Eneo ilipodondoka ndege ya Indonesia lagundulika

Chanzo cha picha, Reuters
Mamlaka ya Indonesia imesema kuwa imebaini eneo ambalo wanaamini kuwa ndege ya abiria aina ya Boeing 737 iliangukia mara tu baada ya kupaa kutoka katika uwanja wa ndege wa Jakarta, siku ya Jumamosi.
Ndege hiyo iliyokuwa imebeba abiria 62, ilipoteza mawasiliano na rada dakika nne tu baada ya kuanza safari yake ya kuelekea eneo la Pontianak magharibi mwa jimbo la Kalimantan.
Jumapili hii, kulikuwa na ishara kutoka kwa rekoda ya ndege hiyo na ndio inafuatiliwa.
Zaidi ya meli 10 zikiwa na wataalamu wa kupiga mbizi, zinafuatilia eneo ambalo ndege hiyo ilianguka
"Kuna maeneo mawili ambayo tunadhania kisanduku jeusi la ndege kinaweza kuepo ," mkuu wa kikosi cha uokozi bwana Bagus Puruhito,alisema.

Chanzo cha picha, EPA
Watafiti pia wanachunguza baadhi ya vitu ambavyo vinaaminika kuwa vilitoka katika ndege hiyo.
Msemaji wa polisi wa eneo la Jakarta, Yusri Yunus,alisema wamepokea mabegi mawili kutoka kikosi cha uokozi.
"Begi la kwanza lilikuwa na bidhaa za abiria, na begi lingine lilikuwa na sehemu za mwili wa binadamu,"aliongeza kuwaambia waandishi: "Bado tunachunguza zaidi matokeo ya kile tulichopata"

Chanzo cha picha, EPA
Bado ndege hiyo inaendelea kutafutwa , na ndege nyingine nne zimetolewa ili kusaidia kutafuta ndege iliyopotea.

Chanzo cha picha, Reuters
Nini kilitokea katika ndege hiyo?
Ndege hiyo ya kampuni ya Sriwijaya Air aina ya Boeing 737 imepoteza mawasiliano ilipokuwa inaelekea Pontianak magharibi mwa eneo la Kalimantan, maafisa wamesema.
Mtandao unaofuatilia safari za ndege Flightradar24.com umesema ndege hiyo ilipoteza mawasiliano baada ya kupaa mita 3,000 ndani ya dakika moja.
Aliyeshuhudia ajali hiyo amesema aliona na kusikia mlipuko mkubwa.
Solihin ambaye ni mvuvi, amezungumza na BBC Indonesia na kuthibitisha ameshuhudia ajali hiyo na rubani wa ndege hiyo akaamua kurejea kwenye aneo la ardhini.

Chanzo cha picha, GM Fikri Izzudin Noor
"Ndege hiyo imeanguka kama radi ndani ya bahari na kulipuka ndani ya maji," amesema.
"Ilikuwa karibu sana na sisi na vipande vya mfano wa mbao nyepesi karibu vipige meli yangu."
Pia picha za kile kinachoonesha kama vifusi vinaonekana kwenye televisheni na mitandao ya kijamii.
Wizara ya usafirishaji imesema shughuli za utafutaji na uokozi wa ndege hiyo zinaendelea.
Wizara hiyo imesema mawasiliano ya mwisho na ndege hiyo yalifanyika 14:40 saa za eneo.
Kulingana na taarifa za usajili, ndege hiyo aina ya Boeing 737-500 imetumika kwa miaka 27.

Chanzo cha picha, Mulyono/Naki













