Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kipi cha kufanya na kutofanya unapopasha chakula moto?
- Author, Nazanin Motamedi
- Nafasi, BBC Persian
- Muda wa kusoma: Dakika 3
Kupasha chakula moto kunaweza kuwa na hatari za kiafya. Kufuata mwongozo huu kutakusaidia kukifanya chakula chako kuwa salama na kupunguza hatari ya magonjwa yatokanayo na chakula.
Kuna njia za asili za kupasha chakula moto, ambapo masufuria hutumika ama vyungu. Pia kuna njia za kisasa, kama ile inayohusisha vifaa vya umeme kama mikrowevu.
Mambo usiyopaswa kufanya
Usipashe kwenye plastiki
Mara nyingi tunaweka chakula kwenye mikrowevu katika vyombo vya plastiki, lakini wataalamu wanaonya juu ya hatari ya kumeza chembechembe za plastiki zilizoyeyuka, kwani baadhi ya plastiki hazijatengenezwa kuhimili joto.
Usipashe tena wali baada ya kununu
Wali hupikwa au kupashwa moto katika mkahawa kabla ya kuuzwa, hivyo basi ni hatari kuupasha moto tena. Ni bora kuula muda mfupi baada ya kuununua.
Usiweke chakula kwenye friji kwa muda mrefu
Inashauriwa kutoweka chakula kilichopikwa kwenye jokofu kwa zaidi ya siku 3-4, ili kupunguza hatari ya magonjwa yatokanayo na chakula. Baada ya muda huu, bakteria wanaweza kukua hadi viwango visivyo salama, hata kama chakula hakina harufu au hakijaharibika.
Usiyeyushe kuku kwa maji ya joto
Sio salama kuyeyusha kuku katika maji ya moto. Kumuweka kuku katika maji ya moto kunasababisha bakteria kukua kwa haraka katika nyuzijoto 40 hadi 140, wakati sehemu ya ndani ya kuku bado ikiwa ya baridi.
Unachopaswa kufanya
Hifadhi chakula kwenye friji kabla ya kukipasha moto tena
Utafiti unaonyesha kuwa kuweka chakula kwenye jokofu (katika nyuzi joto 5°C au chini) huzuia ukuaji wa vimelea hatari. Chakula kilichopikwa kinapaswa kuwekwa kwenye jokofu ndani ya masaa 2 baada ya kupikwa.
Poza chakula chako kabla ya kukiweka kwenye friji
Kuweka chakula cha moto kwenye friji kunaweza kuongeza halijoto ya friji lako na bakteria kukua. Acha chakula chako kipoe kwenye joto la kawaida na ukiweke kwenye jokofu mara tu kinapopoa.
Joto la hatari kwa chakula
Kati ya nyuzijoto 8°C na 63°C, bakteria wanaweza kuongezeka kwa kasi. Kuweka friji yako chini ya nyuzijoto 5°C husaidia kuzuia sumu ya chakula, na kugandisha chakula kwenye nyuzijoto -18°C huzuia shughuli za bakteria. Hata hivyo, bakteria hawafi kwa kukandisha chakula – wanaweza kuibuka tena unapokiyeyusha.
Yeyusha chakula kabla ya kukipasha moto tena
Inapendekezwa kuyeyusha chakula kikamilifu kabla ya kukipasha moto. Hasa kwa vyakula vilivyopikwa kama nyama na kuku, ili kuhakikisha unazuia bakteria hatari. Hata hivyo, baadhi ya vyakula, kama vile mboga mboga vinaweza kupashwa moto upya moja kwa moja bado vikiwa vimeganda, lakini ni vyema kuangalia maelekezo ya kifurushi.
Pasha moto wali ndani ya saa 24
Kuupoza wali na kuweka kwenye jokofu hupunguza hatari ya bakteria, lakini upashaji moto unapaswa kufanywa mara moja tu. Ni hatari kurudi rudia.
Chukua tahadhari
Watu walio na kinga dhaifu, matatizo ya kiafya, wanawake wajawazito, watoto wadogo, na watu wazima - wako katika hatari kubwa ya magonjwa yanayosababishwa na chakula. Hivyo chukua tahadhari unapowatayarishia chakula.
Pasha moto chakula na kiwe moto chote
Ikiwa unapasha moto chakula, koroga katikati ili kuhakikisha chakula chote kimepata moto.