Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Tanzania yapanga kuitisha fidia kutoka Ujerumani
Waziri wa ulinzi nchini Tanzania Hussein Mwinyi, ameiambia redio ya Ujerumani ya Deutsche Welle, kuwa ana mipango ya kuishinikiza serikali ya Ujerumani kulipia dhuluma zilizofanyika wakati wa utawala wa ukoloni.
Bwana Mwinyi alisema kuwa serikali itaomba fidia kwa niaba ya maelfu ya watu, ambao waliteswa na kuuawa na wanajeshi wa Ujerumani wakati walijaribu kuzima uasi kati ya mwaka 1905 na 1907.
Ujerumani iliitawala Tanzania ambayo wakati huo ilikuwa ikijulikana kama Tanganyika kutoka mwaka 1890 hadi mwaka 1919.
"Fidia ndiyo tunatafuta na kuna mfano wa nchi barani Afrika ambazo zimeomba fidia hii. Kenya kwa mfano imeomba fidia kutoka Uingereza na Namibia. Kwa hivyo tuna tumaini ya kupeleka suala hili kwa serikali ya Ujerumani sisi wenyewe," alisema bwana Mwinyi.
Alipoulizwa kuhusu ni nani atafaidika na fidia hiyo, alisema kuwa lengo ni kuwafidia wale waliopoteza maisha na pia kuna wale waathiriwa ambao bado wako hai. Lakini kwa wale waliopoteza maisha, wana watu ambao watanufaika.