Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Marekani yasema 'kiwango cha mashambulizi dhidi ya Iran kitaongezeka' huku Israel ikishambulia Beirut na Tehran

Rais Donald Trump amesema kuwa Marekani inashambulia mifumo ya ndege zisizo na rubani na makombora ya Iran "kila saa moja".

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Ambia Hirsi

  1. Air Tanzania kuwarejesha nyumba Watanzania waliokwama Dubai

    Shirika la ndege la Tanzania, Air Tanzania limetangaza mpango wa kuwarejesha nyumbani raia wa nch hiyo walioathiriwa na hatua ya kusitishwa kwa safari za ndege kufuatia mgogoro uliozuka eneo la mashariki ya kati.

    Katika taarifa iliyotolewa leo Ijumaa Machi 6, Air Tanzania imesema ndege hiyo maalum itasafiri kutoka Dar es Salam kuelekea Dubai na kurejea Dar es Salaam siku ya Jumapili.

    Imesisitiza ndege hiyo sio ya kibiashara na kuongeza kwamba itawapatia kipaumbele wasafiri ambao walikuwa wamekata tiketi kabla ya safari kusitishwa.

    Mashirika ya ndege ya kimataifa yamekuwa yakiahirisha safari za kuelekea Mashariki ya Kati tangu Marekani na Israel zilipoanza mashambulizi dhidi ya Iran Jumamosi iliyopita.

    Safari za ndege zinazoingia na kutoka katika viwanja vya ndege vya Tel Aviv, Dubai, Doha na vituo vingine vya kimataifa katika eneo hilo zimesitishwa.

    Ofisi ya Mambo ya Nje ya Uingereza inawashauri raia wa Uingereza dhidi ya safari zote za kwenda Bahrain, Kuwait, Qatar na Falme za Kiarabu (UAE).

    Wale ambao tayari wapo katika maeneo hayo wameshauriwa kuwa makini.

    Iran imefanya mashambulizi katika mataifa ya Ghuba kama sehemu ya kulipiza kisasi mashambulizi ya Marekani na Israel yaliyoanza mapema Jumamosi.

    Usafiri wa mbali umeathiriwa zaidi, huku Heathrow ikiwaomba wasafiri kuthibitisha safari zao na mashirika yao ya ndege.

  2. China na Iran zinajadiliana kuhusu njia salama kwa meli za mafuta- ripoti

    China inajadiliana na Iran kuziruhusu meli zinazosafirisha mafuta ghafi na gesi ya Qatar kupitia mlango wa Bahari wa Hormuz, Reuters imeripoti Alhamisi, ikinukuu vyanzo ambavyo haikutaja

    Mgogoro kati ya Marekani na Israel na Iran ambao sasa umeingia siku ya saba umeathiri mamia ya meli zilizotia nanga karimu na kivuko hicho ambacho ni njia kuu ya usafiri duniani na kusababisha bei ya mafuta kupanda.

    Reuters na Bloomberg zilinukuu data ya kufuatilia meli iliyoonyesha meli ya mafuta inayodai kuwa ya Kichina ilipitia mkondo huo siku ya Alhamisi, ingawa BBC haijaweza kuthibitisha mienendo yake.

    China ni mnunuzi mkubwa wa mafuta ya Iran na imelaani mashambulizi ya Israel na Marekani dhidi ya nchi hiyo.

    Maelezo zaidi:

  3. Marekani na Venezuela yarejesha uhusiano wa kidiplomasia baada ya Maduro kukamatwa

    Marekani na Venezuela zimekubaliana kurejelea tena uhusiano wa kidiplomasia na kibalozi.

    Taarifa zinasema pande hizo mbili zitafanya juhudi za pamoja ili kukuza utulivu, kuunga mkono ufufuaji wa uchumi na kuendeleza maridhiano ya kisiasa.

    Wakati uhusiano wao wa kidiplomasia umekuwa ukiimarika tangu jeshi la Marekani lilipomkamata Rais wa Venezuela Nicolás Maduro mwezi Januari katika shambulio la kushtukiza, kutangazwa kwa uhusiano rasmi wa nchi hizo mbili kunaashiria hatua kubwa.

    Rais Donald Trump aliamuru wanajeshi kumkamata Maduro na mkewe, na kuwafikisha katika mahakama ya Manhattan kujibu mashtaka ya kutumia silaha na dawa za kulevya, madai ambayo wanayakanusha.

    Ubalozi wa Marekani mjini Caracas, uliofungwa mwaka 2019, tayari umefunguliwa tena, na Washington imemteua mwanadiplomasia mpya nchini Venezuela.

    Hapo jana (Alhamisi) serikali ya Venezuela ilisema iko tayari kuendeleza "hatua mpya ya mazungumzo yenye tija, kwa msingi wa kuheshimiana".

    Ilisema uhusiano huo lazima uwe na "manufaa ya kijamii na kiuchumi kwa watu wa Venezuela".

    Marekani imemshutumu Maduro na maafisa wengine wa serikali yake kwa kuongoza shirika la uhalifu linalojihusisha na shughuli kama vile uchimbaji haramu wa madini na ulanguzi wa dawa za kulevya.

    Soma pia:

  4. Ukraine yaishutumu Hungary kwa kuwateka raia wake saba

    Waziri wa Mambo ya Nje wa Ukraine ameishutumu Hungary kwa kuwashikilia mateka wafanyakazi saba wa benki ya serikali ya Ukraine huko Budapest.

    Andrii Sybiha amechapisha kwenye mtandao wa X, kuwa Waukraine hao walikuwa safarini kupitia Hungary kwa gari wakibeba fedha kutoka Austria kwenda Ukraine, wakati walipokamatwa.

    Amesema hadi sasa haijulikani mahali walipo wala sababu za kukamatwa kwao hazijulikani, na kuishutumu Hungary kwa kuiba fedha na ugaidi unaofanywa na serikali.

    Hungary - ambayo ina uhusiano wa karibu na Urusi - bado haijatoa tamko lolote.

    Hapo awali, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alimkosoa Waziri Mkuu wa Hungary Viktor Orban kwa kuzuia msaada wa Ulaya kwa Kyiv.

    Orban ameishutumu Kyiv kwa kuweka "kizuizi cha mafuta" kwa Hungary na kuchelewesha makusudi kufunguliwa tena kwa bomba la Druzhba.

    Maelezo zaidi:

  5. Hezbollah yawataka raia wa Israel kuondoka karibu na mpaka wa Lebanon

    Kundi la Hezbollah linaloungwa mkono na Iran linawataka raia wa Israel wanaoishi miji iliyo umbali wa kilomita 5 kutoka mpaka wa Lebanon kuondoka.

    Onyo hilo limewekwa katika ujumbe kwenye chaneli yake ya Telegraph kwa Kiebrania mapema Ijumaa, kulingana na shisrika la habari la Reuters.

    "Uvamizi wako wa kijeshi dhidi ya mamlaka ya Lebanon na raia wake, uharibifu wa miundombinu ya kiraia na kampeni ya kuwafukuza raia hautapita bila kupingwa," Hezbollah ilisema.

    Jeshi la Ulinzi la Israel, IDF, lilianza wimbi la mashambulizi dhidhi ya Lebanon ya Alhamisi jioni, baada ya kuwaambia watu waondoke maeneo ya kusini mwa mji mkuu wa Beirut, ambayo ni ngome ya Hezbollah.

    Muda mfupi uliopita, IDF pia ilisema imeanza "wimbi kubwa la mashambulizi dhidi ya miundombinu ya utawala wa kigaidi wa Iran mjini Tehran".

    Maelezo zaidi:

  6. Marekani yazamisha zaidi ya meli 30 za kivita za Iran

    Kamanda wa Kamandi Kuu ya Marekani, Admiral Brad Cooper, anasema kuwa Marekani imezamisha zaidi ya meli 30 za Iran kufikia sasa.

    Aliongeza, "Katika saa chache tu zilizopita, tuliishambulia meli ya kubeba ndege zisizo na rubani ya Iran ambayo ukubwa wake ni sawa na ile iliyobeba ndege za kivita wakati wa Vita vya Pili vya Dunia. Sasa inawaka moto."

    Cooper amesema kuwa Marekani imeshambulia kwa mabomu takriban maeneo 200 nchini Iran katika muda wa saa 72 zilizopita.

    Huku hayo yakijiri afisa wa Ikulu ya White House ameithibitishia BBC kwamba maafisa wa utawala wa Trump wanapanga kukutana na wasimamizi wa ulinzi wa Marekani leo Ijumaa, kujadili utengenezaji wa silaha.

    Mkutano huo utafanyika katika Ikulu ya White House na utahudhuriwa na kampuni kama vile Lockheed Martin & RTX, kampuni mama ya Raytheon, shirika la habari la Reuters liliripoti hapo awali.

    Majadiliano yanatarajiwa kujumuisha kuongeza kasi ya utengenezaji wa silaha, huku Pentagon ikiwa mbioni kujaza tena hifadhi yake silaha ya baada ya shambulio dhidi ya Iran kulingana na Reuters.

    Katika mkutano na waandishi wa habari muda mfupi uliopita, Waziri wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth alisema Marekani ina silaha nyingi na inaweza kuendeleza operesheni yake dhidi ya Iran hadi itakapofikia lengo lake.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Marekani yasema 'kiwango cha mashambulizi dhidi ya Iran kitaongezeka' huku Israel ikishambulia Beirut na Tehran

    Rais wa wa Marekani Donald Trump na Waziri wake wa Ulinzi wa Marekani Pete Hegseth wameikosoa hatua ya Uingereza kwa kukataa vituo vyake vya kijeshi katika eneo la Mashariki ya Kati kutumiwa kuishambulia Iran.

    Trump hapo awali aliangazia kile kinachoendelea nchini Iran katika hafla iliyofanyika Ikulu ya White House.

    Kwa upande wake Hegseth alisema kwa "bahati mbaya "Uingereza ilikataa ombi letu "kutoka siku ya kwanza".

    "Lakini tulifikia lengo letu. Tulifika huko, na hiyo sasa ni sehemu ya mpango ambao tunatumia kufanya mashambulizi ya angani...Ni vikosi zaidi vya wapiganaji, ni uwezo zaidi, ni uwezo wa kujilinda zaidi, na ni mashasmbulizi ya mara kwa mara," alisema.

    "Kiwango mashabulizi dhidi ya Iran na Tehran kinakaribia kuongezeka kwa kasi," alisema.

    Hegseth pia alisema Marekani na Israel zinawalenga wale waliokuwa wakiwakandamiza waandamanaji nchini Iran.

    "Kadiri unavyofanya hivyo zaidi, kuharibu nia na uwezo wao, ndivyo unavyotengeneza fursa kwa watu kusimama kwa ujasiri," Hegseth alisema.

    Melezo zaidi:

  8. Hujambo na karibu kwa matangazo ya moja kwa moja. Leo Ijumaa 06/03/2026