Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Trump aionya Iran 'isiijaribu Marekani', ajibizana na Hassan Rouhani
Rais wa Marekani Donald Trump na mwenzake wa Iran Hassan Rouhani wamejibizana vikali na kutoa vitisho huku uhasama baina ya mataifa hayo mawili ukizidi.
Bw Trump ameandika kwenye Twitter, kwa herufi kubwa, kwamba "Iran itapata madhara ambayo ni wachache sana wamewahi kukumbana nayo katika historia" iwapo itaitishia Marekani.
Bw Rouhani awali alikuwa amesema kwmaba vita na Iran vitakuwa "vita zaidi ya vita vingine vyote".
Mwezi Mei, Marekani ilijitoa kutoka kwa mkataba wa nyuklia na Iran ambao ulikuwa umehusisha Iran kusitisa shughuli zake za nyuklia ili iondolewe vikwazo vya kimataifa.
Marekani sasa imeanza kuiwekea tena Iran vikwazo licha ya pingamizi kutoka kwa Uingereza, Ufaransa, China, Urusi na Ujerumani wote ambao walikuwa wadau katika mkataba huo wa mwaka 2015.
Katika tukio tofauti Jumapili, waziri wa mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo alisema utawala wa Iran "unafanana zaidi na mafia badala ya serikali".
Alikuwa aihutubia kundi la Wamarekani wa asili ya Iran jimbo la California.
Aliwashutumu vikali Bw Rouhani na waziri wa mambo ya nje wa Iran Javad Zarif ambao walifanikisha mkataba huo wa nyuklia na kuwaeleza kama "mawakala walioandaliwa vyema wa kuwawakilisha na kufanikisha utapeli wa ma-ayatollah (viongozi wakuu wa kidini wa Iran".
Bw Pompeo alisema anataka kuzuia mataifa kununua mafuta ya iran kufikia Novemba kama sehemu ya kuiongezea shinikizo Iran.
Kwa nini Marekani ikajiondoa?
Rais Donald Trump alitangaza kujitoa katika mkataba wa kimataifa wa nyuklia wa Iran mwezi Mei na kuuita mpango uliooza na kero kwa raia wote wa Marekani.
Alisema mpango huo unaifaidi tu na kuiongeza nguvu Iran.
Alisema mpango huo hauwezi kuleta amani hata kama Iran ikikubaliana na kila kitu kama sehemu ya utekelezaji wa mpango huo uliosainiwa mwaka 2015 chini ya utawala wa aliyekuwa rais taifa hilo Barack Obama.
Israel na Saudi Arabia kwa pamoja walimpongeza Trump kwa hatua hiyo.
Trump awali alilalamikia mkataba huo kwamba ulikuwa unaiwekea Iran vikwazo kwa muda tu na kwamba ilishindwa kusitisha mpango wake wa makombora na kwamba Iran ilipewa kiasi cha dola bilioni 100 kwa ajili ya kutokomeza silaha na ugaidi huko mashariki mwa kati.