Avgdor Lieberman: apinga kusitishwa mapigano Israel, ajiuzulu

Waziri wa Ulinzi wa Israel Avgdor Lieberman

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Waziri wa Ulinzi wa Israel Avgdor Lieberman

Waziri wa Ulinzi wa Israel amejiuzulu kufuatia uamuzi wa Baraza la Mawazi la nchi yake kukubali kusitishwa mapigano yaliyodumu kwa siku mbili na wapiganaji wa Palestina ukanda wa Gaza.

Avgdor Lieberman ameishutumu hatua hiyo na kuiita kama ni kusalimu amri kwa ugaidi.

Amesema chama chake cha Mrengo wa kulia cha Yisrael Beiteinu kinaweza kujitoa katika serikali ya mseto, hali ambayo inaweza kusababisha uchaguzi wa mapema.

Watu wanane waliuawa siku ya Jumatatu na Jumanne baada ya wapiganaji walipofyatua roketi 460 kuelekea upande wa Israel na Majeshi ya Isreal nayo yakishambulia kwa mabomu Gaza.

Usimamishaji wa mapigano kwa kiasi kikubwa ulifanyika siku ya jumatano, huku shule na shughuli za kibiashara kusini mwa Israel zikifunguliwa tena, baada ya kutoripotiwa mashambulizi ya roketi usiku mzima.

Uharibifu baada ya mashambulio yaliyofanywa na Israel

Chanzo cha picha, AFP

Maelezo ya picha, Uharibifu baada ya mashambulio yaliyofanywa na Israel

Hata hivyo wanajeshi wa Israel wamesema wamempiga risasi na kumkamata Mpalestina mmoja ambaye alikuwa akijaribu kuvunja waya ambao ni mpaka kati ya Israel na Gaza, wakati akitaka kurusha mlipuko.

Maafisa wa afya wa Kipalestina wameripoti pia kuuawa kwa mvuvi mmoja, baada ya kushambuliwa na Israel kaskazini mwa Gaza. Wanajeshi wa Israel wanasema wamemshambulia kwa sababu alikuwa akielekea kwenye waya ulioko mpakani.