Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Silaha za nchi za magharibi zaonekana Urusi

Tayari kumeripotiwa kuonekana kwa silaha zinazotolewa na nchi za Magharibi ndani ya Urusi, tangu Ukraine ilipoanzisha mashambulizi yake mapya mapema mwezi huu.

Muhtasari

  • Mazungumzo ya kusitisha mapigano Gaza, kuwaachilia mateka yaanza tena Doha
  • MPOX yasababisha vifo vya watu zaidi ya 500 mwaka huu DRC
  • Shutuma zalifanya jiji la Eldoret kuondoa sanamu za 'wanariadha' wa Kenya
  • Uvamizi wa Ukraine nchini Urusi: Tunachofahamu kufikia sasa
  • Ni silaha gani za Magharibi zimetolewa kwa Ukraine hadi sasa?
  • Mwanamke mwenye uraia wa Marekani na Urusi afungwa miaka 12 jela kwa kosa la uhaini
  • Zaidi ya watu 40,000 waliuawa huko Gaza, wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas yasema
  • Baba yake nyota wa Barcelona Lamine Yamal achomwa kisu
  • Silaha za nchi za magharibi zaonekana Urusi
  • Kikosi cha anga cha Ukraine chasema kilidungua ndege 29 za Urusi usiku kucha
  • Ukraine iko 'huru kutumia' silaha za Uingereza Urusi
  • Korea Kaskazini kufunguliwa tena kwa utalii baada ya miaka mitano
  • India: Wanawake waandamana usiku kulalamikia mauaji ya daktari tarajali
  • Rais wa zamani wa Argentina ashutumiwa kwa kumdhalilisha mpenzi wake
  • Hamas haitajiunga na mazungumzo ya kusitisha mapigano Gaza
  • Columbia: Rais wa chuo kikuu ajiuzulu baada ya maandamano kuhusu Gaza
  • WHO yatangaza mlipuko wa Mpox kuwa dharura ya kiafya duniani
  • Ukraine yaendelea kusonga mbele ndani ya eneo la Urusi

Moja kwa moja

Asha Juma

  1. Habari za hivi punde, Mgonjwa wa kwanza wa Mpox apatikana Sweden

    Wakala wa afya ya umma nchini Sweden imerekodi kile inachosema kuwa ni kisa cha kwanza cha aina mpya ya ugonjwa wa mpox nje ya bara la Afrika.

    Mtu huyo aliambukizwa alipokuwa akikaa katika eneo la Afrika ambako kwa sasa kuna mlipuko mkubwa wa mpox Clade I, shirika hilo lilisema.

    Habari hizo zinakuja saa chache baada ya Shirika la Afya Duniani (WHO) kutangaza kwamba mlipuko wa ugonjwa wa mpox katika baadhi ya maeneo ya Afrika sasa ni dharura ya afya ya umma ambayo inatia wasiwasi kimataifa.

    Takribani watu 450 walikufa wakati wa mlipuko wa awali katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

  2. Mazungumzo ya kusitisha mapigano Gaza, kuwaachilia mateka yaanza tena Doha

    Mazungumzo kuhusu kusitisha mapigano na kuachiliwa huru kwa mateka katika Ukanda wa Gaza yameanza tena nchini Qatar, huku idadi ya Wapalestina walioripotiwa kuuawa katika vita kati ya Israel na Hamas ikizidi 40,000.

    Makubaliano yanaonekana kama chachu ya kusitisha mzozo wa miezi 10 unaoendelea hadi katika vita vya kikanda vinavyohusisha Iran, lakini matarajio ya mafanikio ni madogo.

    Hamas imesema haitashiriki katika mazungumzo ya moja kwa moja huko Doha kwa sasa, ingawa wapatanishi wanatarajiwa kupeleka ujumbe kwa maafisa wa kundi hilo lenye silaha walioko huko.

    Imetoa wito wa kubuniwa kwa msingi wa pendekezo lililotolewa na rais wa Marekani na kumshutumu waziri mkuu wa Israel kwa kuongeza masharti mapya, jambo ambalo amelikanusha.

    Wapatanishi kutoka Marekani, Qatar na Misri wanakabiliwa na mambo kadhaa yanayoweza kukwama, ikiwa ni pamoja na udhibiti wa ardhi kwenye mpaka wa Gaza na Misri na kurejea kwa raia wa Palestina waliokimbia makazi yao kaskazini mwa Gaza.

    Mazungumzo hayo yalisitishwa tangu kiongozi wa kisiasa wa Hamas na mpatanishi mkuu, Ismail Haniyeh, alipouawa mjini Tehran mwishoni mwa Julai.

    Iran imeapa kulipiza kisasi dhidi ya Israel, ambayo haijathibitisha wala kukanusha kuhusika na hivyo kuzua hofu ya kuongezeka kwa mzozo zaidi.

    Unaweza kusoma;

  3. MPOX yasababisha vifo vya watu zaidi ya 500 mwaka huu DRC,

    Wizara ya Afya katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imesema Homa ya Nyani MPOX imesababisha vifo vya watu mia tano arobaini na wanane mwaka huu,huku mikoa yote nchini humo ikiripotii visa vya ugonjwa huo.

    Waziri wa afya w DRC Samuel Roger Kamba amesema nchi hiyo imerekodi visa takribani 15,600 na zaidi ya vifo mia tano tangu kuanza kwa mwaka huu.

    DRC ina majimbo ishirini na sita na idadi jumla ya watu milioni mia moja.

    Bwana Kamba amesema Majimbo yaliyoathirika vibaya na MPOX ni Kivu Kusini, Kivu Kaskazini,Tshopo,Equateur,North Ubangi,Tshuapa,Mongala na Sankuru.

    Hapo jana,shirika la afya duniani WHO lilitagaza kuwa MPOX ni dharura ya afya ya umma duniani kutokana na kuongezeka kwa visa vya homa hiyo ya nyani DRC na katika mataifa jirani na nchi hiyo.

    Uamuzi huo wa WHO ulikuja siku moja baada ya shirika la kudhibiti magonjwa Afrika CDC kutangaza pia MPOX ni dharura ya afya ya umma barani Afrika.

    Unaweza kusoma;

  4. Shutuma zalifanya jiji la Eldoret kuondoa sanamu za 'wanariadha' wa Kenya

    Mamlaka katika mji wa Eldoret nchini Kenya imeondoa sanamu za wanariadha watatu baada ya kukejeliwa na kuelezewa kuwa ni "aibu" na "mzaha".

    Sanamu hizo zilizinduliwa kabla ya sherehe za Alhamisi kulipa hadhi jiji la Eldoret.

    Hata hivyo, wakazi wa eneo hilo na Wakenya mtandaoni walisema sanamu hizo hazifanani na wanariadha wanaodaiwa kuwawakilisha.

    Eldoret inajulikana kama "Sehemu ya mabingwa", kama ilivyo katikati mwa Bonde la Ufa, ambapo wanariadha wengi wa Kenya wanaoshinda ulimwengu wanatoka.

    Sanamu hizo ziliondolewa usiku kucha kabla ya Rais William Ruto kuuteua rasmi mji wa Eldoret kuwa jiji. Jiji hilo wiki hii lilizindua kazi zake za sanaa, zikiwemo sanamu tatu za wanariadha .

    Sanamu hizo zililenga kuwakilisha urithi wa michezo na kilimo katika eneo hilo na ziliwekwa katika barabara tofauti za mji huo.

    Lakini mara moja zilikosolewa na wengi, na badala yake kuwa vitu vya dhihaka badala ya vitu vilivyowekwa kwa Wakenya kujivunia.

    Mkenya mmoja ambaye alisambaza picha ya sanamu ya mwanariadha wa kike anayeshukiwa kumwakilisha mwanariadha aliyeshikilia rekodi ya dunia ya mita 1,500, Faith Kipyegon, alisema kazi hizo zinawakilisha "usawa wetu wa umoja kama nchi".

    "Ni aibu kuiita sanamu ya Faith Kipyegon," Mkenya mwingine kwenye X alisema.

    Mtumiaji mwingine wa X alisambaza sanamu inayodaiwa kuwa ya gwiji wa mbio za marathon Eliud Kipchoge akiiita "mzaha", akisema "yeyote aliyefanya hivi hataiona mbingu".

    Ripota wa eneo hilo aliambia BBC kwamba maafisa wa kaunti waliondoa sanamu hizo tatu usiku wa kuamkia leo, wawili wakiwakilisha wanariadha wa kike na mmoja wa mwanamume, na kuwapeleka kusikojulikana.

    Mamlaka haijaonyesha wanamwakilisha nani lakini watumiaji wa mitandao ya kijamii wametaja moja kama sanamu ya Kipyegon na nyingine ya Kipchoge.

    Lakini taswira yao ya wanariadha hao imeelezwa kuwa "isiyo na aibu", na "chini ya kiwango".

    Wakenya mtandaoni wamekuwa wakiunga mkono kuondolewa kwa sanamu hizo. Haikuwa wazi kama zingebadilishwa, na lini.

    Kabla ya hafla ya kutangaza Eldoret kuwa jiji la tano la Kenya, Rais Ruto aliwakaribisha wanariadha walioshinda medali katika Michezo ya Olimpiki ya 2024.

    Kila mmoja wao alituzwa pesa kwa mujibu wa mpango wa serikali uliokusudiwa kuwahamasisha wanariadha kwa utendaji mzuri.

    Kenya ilikuwa nchi iliyoorodheshwa ya juu zaidi barani Afrika katika Michezo ya Olimpiki ya Paris, ikishika nafasi ya 17 kwenye jedwali la medali ikiwa na dhahabu nne na jumla ya medali 11.

    Kipyegon alishinda taji la mita 1,500 katika rekodi mpya ya Olimpiki ya dakika 3 na sekunde 51.29, akiwa mwanamke wa kwanza kushinda dhahabu tatu mfululizo katika mashindano hayo.

    Pia alishinda medali ya fedha katika mbio za mita 5,000.

    Hata hivyo, bingwa wa mbio za marathon Kipchoge hakumaliza mbio zake baada ya jeraha la mgongo kumlazimu kujiondoa.

  5. Uvamizi wa Ukraine nchini Urusi: Tunachofahamu kufikia sasa

    Asubuhi ya leo tumekuwa tukikuletea matukio katika vita vya Ukraine kufuatia uthibitisho kutoka kwa Wizara ya Ulinzi kwamba Ukraine inaweza kutumia silaha za Uingereza katika ardhi ya Urusi - isipokuwa makombora ya masafa marefu ya Storm Shadow.

    Serikali ilisema hii haiwakilishi mabadiliko ya sera.

    Tangu wakati huo chanzo cha habari cha Uingereza kimeithibitishia BBC kwamba mizinga ya Challenger 2 imetumika wakati wa uvamizi wa Urusi nchini Ukraine.

    Uingereza ilikuwa imeipa Ukraine mizinga 14 ya aina hiyo mwaka jana.Wakati huo huo, jeshi la wanahewa la Ukraine lilisema liliangusha ndege 29 za Urusi usiku kucha - na kuongeza kuwa mtu mmoja aliuawa na 13 kujeruhiwa.

    Kulingana na shirika la habari la serikali TASS hali ya dharura imetangazwa katika eneo la mpakani la Belgorod.

    Moscow imesema inawarudisha nyuma wanajeshi wa Ukraine, huku wizara ya ulinzi ya Urusi ikidai imelikomboa eneo la makaazi ya Krupets mjini Kursk.

  6. Ni silaha gani za Magharibi zimetolewa kwa Ukraine hadi sasa?

    Kama ambavyo tumekuwa tukiripoti, Wizara ya Ulinzi ya Uingereza imethibitisha kwamba Ukraine inaweza kutumia silaha za Uingereza katika ardhi ya Urusi.

    Ingawa hatujui hasa ikiwa au ni silaha gani zinaweza kutumiwa na vikosi vya Ukraine kusonga mbele, aina mbalimbali zimetolewa na nchi za Magharibi kufikia sasa.

    Miongoni mwa hayo ni makombora ya kifaru ya Javelin na Nlaw yaliyotolewa na Marekani na Uingereza.

    Marekani na Norway pia zimetoa Nasams (Mfumo wa Juu wa Kombora la Anga) kwa ajili ya ulinzi wa anga.

    Mnamo Julai tuliangalia kwa undani silaha zilizotolewa kwa Ukraine wakati huo.

    Unaweza kusoma;

  7. Mwanamke mwenye uraia wa Marekani na Urusi afungwa miaka 12 jela kwa kosa la uhaini

    Mahakama ya Urusi imemhukumu mchezaji mahiri wa balerina, Ksenia Karelina kifungo cha miaka 12 jela kwa kosa la uhaini kwa kutoa $51 (£39) kwa shirika la misaada linaloisaidia Ukraine.

    Karelina, ambaye ana uraia wa Marekani na Urusi, alikutwa na hatia wiki iliyopita baada ya kesi iliyosikilizwa bila kuwepo watu.

    Alikuwa akiishi Los Angeles na akawa raia wa Marekani mwaka wa 2021.

    Alikamatwa wakati wa ziara ya kifamilia Januari mwaka jana Yekaterinburg, yapata kilomita 1,600 (maili 1,000) mashariki mwa Moscow.

    Waendesha mashtaka walikuwa wameomba kifungo cha miaka 15 jela. Mahakama ya Yekaterinburg ilimpata na hatia ya uhaini mkubwa na kumhukumu kifungo cha jela katika jela ya serikali kuu. Karelina alikuwa ameshutumiwa na idara ya usalama ya FSB ya Urusi kwa kuchangisha pesa kwa ajili ya shirika la Ukraine linalotoa silaha kwa wanajeshi wa Ukraine.

    Wanaharakati wa haki za binadamu wa Urusi walisema alipokuwa akiishi Marekani alifanya uhamisho mmoja wa fedha wa $51.80 katika siku ya kwanza ya uvamizi wa Urusi nchini Ukraine tarehe 22 Februari 2022.

    FSB inadhaniwa kugundua shughuli hiyo kwenye simu yake. Wakili wake, Mikhail Mushailov, alisema Karelina alikubali tu kuhamisha pesa hizo na anaamini kuwa fedha hizo zingesaidia waathiriwa wa pande zote mbili.

    Aliviambia vyombo vya habari vya Urusi kuwa atakata rufaa dhidi ya hukumu hiyo.

    Shirika la hisani, Razom kwa ajili ya Ukraine, lilisema mapema mwaka huu "ilishtushwa" kusikia kuhusu kukamatwa kwa mchezaji mahiri wa ballerina na kukana kukusanya pesa kwa ajili ya silaha. Ilisema ni shirika la misaada lililoanzishwa na Marekani linalolenga misaada ya kibinadamu na maafa.

    Tangu kuanza kwa uvamizi kamili wa Urusi nchini Ukraine mnamo Februari 2022, mamlaka ya Urusi imedhibiti wapinzani na mashirika ya haki za binadamu yanasema zaidi ya kesi 1,000 za uhalifu zimefunguliwa dhidi ya wapinzani wanaopinga vita.

    Unaweza kusoma;

  8. Zaidi ya watu 40,000 waliuawa huko Gaza, wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas yasema

    Zaidi ya Wapalestina 40,000 wameuawa kutokana na hatua ya kijeshi ya Israel huko Gaza tangu shambulio la Oktoba 7 lililoongozwa na Hamas dhidi ya Israeli, wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas inasema.

    Idadi hiyo, 40,005 siku ya Alhamisi ni sawa na karibu 1.7% ya wakazi milioni 2.3 wa eneo hilo.

    Kando na vifo, uchambuzi wa picha za satelaiti unaonesha karibu 60% ya majengo huko Gaza yameharibiwa tangu mwanzo wa vita.

    Katika miezi michache iliyopita, mji wa kusini wa Rafah umepata uharibifu mkubwa zaidi, picha zinaonesha.

    Takwimu za wizara ya afya za idadi ya watu waliouawa hazitofautishi kati ya raia na wapiganaji.

    Hatahivyo, uchambuzi wake wa vifo vilivyoripotiwa unasema wengi ni watoto, wanawake au wazee.

    Mwezi huu, jeshi la Israel liliiambia BBC kuwa zaidi ya magaidi 15,000 waliuawa wakati wa vita.

    Waandishi wa habari wa kimataifa, ikiwa ni pamoja na BBC, wamezuiwa na Israel kuingia Gaza kwa kwa kujitegemea, hivyo hawawezi kuthibitisha takwimu kutoka upande wowote.

    Hapo awali, takwimu kutoka Wizara ya Afya ya Gaza (MoH) zilitumika sana nyakati za migogoro na kuonekana kuwa za kuaminika na Umoja wa Mataifa na taasisi za kimataifa. Ilihesabu tu vifo vilivyosajiliwa katika hospitali na hizi ziliingia katika mfumo mkuu pamoja na majina, nambari za utambulisho na maelezo mengine.

    Hata hivyo, mwishoni mwa mwaka jana Wizara ya Afya haikuweza kufanya kazi ipasavyo na vyumba vya kuhifadhia maiti vilivyofurika, mapigano ndani na karibu na hospitali na muunganisho duni wa intaneti na simu.

    Unaweza kusoma;

  9. Baba yake nyota wa Barcelona Lamine Yamal achomwa kisu

    Baba wa nyota wa soka wa Uhispania Lamine Yamal mwenye umri wa miaka 17 ameripotiwa kuchomwa kisu mara kadhaa kwenye eneo moja la maegesho ya magari.

    Kulingana na ripoti katika vyombo vya habari vya Uhispania, Mounir Nasraoui alishambuliwa katika mji wa pwani wa Mataró, kaskazini mwa Barcelona, ​​Jumatano usiku na kundi la watu aliozungumza nao mapema mchana.

    Polisi wa Catalonia wamethibitisha kuwa takriban watu watatu wamekamatwa, shirika la habari la AFP linaripoti.

    Bw Nasraoui alipelekwa hospitalini mjini Barcelona akiwa katika hali mbaya lakini sasa anasemekana kuwa yuko sawa.

    Shambulio hilo lilifanyika karibu na kitongoji cha Rocafonda ambapo Yamal alikulia.

    Mapema siku hiyo, Bw Nasraoui inasemekana aligombana na kundi la watu aliokutana nao alipokuwa akimtembeza mbwa wake, gazeti la Uhispania El Pais liliripoti.

    Saa kadhaa baadaye, alifikiwa na kundi lile lile kwenye maegesho ya magari na kuchomwa kisu "mara kadhaa".Sababu ya kuchomwa kisu haijajulikana kwa sasa.Ripoti kwenye tovuti ya michezo ya Relevo ilisema kuwa Bw Nasraoui alitarajiwa kusalia hospitalini kwa siku mbili au tatu chini ya uangalizi.

    Lamine Yamal, mchezaji mwenye umri mdogo zaidi kuwahi kutokea nchini Uhispania, alishiriki michuano ya Euro 2024 ambapo alitajwa kuwa Mchezaji Chipukizi bora wa Mashindano hayo.

    Winga huyo alitoa pasi iliofungwa na Nico Williams likiwa, bao la ufunguzi wakati Uhispania ilipoilaza England 2-1 kwenye fainali iliyochezwa Berlin.

    Muda mfupi baada ya Uhispania kunyanyua kombe hilo, mashabiki walijipanga katika mitaa ya Mataró wakimshangilia nyota wao mchanga.

    Baada ya kukulia katika mji huo, Yamal alitumia baadhi ya miaka yake ya ujana katika chuo kikuu cha Barcelona cha La Masia.

  10. Silaha za nchi za magharibi zaonekana Urusi

    Tayari kumeripotiwa kuonekana kwa silaha zinazotolewa na nchi za Magharibi ndani ya Urusi, tangu Ukraine ilipoanzisha mashambulizi yake mapya mapema mwezi huu.

    Ni pamoja na magari ya kivita ya Bradley na Stryker yanayotolewa na Marekani pamoja na Marders zinazotolewa na Ujerumani.

    Hakujawa na picha zilizooneshwa kufikia sasa za mizinga ya Challenger ya Uingereza au mizinga ya Abrams ya Marekani kwenye eneo la mpaka.

    Hata hivyo, wataalamu wa kijeshi wa Magharibi wameangazia mafanikio ya mashambulizi ya Ukraine kwa kutumia askari pamoja na magari ya kivita, mizinga na vifaru pamoja na vita vya kielektroniki na ndege zisizo na rubani, kushambulia.

    Hilo lilikuwa jambo ambalo halikuwepo katika shambulio la mwaka jana la Ukraine Kusini na Mashariki mwa nchi hiyo, ambalo lilizuiliwa na ngome za Urusi zilizochimbwa sana na kufanya kuwa vigumu na hatari kutumia silaha.

    Moja ya mizinga 14 ya Uingereza iliyopewa Challenger 2 iliharibiwa katika shambulio hilo lililozuiwa. Vifaru vya Uingereza vilivyotolewa vimekuwa vikiendeshwa na Kikosi cha 82 cha Mashambulizi ya Anga cha Ukraine, ambao walipata mafunzo kwa mara ya kwanza nchini Uingereza jinsi ya kutumia Challenger 2.

    Imeelezwa kuwa Ukraine imetumia baadhi ya vitengo vyake vilivyofunzwa vyema na vilivyo na vifaa bora kufanya mashambulizi yake kwenye mpaka.

  11. Kikosi cha anga cha Ukraine chasema kilidungua ndege 29 za Urusi usiku kucha

    Jeshi la anga la Ukraine linasema kuwa lilidungua ndege zote 29 zisizo na rubani zilizorushwa usiku kucha na Urusi ambayo ililenga maeneo nane ya Ukraine, huku mtu mmoja akiuawa na 13 kujeruhiwa.

    Urusi pia ilirusha makombora matatu ya kh-59 wakati wa shambulio hilo, maafisa wa Ukraine walisema katika taarifa, na kuongeza kuwa uharibifu mdogo tu ndio ulioripotiwa.

    Magavana wa mikoa ya Kyiv, Poltava na Kirovohrad wanasema hakukuwa na majeruhi au uharibifu wa majengo katika eneo la kati la Cherkasy.

    Katika eneo la kusini la Mykolaiv, ndege tano zisizo na rubani zilidunguliwa wakati, ndege nane zisizo na rubani zilidunguliwa huko Kherson. Gavana wa Kherson anasema mashambulizi mbalimbali katika eneo hilo yameua mtu mmoja na kujeruhi 13.

  12. Ukraine iko 'huru kutumia' silaha za Uingereza kwenye ardhi ya Urusi - Wizara ya Ulinzi

    Vikosi vya Ukraine vinaweza kutumia silaha za Uingereza katika ardhi ya Urusi wakati ikijilinda, Wizara ya Ulinzi imethibitisha.

    Msemaji wa wizara hiyo amesema Ukraine ina "haki ya wazi ya kujilinda dhidi ya mashambulizi haramu ya Urusi...hilo haliondoi operesheni ndani ya Urusi".

    "Tunaweka wazi wakati tunawapa kwamba vifaa vitatumika kulingana na sheria za kimataifa," iliongeza.

    Sir Ben Wallace, waziri wa zamani wa ulinzi wa chama cha Conservative, ameripotiwa kusema hapo awali kwamba silaha zote zinazotolewa na Uingereza, isipokuwa makombora ya masafa marefu ya Storm Shadow, zinaweza kutumika ndani ya Urusi.

    Soma zaidi:

  13. Korea Kaskazini kufunguliwa tena kwa utalii baada ya miaka mitano

    Korea Kaskazini itafungua tena jiji moja kwa watalii wa kigeni mnamo mwezi Desemba baada ya karibu miaka mitano ya kufungwa kwa mipaka kwa sababu ya janga la Covid-19.

    Watu wawili wanaosimamia utalii nchini China wametangaza kuwa hivi karibuni watalii wataruhusiwa kuzuru mji wa kaskazini mwa milima wa Samjiyon.

    Korea Kaskazini iliyojitenga ilijifungia mwanzoni mwa janga hili mapema mwaka 2020 na ilianza kulegeza masharti katikati ya mwaka jana.

    Kufungwa kwa mpaka pia kumesitisha uagizaji wa bidhaa muhimu, na kusababisha uhaba wa chakula ambao ulikuwa mbaya zaidi kwasababu ya vikwazo vya kimataifa vilivyowekwa kutokana na mpango wa nyuklia wa nchi hiyo.

    Soma zaidi:

  14. India: Wanawake waandamana usiku kulalamikia mauaji ya daktari tarajali

    Makumi ya maelfu ya wanawake katika jimbo la West Bengal waliandamana siku ya Jumatano usiku kupinga ubakaji na mauaji ya daktari tarajali katika hospitali ya serikali huko Kolkata wiki iliyopita.

    Maandamano hayo yalikuwa hitimisho la karibu wiki moja ya maandamano ya ghasia yaliyochochewa na mauaji ya kikatili ya kijana huyo mwenye umri wa miaka 31 katika Chuo cha Matibabu cha RG Kar Ijumaa iliyopita.

    Baada ya zamu ya kuchosha ya saa 36, ​​alikuwa amepitiwa na usingizi kwenye chumba cha semina kutokana na ukosefu wa sehemu maalum ya kupumzikia.

    Asubuhi iliyofuata, wenzake waligundua mwili wake ukiwa nusu uchi kwenye jukwaa, ukiwa na majeraha mabaya. Mfanyakazi wa kujitolea wa hospitali amekamatwa kuhusiana na uhalifu huo.

    Wakiitikia wito kutoka kwenye mitandao ya kijamii, wanawake kutoka tabaka mbalimbali waliandamana katika jiji la Kolkata na jimbo lote siku licha ya mvua kunyesha.

    Ingawa maandamano kwa kiasi kikubwa yalikuwa ya amani, yalikumbwa na makabiliano kati ya polisi na kikundi kidogo cha watu wasiojulikana ambao walivamia Hospitali ya RG Kar, eneo kulikotokea mauaji ya daktari huyo, na kupora idara ya dharura.

    Polisi walifyatua vitoa machozi kutawanya umati wa watu waliokuwa wakisababisha ghasia. Baadhi ya magari ya polisi pia yaliharibika.

    Pia unaweza kusoma:

  15. Rais wa zamani wa Argentina ashutumiwa kwa kumdhalilisha mpenzi wake

    Waendesha mashtaka nchini Argentina wameanzisha uchunguzi dhidi ya Rais wa zamani Alberto Fernandez, ambaye anatuhumiwa kumsababishia majeraha mabaya mpenzi wake wa zamani.

    Wiki iliyopita, mke wa rais wa zamani Fabiola Yañez, 43, aliwasilisha malalamiko akimtuhumu kiongozi huyo wa zamani wa miaka 65 kwa kumpiga wakati wa uhusiano wao, ambao ulifika tamati baada ya kuondoka madarakani mnamo mwaka 2023.

    Katika ushuhuda uliotolewa kutoka Uhispania, alielezea jinsi alivyodai kuteswa na vitisho vya kisaikolojia na unyanyasaji wa kimwili alivyopitia, na akamshutumu Bw Fernandez kwa kumlazimisha kutoa mimba.

    Bw Fernandez amekanusha tuhuma zote. Hata hivyo, amepigwa marufuku kuondoka nchini humo wakati uchunguzi ukiendelea.

    Siku ya Jumatano, mwendesha mashtaka Ramiro Gonzales aliwasilisha ombi rasmi mahakamani, akitaka mashtaka yafunguliwe dhidi ya rais huyo wa zamani.

    Uchunguzi huo unafanyika baada ya picha zinazoonekana kumuonyesha Bi Yáñez akiwa na jicho jeusi na michubuko na kuonyeshwa kwenye vyombo vya habari vya ndani, na kusababisha hasira nchini Argentina.

    Bw Fernandez anakataa shutuma dhidi yake na kusema kuwa hazina msingi wowote.

    Chini ya sheria za Argentina, hakimu atatoa uamuzi wa mwisho ikiwa kutakuwa na mashtaka yoyote au la.

    Bw Fernandez alianza kujihusisha na siasa mwanzoni mwa miaka ya 1980, katika siku za mwisho za udikteta wa kijeshi na alihudumu kama rais kati ya 2019-23.

  16. Hamas haitajiunga na mazungumzo ya kusitisha mapigano Gaza - afisa mwandamizi

    Afisa mwandamizi wa Hamas ameiambia BBC kwamba haitashiriki katika mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja kuhusu usitishaji vita wa Gaza na mpango wa kuwaachilia mateka ambao utaanza siku ya Alhamisi huko Doha.

    Kundi hilo lilitaka mpango wenye kutoa mwelekeo wa utekelezaji makubaliano hayo na "halitashiriki mazungumzo kwa ajili ya mazungumzo tu ili kuificha Israeli kuendeleza vita vyake", afisa huyo alisema.

    Alirejelea kuwa mpango huo unapaswa kuzingatia ule uliopendekezwa na kuainishwa na Rais wa Marekani Joe Biden mwishoni mwa mwezi Mei na kuishutumu Israeli kwa kuongeza "masharti mapya".

    Waziri mkuu wa Israeli amekanusha kufanya hivyo na kusema Hamas ndio imekuwa ikidai mabadiliko.

    Mazungumzo hayo bado yanatarajiwa kufanyika hata bila ya Hamas, kwani Marekani, Misri na Qatar ambao ni wapatanishi wanasema wanaweza kuyatumia kupata mpango utakaotatua masuala yaliyosalia.

    Mazungumzo hayo yalikabiliwa na changamoto kadhaa mwezi uliopita na kusimamishwa tangu kuuawa kwa kiongozi wa kisiasa wa Hamas na mpatanishi mkuu, Ismail Haniyeh, mjini Tehran.

    Marekani inatumai kuwa kukamilisha makubaliano kunaweza kuizuia Iran kulipiza kisasi cha mauaji dhidi ya Israeli - ambayo haijathibitisha wala kukanusha kuhusika kwake - na kuepusha mzozo wa kikanda.

    Soma zaidi:

  17. Columbia: Rais wa chuo kikuu ajiuzulu baada ya maandamano kuhusu Gaza

    Rais wa Chuo Kikuu cha Columbia Minouche Shafik amejiuzulu wadhifa wake huku kukiwa na mjadala wa uhuru wa kujieleza kuhusu maandamano ya chuo hicho juu ya vita huko Gaza.

    Kujiuzulu kwa Bi Shafik kunafanyika mwaka mmoja tu baada ya kuchukua wadhifa huo katika chuo kikuu cha kibinafsi cha Ivy League huko New York City, na wiki chache tu kabla ya muhula mpya kuanza.

    Bi Shafik sasa ni rais wa tatu wa chuo kikuu cha Ivy League kujiuzulu kutokana na jinsi alivyoshughulikia maandamano ya vita vya Gaza.

    Mnamo mwezi wa Aprili, Bi Shafik aliidhinisha maafisa wa Idara ya Polisi ya New York kuvamia chuo hicho, uamuzi wenye utata ambao ulisababisha kukamatwa kwa wanafunzi wapatao 100 waliokuwa kwenye jengo la chuo hicho.

    Kipindi hicho kiliashiria mara ya kwanza kwa watu wengi kukamatwa katika chuo kikuu cha Columbia tangu maandamano ya kupinga Vita vya Vietnam zaidi ya miongo mitano iliyopita.

    Hatua hiyo ilichochea maandamano mengine katika vyuo vingi nchini Marekani na Canada.

    Katika barua pepe kwa wanafunzi siku ya Jumatano, Bi Shafik alisema amepitia "kipindi cha machafuko na imekuwa vigumu kukabili maoni tofauti katika jamii yetu"

    "Imekuwa kipindi cha kufadhaisha - kwa jamii, kwangu kama rais na kibinafsi – kujikuta mimi mwenyewe, wafanyikazi wenzangu, na wanafunzi kama vitisho..."

    Hasira ya wanafunzi juu ya jinsi Israeli inavyopigana vita vyake dhidi ya Hamas imeibua maswali makali kwa viongozi wa vyuo vikuu, ambao tayari wanatatizika na mijadala mikali ya vyuo kuhusu kile kinachotokea Mashariki ya Kati.

    Soma zaidi:

  18. WHO yatangaza mlipuko wa Mpox kuwa dharura ya kiafya duniani

    Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza mlipuko wa ugonjwa wa mpox katika baadhi ya maeneo ya Afrika kuwa dharura ya kiafya ya umma.

    Ugonjwa unaoambukiza sana - ambao zamani ulijulikana kama monkeypox - umeua takriban watu 450 wakati wa mlipuko wa awali huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

    Sasa umeenea katika maeneo ya Afrika ya kati na mashariki, na wanasayansi wana wasiwasi kuhusu jinsi aina mpya ya ugonjwa huo inavyoenea na kiwango chake cha juu cha vifo.

    Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus alisema uwezekano wa ugonjwa huo kuenea zaidi ndani ya Afrika na kwingineko "kunatia wasiwasi sana".

    "Kukabiliana na ugonjwa huu kwa namna iliyoratibiwa ni muhimu ili kusitisha janga hili na kuokoa maisha," alisema.

    Mpox huambukizwa kupitia mguso wa karibu, kama vile ngono, mguso wa ngozi hadi ngozi na kuzungumza au kupumua karibu na mtu mwingine.

    Husababisha dalili kama za mafua, vidonda vya ngozi na inaweza kusababisha kifo, na kesi nne kati ya 100 husababisha kifo.

    Kuna aina mbili kuu za mpox - Clade 1 na Clade 2.

    Dharura ya awali ya afya ya umma, iliyotangazwa mwaka wa 2022, ilisababishwa na Clade 2 ambayo si kali. Hata hivyo, wakati huu ni Clade 1 mbaya zaidi - ambayo imeua hadi 10% ya wale wanaougua katika milipuko ya awali – idadi hii inaongezeka.

    Tangu wakati huo, ugonjwa wa mpox umegunduliwa katika nchi nyingine za Afrika - ikiwa ni pamoja na Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Kenya na Rwanda.

    Soma zaidi:

  19. Ukraine yaendelea kusonga mbele ndani ya eneo la Urusi

    Eneo la mpaka wa magharibi mwa Urusi la Kursk lilikumbwa na shambulio la kushtukiza wiki iliyopita, na kusababisha mamlaka ya Urusi kutangaza hali ya hatari katika eneo hilo.

    Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alisema wanajeshi wamesonga mbele kilomita 1-2 zaidi ndani ya eneo la Kursk tangu Jumatano asubuhi, na pia wamewakamata wanajeshi 100 wa Urusi.

    Lakini Urusi inadai kuwa imefanikiwa kusitisha hatua za Ukraine za kusonga mbele zaidi.

    Sasa katika wiki yake ya pili, huu ni uvamizi mkubwa zaidi wa Ukraine ndani ya Urusi tangu Moscow ilipoanzisha uvamizi wake mnamo mwaka 2022.

    Kiasi cha eneo la Urusi lililonyakuliwa hakijulikani, huku nchi zote mbili zikitoa kauli zinazokinzana.

    Kamanda wa kitengo cha kikosi maalum cha Chechen Akhmat, Meja Jenerali Apti Alaudinov aliwaambia watazamaji kwenye Televisheni inayodhibitiwa na serikali ya Urusi, Channel One, kwamba vikosi vya Urusi viko karibu "kuwazuia" wanajeshi wa Ukraine kuendelea kusonga mbele.

    Lakini katika video moja, mkuu wa jeshi Oleksandr Syrskyi alisema wanajeshi wa Ukraine sasa wanadhibiti kikamilifu mji wa mpakani wa Kursk wa Sudzha.

    Hata hivyo, BBC haikuweza kuthibitisha dai hili kwa uhuru, lakini ripoti ya televisheni ya Ukraine iliyorekodiwa kutoka ndani ya mji ilionyesha wanajeshi wa Ukraine wakiondoa bendera ya Urusi kutoka kwenye shuleni moja.

    Huku kukiwa na madai ya Ukraine kupata mafanikio ya kudhibiti maeneo, msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Ukraine Heorhiy Tykhy alisema hawana nia ya "kuchukua" eneo la Urusi. "

    Urusi ikikubali kurejesha amani ya haki haraka iwezekanavyo... ndivyo uvamizi wa vikosi vya ulinzi vya Ukraine nchini Urusi utakavyofikia tamati," aliwaambia waandishi wa habari.

    Katika mkutano wa awali na maafisa wa serikali, Bw Zelensky alisema atafikiria kuanzisha "ofisi za makamanda wa kijeshi" katika eneo hilo.

    Soma zaidi:

  20. Hujambo na karibu katika matangazo yetu mubashara ya tarehe 15/8/2024