Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Vita vya Ukraine: Wanajeshi wa Ukraine waingia mjini Kherson

Wanajeshi wa Ukraine wamekaribishwa mjini Kherson na wakaazi waliojawa na furaha, baada ya Urusi kusema kuwa imejiondoa kikamilifu katika mji huo muhimu wa kusini.

Moja kwa moja

  1. Urusi yatangaza 'mji mkuu' mpya kwa eneo la Kherson

    Urusi imefanya mji wa bandari kusini-mashariki mwa Ukraine - Henichesk - mji mkuu wake mpya wa utawala wa muda katika mkoa wa Kherson.

    Henichesk iko karibu na Crimea inayokaliwa na Urusi na umbali mrefu kutoka Kherson, ambayo vikosi vya Ukraine viliikomboa tena siku ya Ijumaa. Ni mji mdogo kuliko Kherson na uko kwenye Bahari ya Azov.

    Shirika la habari la Interfax la Urusi linasema mamlaka ilihamisha afisi zote za kanda pamoja na "sanamu na vitu vya sanaa vya kihistoria" kutoka ukingo wa magharibi wa mto Dnipro - yaani, kutoka mji wa Kherson na mazingira yake. Zaidi ya watu 115,000 walihamishwa kutoka eneo hilo, inaripoti.

    Kherson ilikuwa mojawapo ya mikoa minne ya Ukrain ambayo Rais Vladimir Putin alidai kutwaa Septemba - dai lililokataliwa kimataifa. Urusi ilitwaa Crimea mnamo 2014.

  2. Mzozo wa DRC: Wanajeshi wa Kenya KDF wawasili nchini humo

    Wanajeshi wa Kenya walitua katika mji wa Goma mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo siku ya Jumamosi, ikiwa ni sehemu ya operesheni ya kijeshi ya eneo hilo kuwalenga waasi katika eneo hilo lenye migogoro.

    Kuwasili kwao kunajiri wakati wanamgambo wa M23 wakiwa wameingia katika jimbo la Kivu Kaskazini nchini DRC, na kuteka maeneo mengi na kuzidisha hali ya wasiwasi Afrika ya kati.

    Wiki hii, bunge la Kenya liliidhinisha kutumwa kwa zaidi ya wanajeshi 900 nchini DRC kama sehemu ya kikosi cha pamoja cha kijeshi kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).

    Ndege mbili zilizokuwa zimebeba takriban wanajeshi 100 wa Kenya zilitua katika uwanja wa ndege wa Goma siku ya Jumamosi, kulingana na waandishi wa habari wa AFP waliokuwepo, wanajeshi hao walilakiwa na viongozi wa eneo hilo.

    Kamanda wa Kenya, Luteni Kanali Obiero, aliwaambia waandishi wa habari kwamba dhamira yao ni "kuendesha operesheni " pamoja na vikosi vya Kongo, na kusaidia katika kuwapokonya silaha wanamgambo.

  3. Wanajeshi wa Urusi huenda waliharibu daraja na barabara wakiondoka kherson - Uingereza

    Katika ukaguzi wake wa hivi karibuni wa hali ilivyo, wizara ya ulinzi ya Uingereza inasema kuna ‘uwezekano mkubwa’ wanajeshi wa Urusi waliharibu barabara na daraja la reli juu ya mto Dnipro kama sehemu ya kuondoka kwao.

    Picha ziliibuka jana zilizoonyesha kivukio kikuu cha mto kutoka Kherson - sehemu ya Daraja la Antonivsky lilikuwa limevunjika. Haijulikani uharibu huo umetokea vipi.

    Kuondoka kwa vikosi vya Urusi kutoka Kherson kulitangazwa rasmi Jumatano lakini wizara ya Ulinzi inseam huenda walianza kuanzia Oktoba 22 wakati maafisa waliochaguliwa wa Urusi walipowaomba raia waondoke mjini humo.

    "Kuna uwezekano halisi kuwa vifaa vya jeshi la Urusi na vikosi waliovaa nguo za raia walikuwa wanaondoka kwa kuambatana na raia 80,000 wanaotajwa kuhama katika wiki za hivi karibuni," inasema.

    Wizara hiyo ya Ulinzi Uingereza inasema pia huenda Urusi bado inajaribu kuondoa vikosi vyake katika sehemu nyingine za eneo katika mto kuelekea katika maeneo ya ulinzi katika ukingo wa mashariki.

    "Kherson ndio uliokuwa mji wa pekee kieneo uliodhibitiwa tangu Februari na vikosi vya urusi, kwa hivyo kuondoka huko kuna tia dosari sifa," inaongeza. "Kuondoka huko ni utambulisho wa wazi wa changamoto zinazowakabili vikosi vya Urusi katika ukingo wa magharibi wa mto Dnipro."

    Wizara ya ulinzi imeongeza kuwa Ukraine imedhibiti upya maeneo makubwa ya Kherson katika ukingo wa maharibi wa mto huo, na kwamba vikosi vyake kwa sasa vinadhibiti kwa ukubwa mji wenyewe wa Kherson.

  4. Waziri wa Ulinzi wa Uingereza: Urusi imepata "pigo la kimkakati"

    Waziri wa Ulinzi wa Uingereza: Urusi imepata "pigo la kimkakati"

    Waziri wa Ulinzi wa Uingereza Ben Wallace alitaja kujiondoa kwa jeshi la Urusi kutoka Kherson na kutoka ukingo wa kulia wa Mto Dnieper "piga la kimkakati" upande wa Urusi

    Kulingana na Wallace, kutekwa kwa Kherson lilikuwa lengo pekee la kimkakati ambalo jeshi la Urusi liliweza kufikia mwanzoni mwa vita.

    "Sasa kwa kuwa [jiji hilo] limekombolewa, watu wa kawaida nchini Urusi labda wanapaswa kujiuliza swali: "Kwa nini yote haya yatokee?" Kama matokeo ya uvamizi huo haramu, jeshi la Urusi lilipata hasara kubwa, na lilipata kutengwa na kudhalilishwa kimataifa tu" - alisema Waziri wa Ulinzi.

    Kulingana na Ben Wallace, Ukraine itaendelea kusonga mbele, na Uingereza na jumuiya ya kimataifa itaendelea kuiunga mkono.

    "Wakati kurudi nyuma kunatia moyo, tishio ambalo linaendelea kutokea kwa Shirikisho la Urusi haliwezi kupuuzwa," waziri wa ulinzi wa Uingereza alisema.

  5. Habari za hivi punde, Mzozo wa Ukraine: Jeshi la Ukraine hatimaye laingia mjini Kherson

    Wanajeshi wa Ukraine wamekamilisha ukombozi wa eneo la ukingo wa magharibi (kulia) wa mto Dnieper ya mkoa wa Kherson baada ya kuondoka kwa Warusi.

    Jeshi hilo limeingia wakati ambapo wanajeshi wa Urusi wanaonekana kusalia katika upande wa kulia wa mto Dnieper ijapokuwa idadi hiyo sio kubwa.

    Inaelekea wanajaribu kurudi nyuma kadri jeshi la Ukrain linavyosonga mbele, lakini pia kuna uwezekano kwamba baadhi ya Warusi wana mpango wa kufanya mashambulizi wakiwa msituni katika vikundi vidogo.

  6. Rais wa Angola na aliyekuwa rais wa Kenya kukutana na Rais Felx Tshisekedi

    Rais wa Angola Joao Lourenco anatarajiwa kukutana na aliyekuwa rais wa Kenya Uhuru kenyatta katika harakati za kutatua mzozo unaoendelea nchini DR Congo.

    Wawili hao wanaowakilisha AU na SADC watakutana siku ya Jumapili ili kuangazia masuala ya mgogoro huo wa muda mrefu.

    Kabla ya kufanyika kwa mkutano huo siku ya Jumapili rais Lourenco atakutana na mwenyeji wake wa DR Congo felix Tshisekedi ana kwa ana .

    Kenyatta pia atakutana moja kwa moja na Rais Félix Tshisekedi ili kujiandaa kwa mkutano wa Nairobi III na wahusika wanaohusika katika mchakato huu wa amani, wiki ya mwisho ya mwezi huu.

    Akiwa mjini Kinshasa rais Kenyatta anapanga kukutana na takriban wawakilishi hamsini wa jamii za majimbo ya Ituri, Kivu Kaskazini na Kivu Kusini pamoja na wakuu wa taasisi.

    Mikutano hiyo inajiri wakati ambapo vita vimechacha nchini humo kati ya waasi wa M23 na vikosi vya serikali.

    Kenya imepeleka jeshi lake la KDF hii leo ili kujaribu kuweka amani.

  7. Vita havijaisha - mshauri wa ulinzi wa Ukraine

    Mshauri wa waziri wa ulinzi wa Ukraine amesema kuna "hofu" katika uongozi wa Urusi, lakini akaonya kwamba vita "viko mbali kuisha".

    Yuriy Sak aliambia kipindi cha Leo cha BBC Radio 4: "Siku zote tuliamini kwamba tutakomboa Kherson.

    "Na tuna uhakika kwamba sasa Warusi wanaanza kuamini kwamba hawataweza kushinda vita hivi.

    "Tunaona hofu katika uonozi wao. Tunaona hofu kwenye mashine yao ya propaganda.

    "Lakini bila shaka, huu ni wakati muhimu sana, lakini ni mapema sana kupumzika ... kwa sababu vita haviko mbali sana."

  8. Charline Ruto: Mjadala watanda Kenya kuhusu ufadhili wa mikutano ya bintiye Rais

    Yeye ni mtoto wa pili wa Rais William Ruto, na anajiita Binti wa Kwanza wa Kenya, lakini watumiaji wa mitandao ya kijamii wanauliza kwa nini Charlene Ruto anaonekana kukutana na mawaziri wengi wa serikali na kusafari nje.

    Miezi kadhaa tangu babake achaguliwe kuwa rais, vyombo vya habari vya humu nchini vinaripoti kuwa Bi Ruto amekutana na maafisa kadhaa wa kaunti kote nchini Kenya pamoja na mawaziri nje ya nchi.

    Wasiwasi kama huo ulizuka wakati Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump alipochaguliwa kwa mara ya kwanza na binti yake Ivanka alihudhuria mikutano na baba yake kama mshauri asiye rasmi. Bw Trump baadaye alimteua Ivanka katika jukumu rasmi la serikali.

    Mnamo Alhamisi, Charlene Ruto alisema kwenye Twitter kuwa amekutana na waziri wa vijana wa Morocco, Mohammed Mehdi, kwa "mazungumzo na kubadilishana mawazo ambayo yatasaidia sana katika kuunda miradi ya maendeleo ya vijana kwa mataifa yote mawili".

    Baadhi ya Wakenya sasa wanauliza, ni nani anayefadhili mikutano yote hii, na je ni mikutano rasmi ?

  9. Maafisa wa ngazi ya juu wasimamishwa kazi Chad baada ya maandamano makali.

    Wiki tatu baada ya operesheni kali dhidi ya waandamanaji wanaounga mkono demokrasia nchini Chad, mkuu wa polisi na kiongozi wa jeshi wamefutwa kazi wakiwemo maafisa wengine wa ngazi ya juu.

    Shirika la habari la Ufaransa RFI linasema limezungumza na duru kutoka ndani ambaye ameitaja hatua hiyo kama kukaza Kamba ya uongozi.

    Chad inaongozwa na jeshi ambalo kiongozi wake awali alisema atajiuzulu, lakini hivi karibuni ametangaza kwamba ataendelea kuiongoza nchi hiyo kwa miaka miwili zaidi.

    Tangazo hilo limesababisha kuzuka maandamano ya umma nchini wanaotaka kurudi katika utawala wa kiraia.

    Raia kadhaa wameuawa katika maandamano hayo na kusababisha kuzuka kwa shutuma kimataifa na mkutano wa viongozi wa matifa ya Afrika ya kati kukabiliana na mzozo.

  10. Wales: Vipindi vya masomo kukatishwa ili wanafunzi watazame mechi za Kombe la dunia

    Shule nchini Wales zaruhusiwa kughairi masomo ili kuwaruhusu wanafunzi kutazama timu yao ya taifa kwenye Kombe la Dunia.

    Wales itashiriki michuano hiyo kwa mara ya kwanza baada ya miaka 64 baada ya kufuzu kushiriki michuano ya mwaka huu huko Qatar.

    Serikali ya Wales imesema inaachia shule juu uamuzi iwapo zitawaruhusu wanafunzi kutazama mchezo dhidi ya Iran, ambao utaanza saa 10:00 GMT siku ya Ijumaa tarehe 25 Novemba.

    Mechi nyingine za Wales dhidi ya Marekani na Uingereza zote zitaanza saa 19:00 GMT. Wakiwa wamecheza katika Mashindano mawili ya mwisho ya Uropa, hii itakuwa mara ya kwanza Wales kucheza Kombe la Dunia tangu 1958.

    Mechi yao ya ufunguzi dhidi ya Marekani ni Jumatatu tarehe 21 Novemba.

    Zaidi ya shule 1,000 kote nchini zitashiriki katika Shirikisho la Soka la Wales (FAW) Cymru Football Ijumaa kwa mchezo wa Iran.

    Mtendaji mkuu wa FAW Noel Mooney alisema: "Tumefanya kazi na serikali ya Wales kuunda tamasha katika shule zetu zote na mchezo wa Iran ni bora kwetu. "Tunataka mtoto akumbuke na, kwa matumaini, aendelee kucheza kwa ajili yetu na kuwa siku zijazo."

  11. Wanajeshi wa Kenya KDF waelekea DR Congo kulinda amani

    Mkuu wa Majeshi nchini Kenya Robert Kibochi amewataka maafisa wa Jeshi la Kenya (KDF) kushirikiana vyema na wenzao wakati ambapo wanaelekea nchini DR Congo kwa ziara ya kulinda amani nchini humo.

    Hatua hiyo inajiri baada ya wiki iliopita Rais William Ruto kuamuru kutumwa kwa wanajeshi 903 kutoka KDF kujiunga na ujumbe wa kulinda amani wa kikanda - Kikosi cha Kanda ya Jumuiya ya Afrika Mashariki hukoJamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (EACRF-DRC).

    Lakini zkizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga wanajeshi hao siku ya Jumamosi, Kibochi alisema, "Nawatakia baraka mnapotumika. Ninyi ni mishale. Hakikisha unafanya kazi vyema na wenzenu.

    Kibochi alisisitiza utaalam na tajriba kubwa ya jeshi la KDF , akiongeza kuwa maafisa hao wanahitimu katika jukumu hilo.

    Aliwataka maafisa hao kutii sheria za nchi walizotumwa

  12. Tume ya uchaguzi Nigeria yaonya kuhusu ghasia

    Mkuu wa tume ya uchaguzi nchini Nigeria Mahmood Yakuba, amesena ana wasiwasi kuhusu mashambulio ‘yanayoongezeka’ wakati nchi hiyo ikijitayarisha kwa uchaguzi ujao wa urais mwezi Februari mwakani.

    Kuna wasiwasi kwamba uchaguzi huo ulio na ushindani mkali huenda ukakumbwa na ghasia zaidi ya inavyoshuhudiwa.

    Yakuba ameongeza kuwa tume hiyo tayari imeorodhesha visa 50 vya mashambulio vinavyohusiana na uchaguzi huo katika mwezi wa kwanza wa kampeni peke yake.

    Matamshi hayo yametolewa katika kikao cha dharura kilichoitishwa na tume hiyo baada ya ofisi zake mbili kushambuliwa siku ya Alhamisi.

    Mwezi uliopita, ubalozi wa Marekani ulihamisha baadhi ya wafanyakazi wake kutoka Abuja, ukitaja kuongezeka kwa uwezekano wa kutokea shambulio la kigaidi katika mji mkuu huo.

    Vikosi vya usalama vimekuwa vikipambana na tishio tofauti kote nchini, ikiwemo wapiganaji wenye itikadi kali za dini ya kiislamu, makundi ya wahalifu waliojihami na makundi yanayoshinikiza kujitenga.

  13. Mlinzi wa ubalozi wa Uingereza akiri kufanya ujasusi na kuipa nyaraka za siri Urusi

    Mlinzi mmoja amekiri kuipeleleza Urusi alipokuwa akifanya kazi katika Ubalozi wa Uingereza mjini Berlin.

    Waendesha mashtaka walidai David Smith, 58, alitaka kuumiza Uingereza na ubalozi ambapo alikuwa amefanya kazi kwa miaka minane.

    Muingereza huyo alishutumiwa kwa kukusanya taarifa za kijasusi kuhusu ubalozi huo na kuvujisha nyaraka za siri. Smith alikiri mashtaka katika Old Bailey kwa mashtaka manane chini ya Sheria ya Siri Rasmi.

    Inasemekana alitaka kuishi Urusi au Ukraine wakati alipopitisha ujasusi wa siri kutoka Mei 2020.

    Mashtaka yaliyowekwa dhidi ya Smith yalisema aliwasiliana na Jenerali Meja Sergey Chukhurov, afisa wa jeshi la Urusi aliyeko nje ya Ubalozi wa Urusi mjini Berlin mnamo 2020 - akitoa taarifa kuhusu anwani, nambari za simu na shughuli za watumishi mbalimbali wa serikali wa Uingereza.

    Alikusanya taarifa za siri juu ya uendeshaji na mpangilio wa ubalozi, ambao ulisemekana kuwa na manufaa kwa "adui, yaani hali ya Kirusi". Baadhi ya nyenzo hizi ziliainishwa kama "siri" na zinazohusiana na shughuli za serikali ya Uingereza na ubalozi wake wa Ujerumani.

    Waendesha mashtaka walisema alisukumwa na chuki kali kwa nchi yake na kukasirishwa na kitendo cha kupeperushwa kwa bendera ya Upinde wa mvua kuunga mkono jumuiya ya wapenzi wa jinsi moja (LGBT).

    Alikamatwa mnamo Agosti 2021 na euro 800 (£ 700) za pesa zilipatikana nyumbani kwake huko Potsdam, Ujerumani.

    Smith, ambaye sasa hana makazi maalum, alikiri mashtaka mnamo 4 Novemba, lakini vizuizi vya kuripoti viliwekwa hapo awali.

    Waliondolewa siku ya Ijumaa baada ya upande wa mashtaka kudokeza kuwa haungeomba kusikizwa kwa shtaka la tisa ambalo alikana.

    Smith atahukumiwa siku zijazo na atakabiliwa na kifungo cha miaka 14 jela.

  14. Mapigano dhidi ya M23 yashamiri Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.

    Wakaazi wa jimbo la kivu kaskazini, mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasi ya Congo wanasema kumekuwa na mapigano makali kati ya waasi wa M23 na jeshi la serikali.

    Wiki hii jeshi la anga limetumia helikopta na ndege za kivita kulilenga kundi hilo.

    Waasi hao wanadhaniwa kuhusika na uvamizi dhidi ya shule sita za msingi na kupora akiba ya chakula.

    Ghasia hizo zimechangia kuzorota kwa uhusiano baina ya Congo na Rwanda.

    Kila upande ukituhumu mwenzake kwa kuunga mkono makundi tofauti ya waasi. Tuhuma ambazo pande zote zinakana.

    Jitihada za kidiplomasia zinaendelea katika kurudisha uhusiano baina yan chi hizo mbili Jirani.

    Rais wa Angola João Lourenco amerudi katika eneo hilo kama mpatanishi. Jitihada zake zinaonekana muhimu na bora kabisa kusitisha maelfu zaidi ya watu wanaolazimika kuyaacha makaazi yao wakitotroka vita.

  15. Vita vya Ukraine: Sherehe zatawala Ukraine wakati ikirudisha mji muhimu wa Kherson

    Wanajeshi wa Ukraine wamekaribishwa mjini Kherson na wakaazi waliojawa na furaha, baada ya Urusi kusema kuwa imejiondoa kikamilifu katika mji huo muhimu wa kusini.

    Video ilionyesha wenyeji mitaani, wakipeperusha bendera ya taifa ya Ukraine na kuimba huku wanajeshi wa Kyiv wakiwasili.

    Wengine waliimba nyimbo za kizalendo karibu na moto mkubwa wa kambi hadi usiku.

    Kherson ilikuwa mji mkuu wa kikanda pekee uliochukuliwa na Urusi baada ya uvamizi wa Februari. Kurudi nyuma kumeonekana kama moja ya vikwazo vyake vikubwa vya vita.

    Moscow ilisema wafanyakazi 30,000 wametolewa nje ya eneo hilo - pamoja na vipande karibu 5,000 vya vifaa vya kijeshi, silaha na mali nyingine.

    Ikulu ya White House ilisifu kile ilichokiita "ushindi wa ajabu", huku Rais wa Ukraine Zelensky akiitaja "siku ya kihistoria".

    Lakini waziri wa mambo ya nje wa Ukraine alisema "vita vinaendelea". Akizungumza nchini Cambodia kando ya mkutano wa kilele wa nchi za Asia, Dmytro Kuleba alisema: "Tunashinda vita vya chinichini. Lakini vita vinaendelea."

    Taarifa ya jioni siku ya Ijumaa kutoka upande wa Ukraine ilisema kuwa wanajeshi walikuwa wamesonga mbele hadi ukingo wa magharibi wa mto Dnipro.

    Picha pia ziliibuka zikionyesha kuwa kivuko kikuu cha mto - Daraja la Antonivsky - kilikuwa kimeporomoka kwa kiasi. Bado haijafahamika jinsi uharibifu huo ulivyosababishwa.

    Wanajeshi wa Urusi walioikalia Kherson wanafikiriwa kuchukua nafasi mpya upande wa mashariki wa mto.

    Mkazi wa Kherson alielezea hisia zake "zinazolemea" wakati watu walipoibuka wakiimba na kucheza barabarani.

    Alexei Sandakov alifichua jina lake kamili kwa BBC, hapo awali alijiita "Jimmy". Alisema Kherson alikuwa "huru sasa. Ni tofauti. Kila mtu analia tangu asubuhi".

    Aliongeza kuwa "kila mtu alitaka kukumbatia" askari wa Kiukreni waliowasili.

    Mabadiliko ya udhibiti wa jiji hilo yalifuatia shambulio la haraka la Kiukreni katika miezi ya hivi karibuni, ambapo Kyiv ilisema kuwa imeteka tena makazi 41 karibu na Kherson.

    Katika hotuba yake ya jioni, Rais Zelensky alisema watu wa Kherson "walikuwa wakisubiri" na "hawakukata tamaa juu ya Ukraine".

    Aliongeza kuwa wakaazi wamekuwa wakifanya kazi ya kuondoa "athari zozote za wakaaji" kutoka barabarani, zikiwemo nembo za Kirusi.

    Wakati huo huo, msemaji wa Rais wa Urusi Vladimir Putin alikanusha hatua hiyo iliwakilisha kushindwa kwa aibu.