Kwanini Wamarekani wamempa Trump nafasi nyingine?

Chanzo cha picha, Getty Images
- Author, Sarah Smith
- Nafasi, North America editor
- Muda wa kusoma: Dakika 5
Hakika huu ni ushindi wa kushangaza zaidi katika historia ya kisiasa ya marekani.
Miaka minne baada ya kuondoka Ikulu ya White House, Donald Trump anatazamiwa kurejea tena, baada ya mamilioni ya Wamarekani kupiga kura kumpa nafasi ya pili.
Kampeni ya uchaguzi ilikuwa moja ya vitabu vya historia: alinusurika majaribio mawili ya mauaji na mpinzani wake wa awali Rais Joe Biden alijiondoa miezi michache kabla ya siku ya uchaguzi.
Ingawa kura za mwisho bado zinahesabiwa, Wamarekani wengi katika majimbo muhimu yenye ushawishi walichagua kumpigia kura, huku wengi wakitaja uchumi na suala la uhamiaji kama jambo kuu.

Chanzo cha picha, AP
Ushindi wake unakuja baada ya anguko la kustaajabisha. Alikataa kukubali matokeo ya uchaguzi wa 2020, ambao alishindwa na Biden, na jukumu lake katika kujaribu kutengua matokeo ya uchaguzi ili kusalia ofisini bado linachunguzwa hadi leo.
Anakabiliwa na mashtaka kwa madai ya kuchochea shambulio la vurugu kwenye Bunge la Marekani tarehe 6 Januari 2021. Na pia ataweka historia kama rais wa kwanza aliyeko madarakani kutiwa hatiani kwa kosa la jinai, baada ya kupatikana na hatia ya kughushi rekodi za biashara.
Si vigumu kuona ni kwa nini yeye ni mtu wa aina yake.
Katika muda wote wa kampeni, Trump alitumia matamshi ya uchochezi - akifanya utani mbaya na kutishia kulipiza kisasi dhidi ya maadui zake wa kisiasa.
Ujumbe wake kuhusu uchumi uligusa wengi
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Watu wachache wana msimamo wa kati linapokuja suala la Trump. Wapiga kura wengi niliozungumza nao wakati wa kampeni hii walisema walitamani "angefunga mdomo" - lakini waliweza kuvumilia hilo.
Badala yake, walizingatia swali alilouliza katika kila mkutano. "Je, una hali nzuri sasa kuliko miaka miwili iliyopita?"
Watu wengi sana waliompigia kura Donald Trump waliniambia tena na tena kwamba waliona uchumi ulikuwa bora zaidi alipokuwa ofisini na walikuwa wamechoka kujaribu kujikimu. Ingawa sababu nyingi za mfumuko wa bei zilitokana na nguvu za nje kama vile janga la Covid-19, walilaumu utawala unaoondoka.
Wapiga kura pia walikuwa na wasiwasi mkubwa kuhusu uhamiaji haramu ambao ulikuwa umefikia viwango vya rekodi chini ya Biden. Kawaida hawakuonyesha maoni ya ubaguzi wa rangi au kuamini kuwa wahamiaji walikuwa wakila wanyama wao wanaofungwa, kama Trump na wafuasi wake walivyodai. Bali walitaka tu utekelezwaji wa kusimamia mipaka wenye nguvu zaidi.

Chanzo cha picha, Getty Images
'Marekani kwanza' kwa muhula wa pili wa Trump
"Marekani kwanza" ilikuwa kauli mbiu nyingine ya Trump ambayo ilionekana kugusa hisia kwa wapiga kura wengi. Nchini kote nilisikia watu - upande wa kushoto na kulia - wakilalamika kuhusu mabilioni ya dola kutumika kusaidia Ukraine wakati walidhani kwamba pesa zingetumiwa vizuri zaidi nyumbani.
Mwishowe, hawakuweza kumpigia kura Harris, ambaye alihudumu kama makamu wa rais wa Biden kwa miaka minne. Waliamini ingekuwa ni zaidi ya sawa na uongozi unaondoka, na walitaka mabadiliko.
Pengine ni moja ya jambo la kufikirisha katika uchaguzi huu kwamba mgombea aliyewakilisha zaidi mabadiliko alikuwa yeye mwenyewe madarakani miaka minne tu iliyopita. Lakini kuna tofauti kadhaa kati ya wakati huo na sasa.
Alipoingia madarakani kwa mara ya kwanza mwaka wa 2016, hakua mtu wa kisiasa, na, angalau kwa muda, alizunguka na washauri na wafanyakazi wakongwe wa kisiasa ambao walimuonyesha njia za kisiasa na kuzuia matendo yake. Sasa haonekani kuwa na nia ya kucheza kwa sheria za mchezo wa siasa.
Wengi wa washauri hao hao na wafanyakazi hawa wamezungumza - kumwita "mwongo", "fashisti" na "hafai". Wametahadharisha kwamba ikiwa atajizunguka na watu wanaomuabudu, ambao anatarajiwa kufanya, kwamba hakutakuwa na mtu wa kumzuia kutoka kwa mawazo yake makali zaidi.
Alipoondoka ofisini, alikabiliwa na msururu wa mashtaka ya uhalifu kuhusiana na jukumu lake katika ghasia za jengo la Capitol, jinsi alivyoshughulikia hati zinazohusu usalama wa taifa, na malipo ya pesa ya kumnyamazisha nyota wa ponografia.

Chanzo cha picha, AFP
Lakini kwa vile Mahakama ya Juu iliamua kwamba rais ana kinga kamili dhidi ya kushtakiwa kwa vitendo rasmi katika ofisi, itakuwa vita kali kwa mwendesha mashtaka yeyote kumfungulia mashtaka wakati wa utawala ujao.
Na kama rais, anaweza kuagiza idara yake ya haki kufuta mashtaka ya shirikisho dhidi yake yanayohusiana na ghasia za Januari 6 ili asiwe na wasiwasi kuhusu kifungo cha jela. Wakati huo huo, angeweza kusamehe mamia ya watu waliohukumiwa kifungo kwa sehemu yao katika Machafuko ya Capitol.
Mwishowe, wapiga kura waliwasilishwa matoleo mawili ya Marekani.
Donald Trump aliwaambia kuwa nchi yao ni taifa lenye kushindwa ambalo ni yeye pekee angeweza kufanya makubwa tena na kuliokoa.
Wakati huo huo, Harris alionya kwamba ikiwa Trump atachaguliwa, demokrasia ya Marekani yenyewe itakabiliwa na tishio lililopo. Hilo linabaki kuonekana. Lakini alichosema Trump mwenyewe wakati wa kampeni hakijaondoa kabisa hofu ya watu.

Chanzo cha picha, Reuters
Amewasifu viongozi wa kimabavu kama vile Vladimir Putin wa Urusi na Kim Jong Un wa Korea Kaskazini, ambao alisema walikuwa "viongozi ngangari, upende usipende".
Amezungumza kuhusu kujaribu kuwanyamazisha wakosoaji kwenye vyombo vya habari. Siku chache kabla ya uchaguzi, pia alitoa maoni ambayo yalimaanisha kwamba hatajali ikiwa wanahabari watauawa.
Na ameendelea kukuza nadharia za njama na madai yasiyo na msingi ya udanganyifu wa uchaguzi - ingawa uchaguzi hatimaye ulisababisha ushindi wake.
Sasa, wapiga kura wataelewa ni kiasi gani alichosema wakati wa kampeni kilikuwa ni mazungumzo ya bure tu ama ni - "Trump akiwa Trump". Na kumbuka: sio Wamarekani pekee ambao wanapaswa kukabiliana na ukweli wa muhula wa pili wa Trump.
Ulimwengu uliobaki sasa utagundua nini "Marekani Kwanza" inamaanisha. Kutokana na matokeo ya kiuchumi ya kimataifa ya ushuru wa 20% ambayo amependekeza kwa uagizaji wa Marekani kwa vita vya Ukraine na Mashariki ya Kati ambayo ameapa kukomesha - bila kujali ni upande gani utashinda.
Donald Trump hakufanikiwa kutekeleza mipango yake yote katika muhula wake wa kwanza. Sasa kwa mamlaka ya mara ya pili marekani na ulimwengu, utaona kile anachoweza kufanya.
Imetfasiriwa na Munira Hussein na kuhaririwa na Seif Abdalla












