Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Mbuga ya Maasai Mara: Ndege yaanguka baada ya kugonga nyumbu wawili Kenya
Kulikuwa na hali ya hofu baada ya ndege ya kampuni ya Fly Safarilink nchini Kenya kugonga nyumbu wawili ilipokuwa ikitua katika uwanja wa ndege wa Kichwa Tembo Airstrip katika mbuga ya wanayama pori ya Maasai Mara.
Ndege hiyo nyepesi kwa jina Dash 8 iliopatiwa nambari za usajili 5Y- SLM ilihusika katika kisa hicho baada ya nyumbu hao kupita ghafla katika barabara ya ndege wakati ndege hiyo ilipokuwa ikitua .
''Tunashukuru kuthibitisha kwamba abiria wote na wafanyakazi walioabiri wako salama na kwamba hakuna majeraha ama hata watu kufariki'', ilisema taarifa hiyo iliotolewa na kampuni hiyo ya ndege.
Nyumbu wawili waliogongwa na ndege hiyo walifariki.
Afisa wa Utalii wa Mara Triangle David Top alisema kwamba matairi ya ndege hiyo yalitoka na kuifanya kukosa mwelekeo kabla ya kutoka katika barabara yake.
''Ilikuwa mwendo wa saa 10.30 alfajiri wakati ndege hiyo ilipopata matatizo ya kiufundi na kuwagonga nyumbu wawili'', afisa huyo alinukuliwa na gazeti la The Standard akisema.
Ijapokuwa hakuna uwanja wa ndege katika mbuga ya wanyama pori ya Mara, kuna viwanja kadhaa vidogo vidogo vya kutua ndege katika mazingira yake ambapo ndege za abiria huwaweka na kuwachukua abiria kabla ya kurudi Nairobi.
Kampuni ya ndege ya Safarilink husafirisha abiria katika viwanja tofauti vya ndege ndogo ndogo kama vile Keekorok, Mara kaskazini, Musiara, Serena, Angama, Olkiombo na Kichwa Tembo.
Wakati wa msimu mzuri wa Utalii , wanyama hao hutembea kila mahali katika mbuga hiyo ya wanyama pori , wakitafuta lishe karibu na barabara hiyo ya ndege.
Usimamizi wa kampuni hiyo ulisema kwamba ndege hiyo imeharibika na kwamba wahandisi wake pamoja na wafanya kazi wamepelekwa katika eneo la tukio ili kutazama hali ilivyo.
Wakati ilipokuwa ikitua takriban magari 10 yalikuwa yameegeshwa katika eneo hilo huku madareva pamoja na viongozi wa safari wakisubiri kuwabeba abiria na kuwapeleka katika hoteli na kambi za mahema.