Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Ukraine yathibitisha kuwa Urusi imeuteka mji wa mashariki wa Lysychansk

Mkuu wa majeshi yake alisema kwamba "ili kulinda maisha ya watetezi wa Ukraine, uamuzi ulifanywa wa kujiondoa".

Moja kwa moja

  1. Nguvu haiwezi kutatua mgogoro wa Rwanda na Congo - Kagame,

    Rais wa Rwanda, Paul Kagame, ametoa wito wa kutatuliwa kwa mgogoro wa kisiasa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

    Katika mahojiano na shirika la utangazaji la serikali, alisema uhasama uliopo hauwezi kutatuliwa kwa nguvu pekee.

    Wiki mbili zilizopita viongozi wa Afrika Mashariki waliidhinisha kuundwa kwa kikosi cha kijeshi cha kanda katika eneo lenye machafuko, huku kukiwa na kuzuka upya kwa shughuli za waasi na kuzidisha mvutano kati ya DR Congo na Rwanda.

    Kigali inaishutumu serikali ya Congo kwa kulivamia eneo lake.

    Kinshasa inaishutumu Rwanda kwa kuwaunga mkono waasi wa M23. Kuhusu mpango wa wahamiaji na Uingereza, Rais Kagame alisema nchi hiyo ina nafasi kwa Wanyarwanda pamoja na mataifa mengine.

    Soma zaidi

    • Kutupeleka Rwanda haukutuzuia kufika Ulaya
    • 'Mpango wa Uingereza wa kuwapeleka wahamiaji Rwanda 'ni kinyume cha Mungu' - Welby
    • Jumuiya ya Afrika Mashariki, majeshi na mustakabali wa amani DRC
  2. Uturuki yaishikilia meli kwa madai ya wizi wa nafaka ya Ukraine - ripoti

    Maafisa wa Uturuki wameizuia meli ya mizigo yenye bendera ya Urusi karibu na pwani ya Bahari Nyeusi, ambayo Ukraine inadai inabeba nafaka zilizoibwa, kwa mujibu wa Reuters.

    "Meli iliyopewa jina Zhibek Zholy ilisimamishwa nje ya [bandari ya] Karasu," shirika la habari lilimnukuu afisa mkuu wa Uturuki akisema siku ya Jumatatu.

    Tuhuma za kuibiwa nafaka za Ukraine "zinachunguzwa kwa kina", afisa huyo alisema, huku Urusi, Umoja wa Mataifa na pande tatu zikishiriki katika mazungumzo.

    Afisa katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Ukraine, akinukuu utawala wa baharini wa taifa hilo, aliIambia Reuters kuwa meli hiyo ilikuwa imebeba shehena ya kwanza ya tani 4,500 za nafaka kutoka Berdyansk, bandari inayokaliwa na Urusi kusini mwa Ukraine.

    Uamuzi kuhusu shehena hiyo utatolewa kufuatia mkutano wa wachunguzi siku ya Jumatatu, alisema Vasyl Bodnar, balozi wa Ukraine nchini Uturuki, kwenye televisheni ya taifa - akiongeza kuwa Ukraine ilikuwa na matumaini ya kunyang'anywa nafaka hiyo.

    Kyiv imeishutumu Moscow kwa kuiba nafaka kutoka maeneo kadhaa yaliyotekwa na majeshi ya Urusi tangu uvamizi huo uanze mwezi Februari. Kremlin hapo awali ilikanusha kuiba nafaka za Ukraine.

    • Urusi na Ukraine: Je ulimwengu unaipatia Ukraine silaha za aina gani?
    • Urusi na Ukraine: Nato ni nini na inabadilikaje?
  3. Wakamatwa uwanja wa ndege wakiwa wameficha heroine kwenye chakula cha watoto

    Dawa za kulevya aina ya heroine zilizofichwa ndani ya pakiti za vyakula vya watoto imenaswa katika uwanja wa ndege mkuu wa Lagos, kwa mujibu wa polisi.

    Washukiwa watatu wamekamatwa kuhusiana na kusafirisha kilo 23 za dawa hiyo kwenye Shirika la Ndege la Afrika Kusini kutoka Johannesburg, alisema msemaji wa Shirika la Kitaifa la Kupambana na Dawa za Kulevya Femi Babafemi siku ya Jumapili.

    Katika tukio tofauti, shirika la kupambana na dawa za kulevya lilisema dereva wa usafiri wa umma alikamatwa katika uwanja huo huo wa ndege kwa tuhuma za "kumeza kete 90 za cocaine" kabla ya kujaribu kupanda ndege kuelekea Dubai.

    Maafisa nchini Nigeria mara nyingi wameelezea kuenea kwa matumizi ya dawa za kulevya nchini humo kuwa ni jambo la kutisha na janga.

    Pia ni sehemu ya kupitisha dawa mbalimbali haramu.

  4. Mlipuko wa Ebola wamalizika rasmi nchini DR Congo

    Mlipuko wa hivi punde wa Ebola umedhibitiwa ndani ya miezi mitatu kutokana na "mwitikio wa haraka" na "madhubuti" katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, linasema Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO).

    Watu wanne wamefariki tangu mlipuko huo wa 14 nchini humo tangu 1976 kutangazwa mwezi Aprili katika mji wa magharibi wa Mbandaka.

    Watatu kati ya waliokufa walichukuliwa kuwa "kesi zilizothibitishwa" na mmoja alichukuliwa kuwa kesi shirika la afya ulimwenguni lilisema.

    Shirika la Umoja wa Mataifa lilifanya kazi pamoja na serikali kusambaza chanjo, upimaji, ufuatiliaji,kuzuia na kudhibiti maambukizi, pamoja na ushirikishwaji wa jamii.

    "Matokeo haya yanaonyesha kuimarisha utayari, ufuatiliaji wa magonjwa na ugunduzi wa haraka, kupiga hatua mbele," Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika Dk Matshidiso Moeti alisema katika taarifa yake Jumatatu.

  5. Putin awashukuru wanajeshi kwa 'kukomboa' eneo la Luhansk

    Rais wa Urusi Vladimir Putin amewapongeza wanajeshi wa Urusi kwa "kukomboa" eneo la mashariki mwa Ukraine la Luhansk, huko Donbas.

    Katika mkutano wa televisheni na Waziri wa Ulinzi Sergei Shoigu, Putin anasema wanajeshi waliohusika katika operesheni hiyo wanapaswa kupumzika, lakini vitengo vingine vya kijeshi vinapaswa kuendelea na mapigano.

    Putin pia amewatunuku cheo cha "shujaa wa Urusi" majenerali wawili kufuatia kutekwa kwa eneo hilo.

    Urusi ilitangaza Jumapili kwamba sasa inadhibiti eneo lote la Luhansk baada ya kuuteka mji muhimu wa kimkakati wa Lysychansk.

    Moscow imesema kuwa ni "operesheni maalumu ya kijeshi" - kama inavyoita uvamizi wa Ukraine - inakusudiwa "kuikomboa" mashariki mwa Ukraine kutoka kwa "wazalendo wa Kiukreni". Eneo la mashariki limekuwa kitovu cha hatua yake ya kijeshi baada ya majaribio ya awali ya kuudhibiti mji mkuu Kyiv kushindwa.

    • Urusi na Ukraine: Ni kweli 'Ubabe' wa Putin ulisababisha vita ?
    • Mikakati mitatu ya NATO kukabiliana na Urusi na China
  6. Wanawake wawili wauawa na papa katika Bahari Nyekundu nchini Misri

    Maafisa wa Misri wanasema kuwa wanawake wawili wameuawa katika mashambulizi ya papa walipokuwa wakiogelea katika Bahari Nyekundu.

    Wizara ya mazingira inasema mashambulizi hayo yalitokea ndani ya mita 600 (futi 1,970) kutoka kwa kila mmoja.

    Mamlaka hapo awali ilitangaza kuwa mwanamke wa Austria mwenye umri wa miaka 60 alifariki kutokana na majeraha siku ya Ijumaa.

    Mwanamke wa Romania mwenye umri wa miaka 40 pia anasemekana kuuawa.

    Matukio hayo yametokea katika eneo la Hurghada, ambalo ni kituo kikuu cha watalii.

    Fukwe kadhaa zimefungwa katika eneo hilo kwa sababu hiyo

  7. Uganda yakana kutoa mafunzo kwa wapiganaji wa Tigray

    Jeshi nchini Uganda limekanusha ripoti kwamba linajaribu kuivuruga Ethiopia kwa kutoa mafunzo na kutoa msaada kwa chama cha Tigray People's Liberation Front - TPLF, ambacho kimekuwa na vita na serikali ya Ethiopia tangu 2020.

    Ripoti hizo zilionekana kuibuka mara ya kwanza mnamo Meikatika mitandao ya habari ya nchini Ethiopia.

    Msemaji wa Jeshi la Uganda Brigedia Felix Kulayigye alisema kupitia Twitter siku ya Jumapili kwamba madai ya majaribio ya Uganda kuyumbisha Ethiopia ni uzushi mtupu.

    Makala ya kina ilionekana wiki iliyopita katika kituo cha mtandaoni kilichoko New Zealand, pamoja na orodha ya maafisa wakuu wa jeshi la Uganda na wengine kutoka katika vikosi vya usalama, ambao wanadaiwa kuongoza operesheni ya mafunzo katika wilaya ya kati ya Uganda ya Masaka.

    Stakabadhi hiyo inaonyesha kuwa zaidi ya wanajeshi 4000 wa Tigray walipaswa kupewa mafunzo katika vituo vinne tofauti nchini Uganda.

    Ripoti hiyo inadai zaidi kwamba shughuli ya mafunzo inaungwa mkono na Marekani na Misri.

    Mmoja wa maafisa wakuu waliotajwa kwenye ripoti hiyo ni mtoto wa Rais na kamanda wa jeshi la nchi kavu la Uganda Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ambaye alituma ujumbe kwenye Twitter akiunga mkono vikosi vya Tigray, akiwataja kama "ndugu", mnamo 2021.

    Bado haijabainika stakabadhi hiyo ni ya kweli au ni sehemu ya kampeni ya habari ghushi. Tovuti ya New Zealand, inayojulikana kama Scoop, ilisema haikuweza kuthibitisha chanzo au ikiwa maelezo hayo yalikuwa sahihi au la.

    Lakini kuna baadhi ya vitu visivyoeleweka -Inamtaja James Kabarebe kuwa Waziri wa Ulinzi wa zamani nchini Uganda, lakini nchi hiyo haijawahi kuwa na waziri kwa jina hilo katika nafasi hiyo.

    Brigedia Kulayigye pia alisema katika Twitter kwamba madai ya ushirikiano kati ya Uganda na Sudan Kusini katika operesheni hiyo si ya kweli, kwa sababu balozi wa Uganda nchini Sudan Kusini, ambaye anatajwa kuwa mratibu wa sehemu ya operesheni hiyo, hajawahi kukutana na jenerali wa Sudan Kusini aliyetajwa katika ripoti.

  8. Tazama:Polisi walivyomfyatulia risasi mara 60 mwanaume mweusi huko Ohio

    Polisi wa Marekani wametoa kanda ya video wakimfuata kwa gari mshukiwa katika eneo la Akron, Ohio, ambayo iliishia kwa mtu mweusi kuuawa kwa kupigwa risasi, mara zaidi ya 60 na maafisa waliokuwa wakimfuata .

    Polisi wanaamini Jayland Walker, 25, alifyatua risasi kwanza na maafisa walihofia maisha yao katika tukio la trafiki usiku mnamo 27 Juni.

    Bw Walker hakuwa na silaha alipokimbiakuingia katika gari lake lakini polisi wanasema bastola ilipatikana ndani baadaye.

    Meya wa Akron aliwataka watu wa eneo hilo kuonyesha subira wakati maandamano yakianza.

    "Video hiyo inavunja moyo, ni ngumu kuipokea," Daniel Horrigan alisema baada ya video hiyo kutolewa Jumapili.

    Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dave Yost aliahidi "uchunguzi kamili, wa haki na wa kitaalamu" na Ofisi ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai ya Ohio huku polisi wa Akron wakifanya uchunguzi tofauti wa ndani ikiwa maafisa walikiuka sheria za idara au sera.

    Maafisa wanane waliohusika katika ufyatuaji risasi, saba kati yao ni wazungu na mmoja akiwa mweusi, wamepewa likizo ya kulipwa ya kiutawala.

    Wakili wa familia ya Bw Walker alisema maafisa waliendelea kufyatua risasi hata baada kuanguka .

  9. Wanasayansi wagundua spishi mpya mmea wa lily kubwa za maji

    Aina mpya ya lily kubwa ya maji imegunduliwa - na imekuwa ikijificha mahali pa wazi kwa miaka 177.

    Mmea huo mkubwa ulikuwa kwenye kumbukumbu za Royal Botanic Gardens, Kew na ulikuwa ukikua katika mkusanyiko wa majini lakini ulitambuliwa kimakosa kuwa spishi nyingine.

    Sasa utafiti wa kina wa kisayansi umebaini kuwa ni aina mpya kwa sayansi.

    Pia inashikilia rekodi ya kuwa yungiyungi mkubwa zaidi wa maji duniani, na majani yanakua zaidi ya 3m (10ft) kwa upana.

    Mmea huo umeitwa Victoria boliviana - jina lake baada ya Bolivia, ambapo hukua katika bonde moja la maji katika sehemu ya mfumo wa mto Amazon.

    Mtaalamu wa kilimo cha bustani Carlos Magdalena, mmoja wa wataalam wakuu duniani wa lily ya maji, kwa muda mrefu alishuku kuwa mmea huo ulikuwa tofauti na spishi zingine mbili kubwa zinazojulikana, Victoria amazonica na Victoria cruziana.

    Aliambia BBC News: "Ilimaanisha kwamba tunaweza kuikuza bega kwa bega na spishi zingine mbili chini ya hali sawa. Mara tu tulipofanya hivi tuliweza kuona wazi kwamba kila sehemu ya mmea ilikuwa tofauti kabisa.

  10. Viongozi wa Ecowas wameondoa vikwazo dhidi ya Mali

    Viongozi wa Afrika Magharibi wametangaza kuondolewa kwa vikwazo dhidi ya utawala wa kijeshi nchini Mali.

    Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Kiuchumi ya Afrika Magharibi (Ecowas) wanaokutana katika mji mkuu wa Ghana, Accra, walikubali pendekezo la jeshi la Mali la kufanya uchaguzi na kurejea katika utawala wa kiraia ifikapo Machi 2024.

    Umoja huo ulikuwa umeweka vikwazo vya kiuchumi vilivyodhoofisha baada ya maafisa wa jeshi kufanya mapinduzi mawili katika kipindi cha chini ya mwaka mmoja mnamo Agosti 2020 na Mei 2021.

    Pia ilikubali ratiba ya miaka miwili ya kurejeshwa kwa demokrasia nchini Burkina Faso, lakini iliiambia Guinea, nchi ya tatu ambayo imeshuhudia mapinduzi ya kijeshi, itakabiliwa na vikwazo vya kiuchumi isipokuwa inaweza kuharakisha kipindi chake cha miaka mitatu cha kurejea katika utawala wa demokrasia. .

  11. Shambulio la Denmark sio kitendo cha ugaidi - mkuu wa polisi

    Polisi wa Denmark wanasema hakuna dalili kwamba ufyatuaji risasi wa Jumapili ulikuwa kitendo cha kigaidi.

    Mshukiwa huyo alikuwa na historia ya matatizo ya afya ya akili, wanasema.

    Mkuu wa polisi wa jiji hilo, Soeren Thomassen, anasema mshukiwa alikuwa anajulikana na huduma za afya ya akili.

    "Mshukiwa pia anajulikana miongoni mwa huduma za magonjwa ya akili, zaidi ya hapo sitaki kutoa maoni," Thomassen amesema.

    Waathiriwa walionekana kulengwa bila mpangilio na hakukuwa na chochote cha kuashiria kuwa ni kitendo cha ugaidi, anaongeza.

    Watu wanne, wakiwemo raia wawili wa Uswidi, wako katika hali mahututi lakini wapo katika hali thabiti baada ya kupigwa risasi siku ya Jumapili, ambapo watu watatu waliuawa, mkuu wa polisi anasema.

    Watu watatu waliouawa kwa kupigwa risasi Jumapili wametambuliwa kama mwanamke na mwanamume wa Denmark, wote wenye umri wa miaka 17, na raia wa Urusi mwenye umri wa miaka 47 anayeishi Denmark, polisi wa Denmark walisema.

    Wengine wanne walijeruhiwa katika ufyatuaji risasi huo: wanawake wawili wa Denmark, wenye umri wa miaka 19 na 40, na raia wawili wa Uswidi, mwanamume mwenye umri wa miaka 50 na mwanamke mwenye umri wa miaka 16, mkuu wa polisi wa Copenhagen Soeren Thomassen anasema.

    Aliwaambia waandishi wa habari kwamba polisi hawaamini kwamba shambulio hilo lilihusiana na ugaidi.

    Video za mshukiwa zinazosambaa kwenye mitandao ya kijamii zinaaminika kuwa za kweli, polisi wanasema.

  12. Ukraine yathibitisha kuwa Urusi imeuteka mji wa mashariki wa Lysychansk

    Jeshi la Ukraine limethibitisha kuwa mji wa mashariki wa Lysychansk umeangukia mikononi mwa wanajeshi wa Urusi.

    "Baada ya mapigano makali dhidi ya Lysychansk, vikosi vya ulinzi vya Ukraine vililazimika kujiondoa kwenye nafasi zao," mkuu wa jeshi alisema

    Hapo awali Waziri wa Ulinzi wa Russia Sergei Shoigu alisema vikosi vyake vimeiteka Lysychansk na kuchukua udhibiti kamili wa eneo la Luhansk.

    Wanajeshi wa Ukraine walikuwa wamezidiwa huko.

    Mkuu wa majeshi yake alisema kwamba "ili kulinda maisha ya watetezi wa Ukraine, uamuzi ulifanywa wa kujiondoa".

    Alisema Warusi walikuwa na faida nyingi katika wingi wa silaha, ndege, wafanyikazi na vikosi vingine.

    Rais Volodymyr Zelensky aliahidi kwamba vikosi vya Ukraine vitarejea Lysychansk kutokana na mbinu zao na " kuongezeka kwa usambazaji wa silaha za kisasa".

    Hapo awali, mkuu wa Jamhuri ya Chechen ya Urusi, Ramzan Kadyrov, alichapisha video inayoonyesha wapiganaji wa Chechnya katikati mwa Lysychansk.

    Upande wa magharibi zaidi, mji unaoshikiliwa na Ukraine wa Sloyansk ulikabiliwa na mashambulizi makubwa ya makombora, huku takriban watu sita wakiuawa.

    Upo katika mkoa wa Donetsk, ambao pamoja na Luhansk zinaunda Donbas yenye viwanda.

    Muda mfupi kabla ya kuzindua vita, Rais Vladimir Putin alitambua Luhansk na Donetsk zote kuwa huru kutoka kwa Ukraine. Vikosi vinavyoungwa mkono na Urusi vilianza uasi huko mnamo 2014.

    Zaidi ya wiki moja iliyopita wanajeshi wa Urusi waliteka Severodonetsk, jiji lililokuwa magofu kwa majuma kadhaa ya mashambulizi ya Urusi.

  13. Hujambo na karibu kwa matangazo yetu ya moja kwa moja leo tarehe 4 Julai mwaka wa 2022