Afcon 2019: Tanzania yaifumua Cape Verde 2-0 na kufufua matumaini ya kufuzu

Chanzo cha picha, TFF
Matumaini ya Tanzania kufuzu katika fainali za kombe la mataifa ya Afrika (Afcon) 2019 bado yangalipo baada kuichabanga Cape Verde 2-0 jijini Dar es Salaam.
Huu ulikuwa ni mchezo wa marudiano wa kundi L ambapo Tanzania ilifungwa Ijumaa iliyopita goli 3-0 na kufanya matumaini ya taifa hilo la Afrika mashariki kwenda Cameroon kwa michuono ya Afcon mwakani kufifia.
Ushindi wa leo unaifanya Tanzania kufikisha pointi 5 baada ya kucheza michezo 4. Imetoka sare michezo miwili na kufungwa mmoja.
Tanzania almaarufu kama Taifa Stars kwa sasa ipo nafasi ya pili nyuma ya vinara Uganda wenye pointi 7. Uganda na Lesotho inayoshika mkia kwa sasa kwa kuwa na pointi 2 wanashuka dimbani usiku wa leo na endapo Uganda itashinda watakuwa katika nafasi nzuri ya kufuzu.
Lakini kama Lesotho watapata ushindi mambo yatakuwa magumu kwa timu zote za kundi hilo ambapo kinara Uganda atasalia na pointi 7 akifuatiwa na Tanzania na Lesotho watakaokuwa na pointi 5 kila mmoja na Cape Verde watashika mkia kwa alama zao 4.
Mkala hii imebeba madhui yaliyotoka kwenye mitandao ya kijamii. Tunaomba ruhusa yako kabla kitu chochote hakija pakiwa, sababu wanaweza wakawa wanatumia Cookies na tekinolojia nyingine. Unaweza ukasoma sera sera ya kutumia cookies katika mitandao ya kijamii kabla ya kukubali. Kutazama maudhui haya chagua accept and continue
Mwisho wa X ujumbe
Tanzania ilianza mchezo wa leo kwa kasi, Nahodha wa Tanzania na nyota wa klabu ya Genk ya Ubelgiji Mbwana Samatta aliwaacha watanzania midomo wazi kwa mshangao baada ya kukosa mkwaju wa penati katika dakika ya 21.
Samatta alirekebisha makosa yake katika dakika ya 29 kwa kutengeneza nafasi maridhawa iliyotumiwa vyema na mshambuliaji Saimon Msuva aliyeandikia Tanzania bao la kuongoza.
Tanzania ilirudi na kasi katika kipindi cha pili na nyota wao Samatta kuiandikia bao la pili katika dakika ya 58.

Chanzo cha picha, Getty Images
Baada ya kichapo cha Ijumaa nchini Cape Verde matumaini ya wengi nchini Tanzania yalififia lakini kocha wa Taifa Stars Emmanuel Amunike hakukata tamaa.
Amunike, ambaye ni nyota wa zamani wa Nigeria alisema kuwa; "nafasi bado ipo, kundi letu bado lipo wazi, tunaweza kufanikiwa."
Maneno hayo ya Amunike yanaonekana kuwa na uhalisia sasa, lakini Taifa Stars bado wanakibarua kigumu cha kuvaana na Lesotho ugenini na Uganda nyumbani Dar es Salaam.












