Moshi: Mtanzania aliyeamua kutokufa moyo Olimpiki

Magdalena Moshi

Chanzo cha picha, Missy Moshi / Facebook

Maelezo ya picha, Magdalena Moshi alimaliza nambari tano kundini Rio

Baada ya kupata jeraha la bega mwaka 2012 na matatizo ya kiafya mwaka jana, wengi walidhani huo umekuwa mwisho wa ndoto yake kama mwogeleaji.

Baadhi ya madaktari walikubaliana na hayo.

Lakini Magdalena Ruth Alex Moshi hakufa moyo. Na siku ya Ijumaa, mjini Rio de Janeiro, alijibwaga kwenye dimbwi la kuogelea, akiwakilisha taifa lake Tanzania katika mashindano ya kuogelea 50m freestyle.

Ilikuwa ni mara yake ya tatu kushiriki michezo ya Olimpiki. Alimaliza wa tano katika kundi 4 la waogeleaji wanane, muda wake ukiwa sekunde 29.44, huo ukiwa muda wake bora zaidi.

Moshi, 25, ni mwanafunzi katika chuo kikuu cha Adelaide, Australia.

Amesimulia kizungumkuti alichokuwa nacho mwaka 2012 na ufanisi alioupata hadi kufikia sasa kwenye ujumbe katika Facebook.

Magdalena Moshi

Chanzo cha picha, Missy Moshi / Facebook

"Ningependa kuwashukuru watu wote kote duniani kwa usaidizi wao. Ni heshima kubwa. Asanteni sana pia kwa kitambulisha mada #teammissy," ameandika.

"Nilijitolea kabisa, mwili wangu ulikuwa unatetemeka na hata sikuweza kutembea kuondoka kidimbwini."

Anasema ilikuwa changamoto kubwa kwake akikulia Tanzania, taifa ambalo halina timu ya uogeleaji, akiwa na ndoto ya kushiriki michezo ya ulimpiki tangu akiwa mdogo.

"Nilipokuwa eneo la kuanza kuogelea, bendera ya taifa langu ilikuwa nyuma ya pete za nembo ya Olimpiki, na nilisema, lo, 'nimewezesha bendera hiyo iwekwe hapo mara tatu'," amenukuliwa na gazeti la Gold Coast Bulletin.

Moshi alizaliwa Adelaide na mamake ni wa asili ya Australia lakini alilelewa na babake nchini Tanzania.

Alirejea Australia mwaka 2010 kusomea utabibu.

Ni mmoja wa wanamichezo saba waliowakilisha Tanzania Michezo ya Olimpiki Rio.