Ghana yataka uchunguzi wa UN baada ya wanajeshi wake kujeruhiwa Lebanon
Ghana imewasilisha rasmi malalamiko kwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, baada ya shambulio kusini mwa Lebanon kuwajeruhi wanajeshi wake wawili wa kulinda amani.
Waziri wa Mambo ya nje wa Ghana, Samuel Okudzeto Ablakwa, amesema serikali inadai uchunguzi kamili, wa haraka, usio na upendeleo na wa wazi kuhusu tukio hilo.
Amesema shambulio hilo linakiuka sheria za kimataifa na linaweza kuchukuliwa kama uhalifu wa kivita.
Wanajeshi hao wa Ghana wako nchini Lebanon kama sehemu ya kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa kinachoitwa United Nations Interim Force in Lebanon (UNIFIL), ambacho kimepelekwa kufuatilia mpaka kati ya Israel na Lebanon.
Kwa mujibu wa Jeshi la Ghana, makao makuu ya kikosi cha Ghana kusini mwa Lebanon yalilengwa na makombora Ijumaa jioni.
Hadi sasa haijulikani ni nani aliyetekelezwa shambulio hilo.
Serikali ya Ghana imelilaani vikali tukio hilo na pia imesisitiza kuwa wale wote waliohusika lazima watambuliwe na kuwajibishwa.
Tukio hili linatokea wakati mvutano unaongezeka sana kwenye mpaka wa Israel na Lebanon. Mapigano yameongezeka kati ya jeshi la Israel na kundi la wanamgambo la Hezbollah linaloungwa mkono na Iran.
Hezbollah imeanza kushambulia kaskazini mwa Israel kwa roketi na ndege zisizo na rubani karibu kila siku, ingawa Israel inasema mashambulizi hayo yanazuiwa na mifumo yake ya ulinzi wa anga.
Wakati huo huo, Israel imetoa amri ya kuwataka watu kuhama katika baadhi ya maeneo ya kusini mwa Lebanon, umbali wa takribani kilomita 27 ndani ya nchi hiyo.
Pia unaweza kusoma: