Ni mambo gani yalitabiriwa mwaka 1995 kuhusu mwaka 2025?

Mnamo 1995, kipindi cha BBC Tomorrow's World kiliamua kutabiri namna ulimwengu utakavyokuwa miaka 30 baadaye, yaani 2025.
Kipindi hicho ambacho hakirushwi tena, kilimshirikisha mmoja wa wanasayansi maarufu wa zama hizo, Prof Stephen Hawking, ambaye alitabiri: "Kufikia 2025 tunaweza kutarajia mabadiliko makubwa."
Alielezea juu ya uvumbuzi ambao utatikisa ulimwengu kuanzia kwenye vifaa vya matibbu ya upasuaji hadi sekta ya anga. Baada miongo mitatu kupita - hebu tuangalie ni kwa namna gani utabiri huo umefanikiwa kuuangazia ulimwengu leo?
Intaneti kuleta machafuko

Mnamo mwaka 1995, intaneti ilianza kutumika ulimwenguni - maendeleo ambayo kipindi cha Tomorrow's World kilitabiri yangeleta matatizo katika siku zijazo.
Walitabiri "matajiri wakubwa" na benki zitachukua udhibiti wa intaneti kufikia 2000, na kuanzisha "intaneti itayaokuwa na kasi zaidi na kudhibiti usambazaji wake.
Hilo, kwa upande mmoja, lingesababisha udukuzi, virusi na hata ghasia.
Intaneti bado inatumiwa na watu wengi, na haijaleta ghasia, lakini hakuna shaka vitendo vya wadukuzi vimesababisha kadhia kwa watu wengi.
Kitu kimoja ambacho kipindi hicho hakikutabiri ni kuhusika kwa wadukuzi wa taifa kama Korea Kaskazini, na hilo lilielezwa katika podcast ya Lazarus Heist ya BBC.
Uchimbaji madini katika miamba ya angani
Kipindi hicho hicho kilitabiri kuwa uchimbaji wa madini angani ungekuwa sekta yenye faida kubwa, huku makampuni yakichimba katika miamba (asteroids) iliyo karibu na dunia kwa ajili ya madini ya thamani.
Utabiri ulieleza taka za angani zingehatarisha usalama wa wanaanga.
Kufikia Januari 2025, hakuna sekta ya uchimbaji madini nje ya sayari yetu, lakini hilo linaweza kubadilika.
Mtaalamu wa masuala yajayo Tom Cheesewright ana matumaini kuhusu uchimbaji madini nje ya sayari yetu.
"Utajiri uliokuwa ni mkubwa na teknolojia iko ndani ya uwezo wetu," amesema.
Madaktari bingwa wa upasuaji na roboti zao

Tomorrow's World kilitabiri kufikia 2004, sheria ingepitishwa kwa hospitali zote za Uingereza kuchapisha jedwali la viwango vya mafanikio ya upasuaji uliofanywa na madaktari wake. Madaktari wakuu wa upasuaji wangekuwa maarufu sana, na kulipwa vizuri, kusingekuwa na haja kwao kusafiri kufata wagonjwa.
Badala yake, hologramu za wagonjwa zingetumwa kwao na daktari wa upasuaji angefanya kazi kwa kutumia "glavu maalum." Mwishoni, roboti inaweza kuiga kikamilifu mienendo ya daktari wa upasuaji.
Hadi sasa - hilo halijawezekana kama hivyo, lakini roboti zinasaidia kwa upasuaji.
Kupata huduma za kibenki kwa kutumia chipu iliyopo mkononi mwako

Mahali pengine katika kipindi hicho, tulipewa maono ya huduma zinazotarajiwa za kibenki.
Ilionyesha mwanamke akienda benki, akilalamika hakuna wahudumu binadamu, na kisha kutoa "kiasi cha Euro 100." Benki inampa pesa hizo baada ya kuskani chipu mkononi mwake.
Uhalisia - Huduma ya benki kwa kweli imekuwa ya kidijitali zaidi na zaidi. Ingawa kulipa kupitia chipu ndani ya mwili wa binadamu ni jambo linalowezekana, teknolojia nyingine - hasa alama za vidole na uso - zinatumika zaidi.
Kumbukumbu kutoka kwa watangazaji

Chanzo cha picha, Getty Images
Nyota wa Dunia wa sekta ya kilimo cha bustani Monty Don alikuwa mmoja wa watangazaji kwenye kipindi hicho cha Tomorrow's World miaka 30 iliyopita. Sehemu yake ilitabiri urejeo mkubwa wa misitu ya Uingereza kutokana na uzalishaji wa vifaa vya kilimo na kusababisha kurudi kwa wanyama ikiwa ni pamoja na dubu wa kahawia.
Akitafakari kuhusu hilo sasa, ameiambia BBC News kwamba sehemu yake ya kipindi hicho ilikuwa haina uhalisia.
Akiangalia miaka 30 sasa, amefurahishwa na kizazi cha sasa cha vijana "kinachoguswa zaidi na mabadiliko ya tabia nchi" na anaamini watu watakuwa wakilima chakula chao zaidi ifikapo 2055.

Vivienne Parry alikuwa mtangazaji mwingine kwenye kipindi cha utabiri, na alikuwa na kipengele kilichozungumzia dawa.
Vivienne amejihusisha na Genomics England tangu 2013, na anaangazia baadhi ya utabiri kutoka katika kipindi hicho cha 1995 kuhusu mpangilio wa vinsaba umetimia, anapofanyia utafiti ili kusaidia kutambua na kutibu hali za vinasaba.

Dunia itakuwaje 2055?
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Mtabiri Tracey Follows anaamini programu ya 1995 ilipatia tabiri nyingi kubwa sawa, lakini ikakosea mada mbili kuu za miaka 30 iliyopita - kuenea kwa makampuni ya teknolojia na mitandao ya kijamii.
Kufikia 2055, anafikiri watu wengi "watakuwa wameweza kuunganishwa kimawazo" - mawazo ya wanadamu na teknolojia kupitia seva, ambayo itasaidia katika kubadilishana mawazo.
"Kushirikishana kiakili kutakuwa kwa uhalisi, ambapo utaweza kubadilishana mawazo na mtu mwingine kwa kuyafikiria tu."
Tom Cheesewright anafikiri matarajio mawili ya kusisimua zaidi kwa miaka 30 ijayo yatakuwa maendeleo ya sayansi ya vifaa na matumizi ya tishu bandia, viungo, au sehemu za kiungo kuchukua nafasi ya sehemu za mwili zilizoharibika au kutokuwepo.
Kwa hivyo unadhani ulimwengu utakuwaje katika miaka 30 ijayo?
Licha ya majibu yako, lingekuwa jambo la busara kusikiliza kile Prof Hawking aliambia Tomorrow's World miongo mitatu iliyopita.
"Baadhi ya mabadiliko haya yanasisimua sana, na mengine yanatisha. Kitu kimoja ambacho tunaweza kuwa na uhakika nacho ni kwamba yatakuwa tofauti sana, na pengine si kile tunachotarajia."















