Marekani yawaondoa baadhi ya wafanyikazi wake kutoka Beirut huku mvutano ukiongezeka
Kwa mujibu wa afisa mwandamizi wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, wafanyakazi wasio wa lazima wameagizwa kuondoka katika ubalozi wa Marekani ulioko Beirut, mji mkuu wa Lebanon, kufuatia tathmini ya hali ya usalama.
Uamuzi huo umechukuliwa wakati mvutano ukiendelea kuongezeka katika eneo la Mashariki ya Kati, huku Rais wa Marekani, Donald Trump, akitishia kuchukua hatua za kijeshi dhidi ya Iran iwapo hakutakuwa na makubaliano kuhusu mpango wake wa nyuklia.
Iran tayari imetangaza kuwa itajibu endapo Marekani itafanya shambulio, na inaaminika kuwa kambi na vituo vya kijeshi vya Marekani katika Mashariki ya Kati vinaweza kuwa malengo ya mashambulizi.
Wakati huo huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Marco Rubio, ameahirisha ziara yake ya kwenda Israel bila kutoa sababu rasmi.
Afisa huyo mwandamizi wa Wizara ya Mambo ya Nje amesema: “Tunaendelea kutathmini mazingira ya usalama na, kulingana na tathmini yetu ya karibuni, tumeona ni busara kupunguza idadi ya wafanyakazi hadi wale wa lazima pekee. Ubalozi utaendelea kufanya kazi kwa kutumia wafanyakazi muhimu. Hii ni hatua ya muda inayolenga kuhakikisha usalama wa watumishi wetu na kuendelea kuwahudumia raia wa Marekani.”
Takribani wafanyakazi 50 wa ubalozi wa Marekani wameagizwa kuondoka Beirut.
Afisa mmoja wa uwanja wa ndege ameiambia Reuters kuwa wafanyakazi 32 pamoja na familia zao waliondoka kupitia Uwanja wa Ndege wa Beirut siku ya Jumatatu.
Alhamisi, Trump alisema dunia itafahamu “ndani ya siku kumi zijazo au zaidi” iwapo kutakuwa na makubaliano au kama Marekani itachukua hatua ya kijeshi dhidi ya Iran.
Soma pia: