Fury asitishwa kupigana na bodi ya ndondi Uingereza

Tyson Fury

Chanzo cha picha, Getty Images

Wakuu wa ndondi wamesitisha kibali cha Tyson Fury kupigana siku moja baada ya mwanabondia huyo kusalimisha mataji yake ya ubingwa wa ndondi uzani mzito duniani ili kuweza kukabiliana na matatizo ya afya ya akili.

Fury, mwenye umri wa miaka 28, hajapigana tangu kumshinda Wladimir Klitschko mnamo Novemba 2015 na amesusia mechi mbili za za marudio.

Bodi ya udhibiti wa mchezo wa ndondi Uingereza - British Boxing Board of Control - imethibitisha kuwa kibali chake kimesitishwa kwa muda "ikisubiriwa uchunguzi wa ziasa dhidi ya tuhuma za utumiaji madawa ya kusisimua misuli na masuala ya afya".

Fury alishtakiwa kwa makosa ya kutumia dawa za kusisimuwa misuli na taasisi ya Uingireza ya kupambana na madawa hayo mnamo mwezi Juni.

Jumatano Fury alisalimisha mataji yake ya ubingwa wa ndondi uzani mzito WBO na WBA, akieleza kuwa hawezi kuyatetea mataji hayo kutokana na afya yake.

Tyson Fury alimshinda Wladimir Klitschko mnamo Novemba 2015
Maelezo ya picha, Tyson Fury alimshinda Wladimir Klitschko mnamo Novemba 2015

Inambidi sasa akutane na bodi hiyo ya ndondi Uingereza kabla ya kufikiwa uamuzi kuhusu iwapo atapigana tena au la.

Rufaa aliokata katika kesi ya utumiaji wa dawa za kusisimua misuli inataajiwa kusikilizwa Novemba.

Mapema mwezi huu, Fury alionekana kutangaza kustaafu kwake katika mtandao wa Twitter, kabla ya kujitokeza saa chache baadaye kukiuka kauli hiyo , na kufichua katika mahojiano na jarida la Rolling Stone kwamba anatumia mihadarati kumsaidia kukabiliana na msongo wa mawazo.