Lebanese army soldiers stand guard in the road near a hospital in Beirut

Chanzo cha picha, Getty Images

Maelezo ya picha, Wanajeshi wa Lebanon wakilinda karibu na hospitali moja huko Beirut

Jeshi liko kwenye mgogoro na Israel?

Je, jeshi la Lebanon lina husika katika uhasama uliopo? Jawabu ni hapana.

Lakini jeshi hilo lipo kusini na kwa idadi kubwa. Hivi karibuni jeshi lilitangaza kuwa mwanajeshi wa Lebanon aliuawa na ndege isiyo na rubani ya Israel ambayo ililenga pikipiki iliyokuwa ikipita kwenye kituo cha ukaguzi.

Pia unaweza kusoma

Imetafsiriwa na Rashid Abdallah