Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

IEBC yaagizwa kumruhusu Raila Odinga kutazama sava za matokeo ya Uchaguzi

Mahakama ya Juu imeamuru tume ya uchaguzi IEBC kumpa mgombea urais wa Muungano wa Azimio Raila Odinga idhini ya kutazama sava za tume ya Uchaguzi katika Kituo cha Kitaifa cha Kujumlisha kura ambazo huenda zilitumika kuhifadhi na kusambaza taarifa za upigaji kura.

Moja kwa moja

  1. Makamishna wanne wa IEBC wapata pigo

    Mahakama ya Juu imetupilia mbali majibu yaliyowasilishwa kwa niaba ya shirika la uchaguzi na makamishna wanne wakiongozwa na naibu mwenyekiti Juliana Cherera, na kutoa ushindi wa mapema kwa mwenyekiti Wafula Chebukati.

    Akizungumza Jumanne wakati wa kikao cha pili cha malalamishi ya kesi ya uchaguzi wa urais ya 2022 katika Mahakama ya Milimani, Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu alisema mahakama imemuamuru Mwanasheria Mkuu Prof Githu Muigai, ambaye anawakilisha kundi la Chebukati kuwa wakili anayewakilisha Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) katika suala hilo.

    Mrengo unaoongozwa na Juliana Cherera ulikuwa umemwasilisha mbele ya mahakama hiyo Wakili Paul Muite kama wakili wa IEBC.

    Lakini mwendo wa alasiri, mahakama iliwapatia pigo makamishna wanne -- Bi Cherera, Bi Irene Masit, Bw Justus Nyang'aya na Bw Francis Wanderi -- huku ikifafanua kuwa wako huru kuhifadhi huduma za Bw Muite na Issa Mansu kwa muda wa kesi hiyo.

    Katika kikao cha asubuhi, mawakili wote wawili walikuwa wamesisitiza kuwa wanawakilisha IEBC katika ombi la kupinga uchaguzi wa urais lililowasilishwa na kiongozi wa Azimio Raila Odinga.

    Mrengo unaoongozwa na Cherera ulikuwa umewasilisha jibu kwa niaba ya IEBC iliyotaka kubatilishwa kwa matokeo ya uchaguzi wa Rais yaliyomtangaza William Ruto kuwa Rais mteule.

    Katika usomaji wa awali wa uamuzi wa mahakama, Jaji Mwilu alikuwa amewataka makamishna wanaogombana wa shirika la IEBC kutatua mizozo yao ya ndani nje ya mahakama. Bi Mwilu alikuwa amesema mahakama haitajiingiza katika suala la kuamua ni wakili gani atawakilisha IEBC.

  2. Na kufikia hapo ndio tunakamilisha matangazo yetu kwa hii leo.

  3. Wanajeshi wa Ukraine:Tunaipiga Urusi kwa mashambulio ya usahihi wa hali ya juu

    Utawala wa kijeshi wa Ukraine unasema kuwa wanajeshi wake wanaoshambulia wanajeshi wa Urusi wanaoshikilia mji wa Kherson wamefanikiwa "kuharibu maghala, mengi ya silaha na sehemu za udhibiti wa adui kwa mashambulizi ya usahihi wa hali ya juu"

    Wanajeshi hao pia wameweza kusababisha uharibifu wa "madaraja kuvuka Dnipro", maafisa walisema katika ujumbe uliotumwa kwa Telegram, na kuifanya "kuweza kukata mawasiliano ya jeshi la Urusi kutoka kwa usambazaji wa silaha na wanajeshi wake kutoka Crimea".

    Shirika la habari la serikali ya Urusi Tass limeripoti kuwa Urusi inatumia mifumo ya ulinzi wa anga katika jaribio la kukabiliana na mashambulizi ya Ukraine katika eneo hilo.

  4. Majeshi ya umoja wa Sudan Kusini hatimaye yafuzu

    Zaidi ya wanajeshi 21,000 wamefuzu nchini Sudan Kusini, kama sehemu ya kikosi cha pamoja kitakachosimamia usalama wa nchi hiyo.

    Hii inafuatia kuongezwa kwa makataa kadhaa baada ya makubaliano ya amani ya mwaka 2018, ambayo yanahitaji kwamba pande zote zinazopigana ziweke silaha zao chini na kuunda jeshi la pamoja la serikali.

    Wanajeshi wengi katika hafla hiyo, hapo awali walikuwa wa vikundi tofauti vya mapigano.

    Lakini leo, waliahidi utii kwa nchi yao.

    Vikosi vya umoja ni pamoja na jeshi, polisi na maafisa wa huduma ya magereza.

    Waziri wa Ulinzi Angelina Teny aliambia vyombo vya habari vya ndani siku ya Jumatatu kwamba idara yake sasa itaanza kupeleka vikosi vya usalama kwao na kwamba kundi lingine litahitimu katika kipindi cha takriban miezi sita.

    Viongozi wa kanda, ambao ni wadhamini wa mkataba huo wa amani, walishuhudia sherehe za kuhitimu.

    Mnamo mwaka wa 2013, vita vilizuka nchini Sudan Kusini kati ya vikosi vinavyomuunga mkono Rais Salva Kiir na makamu wake wa wakati huo Riek Machar.

    Maelfu ya raia waliuawa, na wengine kuyahama makazi yao.

    Mkataba wa amani uliotiwa saini mnamo mwaka 2018 ulimaliza mapigano mengi, na ilikubaliwa kuwa takriban wanajeshi 80,000 wafunzwe kwa ajili ya kikosi cha usalama kilichoungana.

    Serikali ya pamoja ya mpito iliundwa mwaka 2020, ikiwa na mipango ya kufanya uchaguzi mwezi Desemba, lakini uchaguzi huo umeahirishwa hadi 2024.

    Sudan Kusini inakabiliwa na hali tete ya amani na makundi yenye silaha bado yanafanya kazi katika baadhi ya maeneo.

  5. Tanzania imezindua sensa ya majengo,

    Tanzania leo imezindua sensa ya majengo kwa siku nne ili kujua idadi ya majengo, umiliki, gharama na upatikanaji wa miundombinu muhimu katika makazi yote nchini humo.

    Aidha Kamishina wa Sensa,Anna Makinda amesema kufikia jana Jumatatu, zaidi ya asilimia 93 ya kaya nchini humo tayari zilikuwa zimehesabiwa.

    Makinda alisema zoezi la kuhesabu kaya linaendelea vyema na sasa wanaendelea na usimamizi wa sensa ya majengo itakayosaidia kutambua umiliku wa makazi, ubora wa nyumba lakini pia kurahisisha upatikanaji wa maji, umeme, barabara na kadhalika.

    Pia kwa mujibu wa mamlaka nchini humo, takwimu hizo za sensa ya majengo na mali zisizohamishika zitasaidia katika kuboresha sera ya makazi.

    Katika sensa ya watu ya mwaka 2012, ilibainika kuwa kati ya nyumba milioni 9.3 zilizokuwepo nchini Tanzania, nyumba milioni 6.3 ziliezekwa kwa mabati na milioni tatu ziliezekwa kwa udongo.

    Soma zaidi:

  6. IEBC yaagizwa kumruhusu Raila Odinga kutazama sava za matokeo ya Uchaguzi

    Mahakama ya Juu imeamuru tume ya uchaguzi IEBC kumpa mgombea urais wa Muungano wa Azimio Raila Odinga idhini ya kutazama sava za tume ya Uchaguzi katika Kituo cha Kitaifa cha Kujumlisha kura ambazo huenda zilitumika kuhifadhi na kusambaza taarifa za upigaji kura.

    Mahakama pia iliagiza tume hiyo kumpa masanduku ya kura ya vituo mbalimbali vya kupigia kura kwa lengo la ukaguzi, ili kuchunguzwa na kuhesabiwa upya.

    Vituo hivyo ni pamoja na Shule ya Msingi ya Nandi Hills na Sinendeti huko Nandi, Belgut, Kapsuser na Shule ya Msingi ya Chepkutum katika Kaunti ya Kericho; Vituo vya Kupigia Kura vya Jomvi, Mikindani na Wizara ya Maji katika Kaunti ya Mombasa; Shule za Msingi ya Mvita, na Majengo katika Kaunti ya Mombasa; Tinderet CONMO, katika Kaunti ya Nandi; Jarok, Gathanji na Shule ya Msingi ya Kiheo katika Kaunti ya Nyandarua.

    Matokeo ya hesabu hiyo yanahitajika kuwasilishwa mbele ya mahakama hiyo hapo siku ya Alhamisi saa nane.

    Maagizo hayo yatamwezesha Bw Odinga na walalamishi wengine wa uchaguzi wa Rais kuthibitisha madai kwamba kura ziliibiwa.

    Kulingana na agizo hilo, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inahitajika kumpa Bw Odinga ufikiaji unaosimamiwa na seva zozote ambazo zinaweza kuhifadhi habari za kitaalamu zinazotumiwa kunasa nakala ya Fomu 34C ambayo ni jumla ya kura zilizopigwa.

    Walalamishi wengine watakaopewa fursa ya kutazama sava hizo ni pamoja na mgombea mwenza wa Bw Odinga Martha Karua, Youth Advocacy for Africa (YAA), Peter Kirika, Khelef Khalifa, George Osewe, Ruth Mumbi na Grace Kamau.

    IEBC pia iliamriwa kuwapa nakala za sera yake ya usalama ya mfumo wa teknolojia inayojumuisha sio tu sera ya neno la siri, matrix ya neno la siri na wamiliki wa nywila za usimamizi wa mfumo.

    Pia watapewa Habari zozote kuhusu utumiaji wa mfumo huo wa teknolojiana viwango vyake vya kuutumia , mazungumzo yaliofanyika ndani yake kwa utambulisho , ujumlishaji wa kura, upperushaji matokeo na uchapishaji matokeo hayo.

    Tukisalia katika masuala ya Teknolojia , IEBC itatoa sera yake ya usalama kuhusu utumiaji wa mfumo huo na idadi ya watu walioingia .

  7. Matokeo ya Uchaguzi Kenya 2022: Kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi nchini Kenya yaanza kusikilizwa

    Majaji saba wameanza kusikiliza maombi ya kutaka kubatilishwa kwa uchaguzi wa William Ruto kuwa rais mteule wa Kenya.

    Wakiongozwa na Jaji Mkuu Martha Koome, majaji hao walifutilia mbali maombi mawili na kuunganisha mengine saba kwa sababu yaliibua masuala sawa na kutaka maagizo sawa.

    Mahakama pia ilitupilia mbali maombi matatu likiwemo ombi la Bw Ruto, ambaye alitaka kukizuia Chama cha Wanasheria nchini Kenya kushiriki katika kesi hiyo.

    Mahakama imeweka masuala tisa ambayo yatachagiza uamuzi wa mwisho utakaotolewa tarehe 5 Septemba.

    Kiongozi mkongwe wa upinzani Raila Odinga alikataa matokeo ya uchaguzi akisema tangazo hilo lilikuwa kinyume cha sheria.

    Alitaja mgawanyiko kati ya makamishna saba wa uchaguzi na mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati kukosa kueleza jinsi alivyofika kwenye mchujo wa mwisho.

    Bw Chebukati alimtangaza Bw Ruto kuwa rais mteule wa Kenya akisema alipata kura 7.1m dhidi ya Bw Odinga kura 6.9m.

    Mahakama hiyo ambayo ilifanya kikao cha awali Jumanne asubuhi, imeahirisha kikao hicho na itaendelea tena alasiri ili kutafakari masuala kadhaa yaliyotolewa na mawakili.

    Kesi hiyo itaendelea kusikilizwa kikamilifu kuanzia Jumatano.

    Soma zaidi:

  8. Habari za hivi punde, Bournemouth yampiga kalamu kocha wake baada ya kipigo cha 9-0 na Liverpool

    Bournemouth imemfuta kazi kocha wake Scott Parker baada ya kufungwa magoli 9-0 na Liverpool Jumamosi, mechi nne tu baada ya msimu kuanza.

    Baada ya kupoteza, Parker, 41, alisema "hakushangazwa" na akasema timu "haikuwa katika kiwango cha kuikabili liverpool".

    "Ili tuendelee kusonga mbele kama timu na klabu kwa ujumla, ni lazima tuwe sawa katika mkakati wetu wa kuendesha klabu kwa uendelevu," alisema mmiliki wa klabu hiyo Maxim Demin.

    "Lazima pia tuonyeshe imani na kuheshimiana."

    Demin aliongeza: "Hiyo ndiyo njia ambayo imeiletea klabu hii mafanikio makubwa katika historia ya hivi karibuni, na ambayo hatutakengeuka kuanzia sasa. Utafutaji wetu wa kocha mkuu mpya utaanza mara moja."

    Kipigo cha Liverpool kilikuwa kipigo cha tatu mfululizo kwa Bournemouth kwenye ligi, baada ya kushinda mechi yao ya ufunguzi.

    Gary O'Neil atachukua usukani wa timu kwa muda na atasaidiwa na Shaun Cooper na Tommy Elphick.

  9. Umoja wa Ulaya unatayarisha kituo cha mafunzo ya kijeshi nchini Ukraine

    Mawaziri wakuu wa Umoja wa Ulaya, wanakutana katika Jamhuri ya Czech, huku mawaziri wa ulinzi wakienda kujadili jinsi ya kuanzisha kituo kikuu cha mafunzo kwa jeshi la Ukraine nchini humo.

    Wataalamu maalum wamekuwa wakitoa mafunzo kwa jeshi la Ukraine kwa muda, wengi wao wakifanya kazi na silaha mpya.

    Lakini mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya, Josep Borrell, alisema anatumai ‘’mafunzo ya hali ya juu’’ yatatolewa kwa vikosi vya Ukraine.

    Aliongeza kuwa mfumo wa kati wa mafunzo utaruhusu wataalam wa EU kutabiri vita, wakati huo huo kutoa msaada mkubwa kwa Waukraine.

    Kwa upande mwingine, mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya pia wamepangwa kukutana wiki hii, na matokeo ya mkutano wao kuwasilishwa kwa majadiliano kuhusiana na vikwazo vya visa kwa raia wa Urusi.

    Wanachama wa Umoja wa Ulaya wanatarajiwa kuendelea na majadiliano katika mji mkuu wa Czech wa Prague hadi Jumatano.

    Soma zaidi:

  10. Wagombea wa Muungano wa Azimio washinda ugavana Mombasa na Kakamega

    Mgombea wa chama cha ODM Fernandes Odinga Barasa ameshinda kinyang’anyiro cha kuwania kiti cha Ugavana katika kaunti ya Kakamega nchini Kenya baada ya kumshinda mpinzani wake wa chama cha Amani National Congress ANC Cleophas Malala.

    Bwana Baraza alitangazwa mshindi baada ya kujipatia kura 192,929 ikilinganishwa na Bwana Malala aliyepata kura 159,508.

    Baada ya kutangazwa mshindi , bwana Barasa aliambatana na mkewena wafuasi wake katika kituo kikuu cha kujumlisha kura cha Kakamega ili kuchukua cheti chake cha ushindi.

    Akizungumza baada ya kukabidhiwa cheti hicho, Baraza alikishukuru chama cha ODM , mtangulizi wake Wycliffe Oparanya na mgombea wa urais wa Muungano wa Azimio Raila Odinga kwa kumuunga mkono.

    Wakati huohuo Abdulswamad Nassir wa chama cha Orange Democratic Movement ndiye gavana mteule wa Mombasa baada ya kupata kura 119,083 dhidi ya mpinzani wake wa karibu wa UDA Hassan Omar aliyepata kura 98,108.

    Mapema Jumanne asubuhi, matokeo yaliyojumlishwa kutoka takriban maeneo bunge yote ya Mombasa yalionyesha mgombeaji wa ODM akiwa anaongoza katika kinyang'anyiro cha ugavana. Matokeo kutoka eneo bunge la Likoni ndiyo yaliyokuwa yakisubiriwa.

    Hatahivyo ushindi wa Barasa unajiri kama pigo kwa kambi ya Muungano wa Kenya Kwanza unaoongozwa na rais mteule William Ruto na kiongozi wa ANC Musalia Mudavadi ambao ulijaribu kila njia kukinyakua kiti hicho kutoka kwa Muungano wa Azimio la Umoja.

    Uchaguzi huo ulikumbwa na tatizo la idadi ndogo ya wapiga kura waliojitokezasiku ya Jumatatu na ushindi huo wa Barasa umeongeza nguvu kwa Muungano wa Azimio na mgombea wake wa urais Raila Odinga katika mkoa wa Magharibi.

    Kulikuwa na wagombea saba waliokuwa wakigombea kiti cha ugavana. Walijumuisha aliyekuwa Mbunge wa Lugari Cyrus Jirongo (UDP) aliyepata kura 5,974, Bw Suleiman Sumba (Kanu) kura 178, Samuel Omukoko (MDP) kura 761, wakili Michael Osundwa (Independent) alipata kura 1,146 naye Austin Opitso Otieno (Huru) alipata kura 761.

    Uchaguzi wa kaunti za Kakamega na Mombasa uliahirishwa baada ya makaratasi ya kupigia kura kuchanganyika na yale ya kaunti nyengine.

    Katika kinyang'anyiro cha ubunge wa Pokot Kusini, David Pkosing aliyemaliza muda wake alimshinda Simon Kalekem wa United Democratic Alliance (UDA) baada ya kupata kura 28,225. Mgombea wa UDA alipata kura 15, 295.

    Kwengineko, Titus Lotee amembwaga mbunge wa zamani Mark Lomunokol kunyakua kiti cha Eneobunge la Kacheliba. Lomunokol was vying on a UDA party ticket. Totee alipata kura 20,073 naye Lomunokol akapata kura 17, 963.

    Kati uchaguzi wa ubunge wa Kitui vijijini, David Mwalika wa chama cha Wiper alimpiku mpinzani wake wa karibu Charles Nyamai wa UDA baada ya kujizolea kura 19,745. Nyamai alipata kura 10,178.

    Hata hivyo chama cha UDA kilishinda kiti cha eneo bunge la Rongai kupitia mgombea wake Paul Chebor ambaye alimbwaga Raymond Moi wa chama KANU.

    Cheboi alipata jumla ya kura 27,021 huku mwana wa rais wa zamani wa Kenya hayati Daniel Moi akipata kura 14,725.

    Chaguzi katika maeneo bunge hayo manne uliahirishwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Ukaguzi wa Mipaka (IEBC) kufuatia mkanganyinyiko uliotokea wakati wa kuchapisha makaratasi ya kupigia kura .

    Kufuatia matokeo ya uchaguzi huo wa hivi punde, Azimio sasa ina wanachama 165 huku Kenya Kwanza ikipanda hadi 160 kutoka 159.

  11. Nasa inasema hii ndio sauti inayosikika katika shimo jeusi kwenye anga za mbali

    Katika ombwe la anga za mbali, hakuna mengi unayoweza kusikia. Lakini angaza mbali unaweza kusikia kelele katika eneo linalozingira Shimo Jeusi.

    Shirika la anga za mbali la Marekani Nasa limetoa sauti zinazotoka kwenye moja ya mahimo ambalo liko katikati ya uzio wa nyota wa Perseus galaxy.

    Ilisema Nasa: ‘Uzio wa nyota una kiasi kikubwa cha gesi nyingi ambacho kimekuwa na sauti inayosikika.

    Hii ni sauti yake iliyokuzwa na kuchanganywa na data nyingine, ili kuisikia sauti ya Shimo Jeusi!.'

    Mashimo Meusi yanadhaniwa kuwa yametokana na kuporomoka kwa nyota nyingi sana.

  12. Warusi lazima watoroke ikiwa wanataka kunusurika- Zelensky

    Ikiwa wanataka kunusurika, ihuu ndio wakati wa wanajeshi wa Urusi kutoroka, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alidai katika hotuba yake ya kila siku kwa taifa jana usiku wakati alipokuwa akijadili matukio ya hivi punde dhidi ya vikosi vya Urusi upande wa kusini maeneo ya Kherson.

    Mpaka kati ya nchi hizo mbili haujabadilika, alisema, akiongeza kuwa “wavamizi wanajua hilo” na Ukraine itawafurusha nchini humo.

    “Ukraine inarejelea hali yake ya kawaida,” Zelensky aliwaambia watu wa Ukraine. “Na itakomboa maeneo ya Kharkiv, Luhansk, Donetsk, Zaporizhzhia, Kherson, Crimea, na kwa ujumla maeneo yote yanayozunguka Bahari Nyeusi na Bahari ya Azov - kutoka Kisiwa cha Zmiinyi hadi Kerch Strait.

    “Hili litafanyika. Haya ni maeneo yetu. Na kama jamii yetu inavyoelewa. Hauna eneo lao katika ardhi ya Ukraine.”

    Alisema tangu kuanza kwa vita mwaka 2014 na Urusi kunyakuwa Crimea na kujaribu kuteka eneo la Donbas “lazima ikomee hapo”, baada ya maeneo hayo mawili kukombolewa.

    Unaweza pia kusoma

  13. Kikosi cha kwanza cha muungano chahitimu Sudan Kusini

    Sudan Kusini iko tayari kwa mahafali ya kundi lake la kwanza la vikosi vya muungano nchini humo - jeshi la taifa na huduma za polisi.

    Mahafali yaliyopangwa kufanyika Jumanne asubuhi katika mji mkuu, Juba, yanatarajiwa kushuhudiwa na viongozi watano kutoka eneo hilo - ambao ni wadhamini wa makubaliano ya amani. Sikukuu ya umma imetangazwa ili kuwawezesha wananchi kushuhudia sherehe hizo.

    Serikali ya umoja wa Sudan Kusini iliundwa Februari 2020, lakini bado haijaunda jeshi la umoja wa kitaifa. Waziri wa Ulinzi na Masuala ya Wastaafu Angelina Teny aliwaambia waandishi wa habari Jumatatu kwamba angalau wanajeshi 10,000 watahitimu wakati wa sherehe rasmi.

    Alisema kundi lijalo la vikosi vya umoja linatarajiwa kuhitimu katika kipindi cha miezi sita ijayo. Nguvu ya umoja ilikuwa nguzo muhimu ya mkataba wa amani ulioimarishwa uliotiwa saini Septemba 2018 ili kumaliza miaka mitano ya mzozo.

    Hadi wanajeshi 83,000 awali walitakiwa kujiunga na jeshi la taifa, lakini makubaliano mapya yaliyofikiwa mwezi Aprili mwaka huu yalikubaliwa kuhusu wanajeshi 53,000.

    Tangu uhuru, Sudan Kusini imekumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyosababisha maelfu ya watu kuuawa, huku makundi yanayopigana yakigawanyika kwa misingi ya kikabila.

  14. Meli ya nafaka ya Ukraine yatia nanga nchini Djibouti

    Meli iliyobeba nafaka ya Ukraine imetia nanga katika taifa la Afrika Mashariki la Djibouti.

    Ni shehena ya kwanza ya nafaka kutoka Ukraine hadi Afrika tangu uvamizi wa Urusi.

    Usafirishaji kwenye meli hiyo ‘Brave Commander’ umepangwa na UN ili kufikisha ngano hiyo katika nchi zilizo hatarini kukumbwa na njaa.

    Inapaswa kuchukua takriban siku nne kushusha na kubeba mizigo kabla ya kusafirishwa kwa barabara hadi nchi jirani ya Ethiopia, ambako zaidi ya watu milioni 20 wanahitaji msaada wa chakula.

    Ethiopia inakabiliwa na ukame mbaya zaidi kuwahi kutokea katika kipindi cha miaka 40, pamoja na mizozo kadhaa.

    Usafirishaji huo umepungua baharini ikilinganishwa na kile kinachohitajika katika nchi za Afrika Mashariki - ambako ukame umeenea.

    Unaweza pia kusoma

  15. Mafuriko Pakistan: Thuluthi moja ya nchi imesombwa na maji – waziri

    Thuluthi moja ya Pakistan imesombwa kabisa na maji ya mafuriko, waziri wake wa hali ya hewa anasema.

    Mafuriko hayo mabaya yamesomba barabara nyumbana mimea- na kuacha nyuma uharibifu mkubwa katika maeneo tofauti nchini Pakistan.

    "Kwote ni kama bahari kubwa, hakuna ardhi kavu ya kusukuma maji nje," Sherry Rehman alisema, akiutaja kuwa "mgogoro mkubwa usiomithilika."

    Karibu wa 1,136 wameuawa tangu kuanza kwa msimu wa masika mwezi Juni, kulingana na maafisa.

    Mvua ya kiangazi ndiyo kubwa zaidi kurekodiwa katika muongo mmoja na serikali inasema imechangiwa na mabadiliko ya tabia nchi.

    "Kiuhalisia, theluthi moja ya Pakistan iko chini ya maji, hali ambayo haujawahi kushuhudia hapo awali," Bi Rehman aliambia shirika la habari la AFP.

    "Hatujawahi kuona kitu kama hiki," aliongeza waziri huyo.

    Akizungumza na BBC, Waziri wa Mambo ya Nje wa Pakistan Bilawal Bhutto-Zardari alisema thuluthi moja ya waliouawa wanaaminika kuwa watoto. "Bado tunaendelea kutathmini ukubwa wa uharibifu," aliongeza.

  16. Mahakama ya Juu Zaidi Kenya kufanya kikao cha kuweka mikakati ya kesi ya kupinga matokeo ya Urais

    Mahakama ya juu zaidi nchini kenya imepangiwa kufanya kikao cha kutathmini masuala yatakayoibuka kwenye kesi tisa zilizowasilishwa katika kupinga kutangazwa kwa William Ruto kuwa Rais Mteule.

    Kwenye tangazo lililotolewa na msajili wa mahakama hiyo, Bi Letizia Wachira, kikao hicho kimepangiwa kuanza leo katika Mahakama ya Milimani.

    Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Idara ya Mahakama, kesi hizo zitaanza kusikilizwa kesho Jumatano na kumalizika Jumapili.

    Majaji watapumzika kwa siku moja ili kutathmini masuala yatakayowasilishwa na pande zote. Baadaye, watarejea Jumatatu ili kutoa uamuzi wao.

    Wakati wa kikao cha leo Jumanne, mahakama itaeleza kanuni ambazo zitazingatiwa na walalamishi na mawakili wao.

    Huku hayo yakiarifiwa majaji watano kutoka mataifa ya kigeni wamefika nchini kufuatilia kesi ya kupinga matokeo ya urais itakayoanza leo saa tano katika Mahakama ya juu

    Majaji hao wanachama wa Chama cha Majaji wa Afrika (AJJF), walitua nchini siku ya Jumatatu wakiongozwa na Jaji Mkuu (mstaafu) Mohammed Chande Othman wa Tanzania.

    Majaji wengine katika ujumbe huo ni Lillian Tibatemwa-Ekirikubinza wa Mahakama ya Upeo Uganda, Ivy Kamanga wa Mahakama ya ya Upeo Malawi, Moses Chinhengo wa Mahakama ya Rufaa Lesotho na Henry Boissie Mbha ambaye ni Rais wa Mahakama ya Masuala ya Uchaguzi Afrika Kusini.

    Maelezo zaidi:

  17. Urusi kufanya mazoezi makubwa ya kijeshi na China pamoja na mataifa mengine

    Urusi imesema itaanzisha mazoezi makubwa ya kijeshi pamoja na vikosi kutoka China ili kuonyesha uhusiano wa karibu wa ulinzi kati ya Moscow na Beijing huku kukiwa na vita nchini Ukraine.

    Mazoezi ya Vostok 2022 (Mashariki 2022) yatafanyika Septemba 1-7 katika maeneo mbalimbali katika Mashariki ya Mbali ya Urusi na Bahari ya Japan na kuhusisha zaidi ya askari 50,000 na vitengo vya silaha 5,000, ikiwa ni pamoja na ndege 140 na meli za kivita 60, kulingana na ulinzi wa Urusi

    Wizara ya ulinzi Ilitoa video ya wanajeshi wa China wakiwasili nchini Urusi kwa ajili ya maandalizi ya zoezi hilo kubwa.

    Mazoezi hayo yatafanyika katika vituo saba vya kurusha risasi mashariki mwa Urusi na yatashirikisha wanajeshi kutoka mataifa kadhaa ya zamani ya Usovieti, China, India, Laos, Mongolia, Nicaragua na Syria.

    Wizara hiyo ilisema vitengo vya wanajeshi wa anga vya Urusi, walipuaji wa masafa marefu, na ndege za kijeshi za shehena zitashiriki katika mazoezi hayo pamoja na vikosi vingine.

    Wakati wa kwanza kutangaza zoezi hilo mwezi uliopita, jeshi la Urusi lilisisitiza kuwa ni sehemu ya mafunzo ya mapigano yaliyopangwa ambayo yanaendelea licha ya hatua ya kijeshi ya Moscow nchini Ukraine. Haijafichua idadi ya wanajeshi waliohusika katika kile Kremlin inachokiita "operesheni maalum ya kijeshi" huko.

    Unaweza pia kusoma

  18. Hujambo na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja leo.