Wanaharakati waandamana Kenya kushinikiza kufunguliwa kwa vituo vya utangazaji

Wanaharakati na waandishi habari wamiminika mjini Nairobi kushinikiza kufunguliwa kwa vituo vya utangazaji vilivyofungwa
Maelezo ya picha, Wanaharakati na waandishi habari wamiminika mjini Nairobi kushinikiza kufunguliwa kwa vituo vya utangazaji vilivyofungwa

Maandamano makubwa yatarajiwa hii leo Nairobi kuishinikiza serikali kuvifungua vyombo vitatu vya habari nchini vilivyofungiwa kupeperusha matangazo kwa siku ya saba leo.

Maandamano haya yanajiri wakati viongozi wa upinzani waliokamatwa kwa madai ya kushiriki njama ya kumuapisha kiongozi wa upinzani Raila Odinga kama rais.

Serikali ilizifunga stesheni tatu za televisheni NTV, Citizen na KTN kwa madai kuwa vilipanga kupeperusha moja kwa moja matangazo licha ya onyo kutofanya hivo.

Na sasa makundi ya kutetea haki za kibinadamu, waandishi habari na baadhi ya wananchi wanapanga kufanya maadamano hii leo Nairobi kuishinikiza serikali kutii amri ya mahakama.

Studio ya TV haina watu

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, NTV, Citizen na KTN zilifungwa kwa madai kuwa vilipanga kupeperusha matangazo ya moja kwa moja ya kuapishwa kwa Raila Odinga

Waandalizi wa maandamano hayo wanaishtumu serikali wakidai imekiuka haki za kibinadamu, kuendeleza mashambulizi dhidi ya vyombo vya habari kando na kupunguza uhuru wa demokrasia nchini kwa kutoheshimu katiba.

Kufutia kuapishwa kwa Odinga Jummanne iliyopita, vyomba vya usalama vime wakamata viongozi wa upinzani inaodai walishiriki katika kumuapisha Odinga kuwa anachokitaja Rais wa watu.

Viongozi watatu wa muunganow a upinzani NASA, wabunge TJ Kajwang na Geroge Aladwa pamoja na wakili Miguna Miguna walikamatwa.

Raila Odinga akila kiapo cha kuwa rais wa wananchi wa Kenya

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Raila Odinga akila kiapo cha kuwa rais wa wananchi wa Kenya

Wote waliachiliwa kwa dhamana ili Miguna anasalia kizimbani licha ya mahakama kuu kuamrisha aachiliwe na anatarajiwa kufikishwa tena mahakamani Leo.

Katika mkutano wa hadhara jijini Nairobi siku ya Jumapili viongozi wa upinzani wameapa kufanya maandamano iwapo Miguna hataachiliwa huru

'Ikifikia kesho kama Miguna Miguna hajaachiliwa.. Wale watu wote tulikuwa Uhuru Park, tutajitokeza twende police station.. tuwe tayari kushikwa', amesema Godfrey Otsosi kiongozi wa chama cha ANC katika muungano wa upinzani Nasa Kenya.

Lakini kwa upande wake, serikali imeshikilia kuwa upinzani unakiuka sheria na hauheshimu uamuzi wa wanachi uliowaweka madarakani.

Makamu wa Rais,William Ruto amesisitiza kuwa hawatafanya mazungumzo na upinzani kuhusu kugawana mamlaka serikali.

William Ruto na Uhuru Kenyatta

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Rais Uhuru Kenyatta na makamu wake William Ruto

'Wametuambia ya kwamba ni vizuri tuongee. Mimi nawaambia tuko tayari kuongea vile mamilioni ya vijana wa kenya watapata kazi, tuko tayari. Vile tutazalisha chakula cha kutosha tuondoe aibu ya njaa, lakini kama munataka tuongee ati nani atakuwa rais, sijui nani atakuwa makamu ya rais......hiyo we are not qualified...watu wanaopanga maneno hayo ni wananchi wa Kenya. Hao ndio wanaamua', amesema makamu wa rais William Ruto.

Stesheni hizo tatu za televisheni nchini NTV Kenya, KTN na Citizen TV zinasalia kwenye giza bila ya kujua hatma yao licha ya mahakama kuu kuamuru zifunguliwe kufuatia kesi iliyowasilishwa mahakamani na mwanaharakati Okiya Omtatah.