Vita vya Afghanistan: Kabul yaangukia kwenye himaya ya Taliban huku rais wa nchi hiyo akikimbia

Chanzo cha picha, EPA
Taliban imetangaza ushindi nchini Afghanistan baada ya kuteka mji mkuu Kabul, na kutamatisha karibu miaka 20 uwepo wa Marekani na washirika wake nchini humo
Wapiganaji wamechukua ikulu ya rais. Serikali imeanguka, huku Rais Ashraf Ghani akikimbia.
Msemaji wa kikundi hicho ameuambia mtandao wa habari wa Al Jazeera: "Vita vimekwisha."
Kabul imeingia kwenye machafuko, na wakazi na raia wa kigeni wamekuwa wakijaribu kutoroka.
Katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa mji mkuu, shuhuda aliiambia BBC kwamba wafanyakazi wameacha madawati yao na watu wanakimbilia ndege.
Kabul ulikuwa mji mkuu wa mwisho nchini Afghanistan kudhibitiwa na Taliban, kasi ya udhibiti wa miji ukiwashtua waagalizi wengi.

Wanamgambo hao waliweza kuchukua udhibiti baada ya wanajeshi wengi wa kigeni kuondoka nchini humo.
Rais wa Marekani Joe Biden ametetea kujiondoa kwa wanajeshi wa Marekani, akisema kuwa hakuweza kuhalalisha "uwepo wa Marekani usio na mwisho katikati ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vya nchi nyingine".
Zaidi ya nchi 60, pamoja na Marekani na Uingereza, zimetoa taarifa ya pamoja ikisema watu wa Afghanistan "wanastahili kuishi kwa usalama na utu", na kwamba usalama na utawala wa kiraia unapaswa kurejeshwa mara moja.
Pia walitoa wito kwa Taliban kumruhusu mtu yeyote anayetaka kuondoka kufanya hivyo, na kuweka barabara, viwanja vya ndege na vivuko vya mipaka wazi.
'Watu wanakimbia na kujificha'
Taliban waliamuru wapiganaji wao kuingia Kabul Jumapili, baada ya kuwazuia mapema nje kidogo ya jiji.
Walisema walikuwa wakienda kuzuia machafuko na uporaji baada ya vikosi vya usalama kuacha sehemu za mji mkuu.
Picha zilizotangazwa na mtandao wa televisheni Al Jazeera zilionesha wapiganaji ndani ya ikulu ya rais, wakipiga bunduki.
Mkala hii imebeba madhui yaliyotoka kwenye mitandao ya kijamii. Tunaomba ruhusa yako kabla kitu chochote hakija pakiwa, sababu wanaweza wakawa wanatumia Cookies na tekinolojia nyingine. Unaweza ukasoma sera sera ya kutumia cookies katika mitandao ya kijamii kabla ya kukubali. Kutazama maudhui haya chagua accept and continue
Mwisho wa X ujumbe

Kuingia kwa Taliban mjini Kabul kulikuja baada ya Rais Ghani kukimbia. Maelezo ya mahali alipo hayajathibitishwa lakini Al Jazeera, ikimtaja mfanyakazi wake, akisema alikuwa amesafiri kwenda Tashkent katika nchi jirani ya Uzbekistan.
Katika chapisho lake kwenye mtandao wa Facebook lililoelekezwa kwa raia wa Afghanistan, Bwana Ghani alisema alifanya uamuzi mgumu kuondoka ili kuepuka umwagaji damu katika mji mkuu.
"Taliban ilishinda ushindi kwa njia ya upanga na bunduki na wana jukumu la kulinda heshima, ustawi na heshima ya wenzetu," alisema.
Rais alikosolewa na wanasiasa wengine kwa kuondoka.
"Mungu atamwajibisha na taifa pia litahukumu," alisema Abdullah Abdullah, mwenyekiti wa Baraza Kuu la Upatanishi wa Kitaifa la Afghanistan.

Chanzo cha picha, Anadolu Agency via Getty Images
Kulikuwa na hofu huko Kabul wakati Taliban walipokaribia ushindi. Wakazi walielekea uwanja wa ndege, wakiacha magari na kusafiri kwa miguu kwa nia ya kutaka kutoka nje ya nchi.
Mwanafunzi mmoja wa miaka 22 aliiambia BBC kwamba alikuwa ametembea kwa zaidi ya saa tano.
"Miguu yangu inauma, ina malengelenge na napata shida kusimama," alisema.
"Sasa kwa kuwa ninaondoka, ninafikiria juu ya familia yangu - hawana njia yoyote ya kutoroka. Sioni mustakabali wetu."

Chanzo cha picha, AFP
Ubalozi wa Marekani ulisema kulikuwa na ripoti za ufyatuaji risasi katika uwanja wa ndege wa Kabul, na kuonya raia wake kujilinda kwani "hali ya usalama ... inabadilika haraka".
Katikati mwa jiji, foleni kubwa zilikuwepo kwenye benki siku nzima wakati watu walipotaka kutoa pesa.
Mbunge wa eneo hilo Farzana Kocha aliambia BBC kuwa watu hawajui la kufanya, wengine wakikimbia au kujificha ndani ya nyumba.
Kulikuwa na ripoti za mapigano na majeruhi katika wilaya ya mji huo Qarabagh.
Msemaji wa Taliban Suhail Shaheen aliiambia BBC kuwa watu huko Kabul hawana haja ya kuwa na wasiwasi na kwamba mali na maisha yao ni salama.
"Sisi ni watumishi wa watu na wa nchi hii," alisema.
Kuwaondoa raia
Marekani imepeleka maelfu ya wanajeshi kusaidia kuondoa wafanyakazi wake na Waafghan ambao walisaidia katika ujumbe wake. Helikopta zinazosafirisha wafanyakazi wa ubalozi ziliweza kusikika juu ya jiji siku ya Jumapili, na kulikuwa na ripoti za moshi unaopanda karibu na eneo la ubalozi wakati nyaraka muhimu zikiharibiwa.
Karibu wanajeshi 600 wa Uingereza wametumwa kusaidia operesheni yao ya kujiondoa.
Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson alisema kipaumbele chake ni kusaidia raia wa Uingereza na "wale wote ambao wamesaidia juhudi za Uingereza zaidi ya miaka 20" kutoka Afghanistan "haraka iwezekanavyo".
Alitoa wito kwa nguvu "zenye nia moja" kufanya kazi pamoja na kutotambua serikali yoyote mpya bila makubaliano.
Nchi nyingine pia zinawahamisha raia wao, na kupunguza uwepo wao nchini Afghanistan na wakati mwingine hufunga balozi zao kabisa.
Urusi imepanga kuitisha mkutano wa dharura wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ili kujadili hali ya Afghanistan.
Imesema kuwa haitafunga ubalozi wake kwa sababu imepewa hakikisho la usalama na Taliban.












