Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Maafisa wa Marekani watoa picha ya mshukiwa Rahmanullah Lakanwal

Rais Donald Trump, ambaye alikuwa Florida wakati huo, alisema mtu aliyefanya shambulizi kwa kutumia bunduki alikuwa raia wa Afghanistan ambaye aliingia Marekani mnamo Septemba 2021.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Maafisa wa Marekani watoa picha ya mshukiwa Rahmanullah Lakanwal

    Maafisa wa Marekani walionyesha picha ya mshukiwa. Jina lake ni Rahmanullah Lakanwal, Mwafghanistan aliyeishi katika jimbo la Washington, na ambaye hapo awali alifanya kazi na Marekani nchini Afghanistan.

    Mkurugenzi wa CIA John Ratcliffe, aliiambia CBS, mshirika wa BBC nchini Marekani, kwamba mshukiwa wa ufyatuaji risasi aliruhusiwa kuingia Marekani "kutokana na kazi yake ya awali na serikali ya Marekani".

    "Kufuatia kujiondoa kwa Biden kutoka Afghanistan, utawala wa Biden ulihalalisha kumleta mshukiwa huyo nchini Marekani mnamo Septemba 2021 kutokana na kazi yake ya awali na serikali ya Marekani, ikiwa ni pamoja na CIA, kama afisa wa kikosi mshirika huko Kandahar, ambacho kilimalizika muda mfupi baada ya kuondolewa," Ratcliffe anasema.

  2. Venezuela yapiga marufuku mashirika sita makubwa ya ndege baada ya mvutano na Marekani kuongezeka

    Venezuela imepiga marufuku mashirika sita makubwa ya ndege ya kimataifa kutua nchini humo baada ya kushindwa kufikia tarehe ya mwisho ya saa 48 ya kuanza tena safari za ndege huko.

    Mashirika hayo ya ndege yalikuwa yamesitisha kwa muda njia zao kuingia katika mji mkuu, Caracas, baada ya Marekani kuonya kuhusu "shughuli za kijeshi zilizoongezeka" katika eneo hilo.

    Ikiwa imekasirishwa na hili, serikali ya Venezuela ilitoa amri ya mwisho ambayo iliisha Jumatano.

    Huku mashirika kadhaa madogo ya ndege yakiendelea kuruka hadi Venezuela, maelfu ya abiria wameathiriwa. Marekani imetuma kikosi kikubwa kuisaidia Venezuela, ambayo inasema ni kupambana na biashara ya dawa za kulevya lakini ambayo kiongozi wa Venezuela ameishutumu kama jaribio la kumpindua.

    Unaweza kusoma;

  3. Watu wasiopungua 55 wamefariki na mamia hawajulikani walipo baada ya moto kuteketeza majengo Hong Kong

    Watu wasiopungua 55 wamepoteza maisha katika moto mkubwa ulioteketeza majengo mengi marefu huko Hong Kong, moto mbaya zaidi jijini kuwahi kutokea katika zaidi ya miaka 70.

    Baadhi ya wakazi bado wamekwama ndani ya majengo hayo, huku zaidi ya watu 270 wakiwa hawajulikani waliko.

    Mamia ya maafisa zima moto wamekuwa wakikabiliana na moto huo, ambao sasa unadhibitiwa kwa kiasi kikubwa katika majengo yote yaliyoathiriwa .

    Jengo la makazi lilikuwa likifanyiwa ukarabati mkubwa wakati moto ulipoanza. Chanzo halisi hakijulikani lakini polisi wanasema vifaa vilivyo nje ya majengo hayo vinaweza kuwa viliwezesha kuenea kwake.

    Watendaji watatu wa kampuni ya ujenzi wamekamatwa kwa tuhuma za mauaji bila kukusudia na uzembe mkubwa.

    Moto huo ulianza saa 14:51 saa za huko (06:51 GMT) siku ya Jumatano, huku miali ya moto na mawingu mazito ya moshi wa kijivu yakionekana kutoka kwenye minara, yakitawala anga ya jiji.

    Watu hamsini na mmoja walifariki katika eneo la tukio, huku wengine wanne wakifariki hospitalini. Afisa wa zimamoto Ho Wai-ho, mwenye umri wa miaka 37, alikuwa miongoni mwa waliopoteza maisha katika moto huo.

    Alipatikana ameanguka katika eneo la tukio kama dakika 30 baada ya kupotea kwa mawasiliano naye.

    "Nimehuzunika sana," Jason Kong mwenye umri wa miaka 65 aliliambia shirika la habari la Reuters. "Sijui kinachoendelea tena. Tazama, vyumba vyote vinaungua tu. Sijui la kufanya."

    Alisema jirani alikuwa amempigia simu na kusema bado alikuwa amenaswa ndani ya moja ya majengo ya mnara. Joto kali la moto huo, pamoja na uchafu hatari unayotokana na kuanguka kwa mnara, imezuia juhudi za uokoaji, lakini idara ya zimamoto ilisema haikuwa ikizuia kupata watu zaidi waliojeruhiwa ndani.

    "Joto ndani ya majengo husika ni kali sana, kwa hivyo ni vigumu sana kwetu kuingia... na kupanda ghorofani kufanya operesheni ya kuzima moto na uokoaji," alisema Derek Armstrong Chan, naibu mkurugenzi wa huduma za zimamoto.

  4. Marekani yasitisha maombi ya uhamiaji kwa Waafghanistan baada ya wanajeshi wake kupigwa risasi

    Marekani imesitisha kushughulikia maombi yote ya uhamiaji kutoka kwa Waafghanistan, baada ya mwanaume mmoja wa Afghanistan kutambuliwa kuwa mshukiwa wa tukio la kuwapiga risasi wanajeshi wawili wa Walinzi wa Taifa karibu na Ikulu ya White House.

    Huduma ya Uraia na Uhamiaji ya Marekani ilisema uamuzi huo ulifanywa ikisubiri mapitio ya "itifaki za usalama na uchunguzi".

    Mshukiwa wa ufyatuaji risasi siku ya Jumatano, ambao uliwaacha maafisa wawili wakiwa wamejeruhiwa vibaya, inasemekana aliwasili Marekani kutoka Afghanistan mnamo Septemba 2021.

    Rais wa Marekani Donald Trump alisema shambulio hilo lilikuwa "kitendo cha ugaidi", akiongeza kuwa atachukua hatua za kuwaondoa wageni "kutoka nchi yoyote ambayo haistahili kuwa hapa".

    Makumi ya maelfu ya Waafghanistan waliingia Marekani chini ya ulinzi maalum wa uhamiaji kufuatia kujiondoa kwa Marekani nchini Afghanistan mwaka 2021 chini ya Rais wa zamani Joe Biden.

  5. Polisi wachunguza wizi wa mbwa wanne kutoka ikulu ya rais Malawi

    Polisi nchini Malawi wanachunguza jinsi mbwa wanne wa polisi walivyopotea kutoka ikulu ya rais katika mji mkuu, Lilongwe, wakati wa mpito wa kisiasa mwezi Septemba.

    Godfrey Arthur Jalale, ambaye alihudumu kama naibu mkuu wa wafanyakazi wa Ikulu chini ya Rais wa zamani Lazarus Chakwera, amekamatwa kuhusiana na wizi wa mbwa wanne wa German Shepherds.

    Anakana shtaka hilo. Chakwera alihama ikulu baada ya kushindwa katika uchaguzi na Rais Peter Mutharika, ambaye alirejea kwa njia ya kushangaza.

    Jumatano jioni, polisi walikana ripoti kwamba Chakwera alikuwa amekamatwa lakini walithibitisha kupata kibali cha upekuzi wa makazi yake baada ya taarifa kueleza mbwa walioibwa walikuwa wakiwekwa hapo.

    Vyombo vya habari vya ndani vimeripoti wizi wa mali ya serikali kutoka kwenye makazi mawili ya rais, Jumba la Kamuzu, na Jumba la Sanjika, huko Blantyre, jiji la pili kwa ukubwa nchini.

    Mbwa hao wanne, wenye thamani ya $2,300 (£1,700), walitolewa nje ya jumba hilo kati ya Septemba 19 na Oktoba 4, kulingana na waendesha mashtaka wa serikali.

    Katika taarifa siku ya Jumatano, polisi walisema "wameongeza uchunguzi kufuatia ripoti za uporaji wa mali" kutoka Jumba la Kamuzu.

    "Huduma ya Polisi ya Malawi inawahakikishia umma kwamba uchunguzi unaendelea vizuri," iliongeza. Wabunge wa MCP walisusia vikao vya bunge Jumatano na kupiga kambi katika makazi ya Chakwera huko Lilongwe.

  6. Aliyekuwa rais wa Peru ahukumiwa kifungo cha miaka 14 jela

    Mahakama ya Peru Jumatano imemhukumu Rais wa zamani Martin Vizcarra kifungo cha miaka 14 jela baada ya kumpata na hatia ya kuchukua hongo miaka kadhaa kabla ya kuchukua madaraka, na kuongeza orodha ya viongozi wa zamani waliofungwa jela kwa ufisadi.

    Kulingana na uamuzi huo, Vizcarra alipokea hongo sawa na $676,000 kutoka kwa makampuni ya ujenzi badala ya kandarasi za kazi za umma alipokuwa gavana wa eneo la kusini la Moquegua kuanzia 2011 hadi 2014.

    Wakati wote wa kesi hiyo iliyoanza Oktoba iliyopita, Vizcarra alikanusha mashtaka hayo, akidai alikuwa mwathirika wa mateso ya kisiasa. Aliingia madarakani mwaka wa 2018 baada ya mtangulizi wake kujiuzulu na akafukuzwa miaka miwili baadaye na Bunge huku kukiwa na uchunguzi wa ufisadi.

    "Hii sio haki, ni kulipiza kisasi," Vizcarra alisema katika chapisho kwenye X baada ya hukumu yake. "Lakini hawatanimaliza."

    Timu yake ya wanasheria ilithibitisha kuwa imekata rufaa dhidi ya hukumu hiyo, ambayo pia ilimpiga marufuku Vizcarra kushikilia ofisi ya umma kwa miaka tisa.

    Kaka yake mkubwa, Mario Vizcarra, anapanga kugombea katika uchaguzi wa rais wa Aprili 2026 kwa chama cha "Peru Kwanza", ambapo rais huyo wa zamani amewahi kuwa mshauri mkuu.

    Timu yake ya wanasheria ilithibitisha kuwa imekata rufaa dhidi ya hukumu hiyo, ambayo pia ilimpiga marufuku Vizcarra kushikilia ofisi ya umma kwa miaka tisa.

    Kaka yake mkubwa, Mario Vizcarra, anapanga kugombea katika uchaguzi wa rais wa Aprili 2026 kwa chama cha "Peru First", ambapo rais huyo wa zamani amewahi kuwa mshauri mkuu.

  7. Kundi la Marekani laishtaki Apple juu ya mzozo wa madini ya Congo

    Kundi la mawakili lenye makao yake makuu nchini Marekani limefungua kesi mjini Washington likiishutumu kampuni ya Apple kwa kutumia madini yanayohusishwa na migogoro na ukiukaji wa haki za binadamu katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Rwanda licha ya kampuni ya kutengeneza iPhone kukanusha madai hayo.

    Mawakili wa Kimataifa wa haki za binadamu (IRAdvocates) awali, waliwahi kufungua kesi dhidi ya makampuni ya teknolojia ikiwa ni pamoja na Tesla, Apple na makampuni mengine kuhusu upatikanaji wa madini ya cobalti, lakini mahakama za Marekani zilitupilia mbali kesi hiyo mwaka jana.

    Waendesha mashtaka wa Ufaransa pia walitupilia mbali kesi ya Congo dhidi ya kampuni tanzu za Apple mnamo mwezi Desemba kuhusu madini yanayokumbwa na mzozo, kwa sababu ya ukosefu wa ushahidi.

    Malalamiko ya jinai yanayohusiana na hayo nchini Ubelgiji bado yanachunguzwa.

    Apple ilikanusha kufanya makosa yoyote katika kujibu mashtaka ya Congo, ikisema iliwaagiza wanaowauzia kusitisha utafutaji wa nyenzo kutoka Congo na nchi jirani ya Rwanda.

    Apple ilisema Jumatano "inapinga vikali" madai ya hivi punde kwamba kampuni hiyo inanufaika kutokana na kazi ya kulazimishwa na uchimbaji madini usio salama barani Afrika, na kuyataja madai hayo kuwa "hayana msingi."

    Soma zaidi:

  8. Wakenya 125 matajiri zaidi wanamiliki mali nyingi zaidi ya watu milioni 42.6 - Oxfam

    Takriban nusu ya wakazi wa Kenya wanaishi katika umaskini uliokithiri - kwa chini ya Ksh.130 kwa siku - ripoti mpya ya Oxfam Kenya inafichua.

    Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa watu 125 matajiri zaidi nchini Kenya wanamiliki mali nyingi zaidi ya watu milioni 42.6, huku kukiwa na ongezeko la viwango vya umaskini.

    Ripoti iliyopewa jina la ‘Mgogoro wa Kukosekana kwa Usawa wa Kenya: Mgawanyiko Mkubwa wa Kiuchumi’ ilitolewa Jumatano, Novemba 11, 2025, kuonyesha kwamba idadi ya watu wanaoishi katika umaskini uliokithiri imeongezeka kwa milioni 7 (37%) tangu 2015.

    Matokeo hayo pia yanaonyesha kuwa ukosefu wa ufadhili wa kutosha wa elimu, afya na kilimo kwa ajili ya kutoa kipaumbele kwa ulipaji wa madeni umechangia kuongeza pengo kati ya matajiri wakubwa na wale wanaoishi katika umaskini uliokithiri.

    Mnamo mwaka 2024, kati ya kila Ksh.100 zilizochukuliwa kama kodi, Ksh.68 zilitumika kulipa deni - mara mbili ya bajeti ya elimu na karibu mara 15 ya bajeti ya afya ya kitaifa.

    Soma zaidi:

  9. Waangalizi wa uchaguzi wa AU na ECOWAS wasikitishwa na tangazo la mapinduzi Guinea-Bissau

    Viongozi wa Umoja wa Afrika na wa ECOWAS wa ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi nchini Guinea-Bissau wameelezea "wasiwasi mkubwa juu ya tangazo la mapinduzi ya serikali na vikosi vya jeshi".

    Katika taarifa ya pamoja ambayo pia ilijumuisha mkuu wa Mkutano wa Wazee wa Afrika Magharibi, maafisa hao walisema nchi ilikuwa tayari kwa tangazo la matokeo ya uchaguzi baada ya kile kilichoelezwa kama mchakato wa "taratibu na amani".

    "Ni jambo la kusikitisha kwamba tangazo hili lilikuja wakati ambapo ujumbe ulikuwa umemaliza mkutano na wagombea wawili wa urais, ambao walituhakikishia utayari wao wa kukubali mapenzi ya raia", walisema.

    Waangalizi wa kikanda pia walikosoa kukamatwa kwa maafisa kadhaa wa ngazi ya juu nchini humo ikiwa ni pamoja na maafisa wa uchaguzi, wakidai waachiliwe huru mara moja.

    Walielezea mapinduzi ya kijeshi ya Jumatano kama "jaribio la wazi" la kuvuruga maendeleo ya demokrasia ya nchi.

    Wakati wakishtumu hatua hiyo, viongozi hao pia walihimiza Umoja wa Afrika na ECOWAS kuhakikisha kwamba utaratibu wa kikatiba unarejeshwa katika taifa hilo la Afrika Magharibi lenye watu zaidi ya milioni mbili.

    Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ambaye anafuatilia kwa karibu hali hiyo, amewahimiza wale wanaohusika katika hali ya nchini Guinea-Bissau "kuonyesha kujizuia" na "kuheshimu utawala wa sheria".

    Canada pia ilitoa ushauri wa kusafiri kwa wananchi wake muda mfupi baada ya utawala wa kijeshi wa Guinea-Bissau.

    Soma zaidi:

  10. Rais wa Nigeria atangaza hali ya dharura ya usalama

    Rais wa Nigeria Bola Ahmed Tinubu ametangaza hali ya dharura ya usalama wa kitaifa katikati ya ongezeko kubwa la mashambulizi ya mauaji na utekaji nyara wa watu wengi katika majimbo kadhaa nchini humo.

    Katika agizo lenye maneno makali lililotolewa Jumatano, aliamuru kuongezwa haraka kwa vikosi vya usalama wa nchi na hatua kali kuchukuliwa kukabiliana na kile alichokiita "mawakala wa uovu" wanaodhoofisha taifa.

    Kwa mujibu wa amri mpya, Jeshi la Polisi la Nigeria lazima liongeze maafisa wengine 20,000 - na kuongeza jumla ya idadi iliyopangwa hadi 50,000.

    Rais pia aliidhinisha matumizi ya kambi za National Youth Service Corps (NYSC) kama vituo vya mafunzo vya muda ili kuharakisha kupelekwa kwao kuanza majukumu.

    Pia alitoa maagizo kwamba maafisa wa polisi walioondolewa katika kazi za ulinzi wa watu mashuhuri wapate mafunzo ya dharura kabla ya kupelekwa katika maeneo hatari.

    "Idara ya Huduma za Jimbo pia ina mamlaka yangu kupeleka mara moja walinzi wote wa misitu ambao tayari wamepata mafunzo kukabiliana na magaidi na majambazi wanaokaa kwenye misitu yetu na kuajiri wengine zaidi kulinda misitu.

    Hakutakuwa na mahali pa kujificha zaidi kwa mawakala wa uovu," Rais Tinubu alisema.

    Rais alisisitiza kwamba shughuli za kuwaokoa wanafunzi waliotekwa nyara kutoka shule ya Katoliki ya St. Mary katika Jimbo la Niger - na Wanigeria wengine ambao bado wanashikiliwa na vikundi vyenye silaha - zitaendelea "bila kukoma".

    Pia alihimiza bunge kuanza kupitia sheria za Nigeria kuruhusu majimbo ambayo yanataka jeshi la polisi "kikanda" kufanya hivyo kisheria - mahitaji ya muda mrefu wakati ukosefu wa usalama unaoendelea kuzorota.

    Bwana Tinubu alionya serikali dhidi ya kuanzisha shule za bweni katika wilaya zilizotengwa bila ulinzi wa kutosha, na kutoa wito kwa makanisa na misikiti katika jamii zilizo hatarini kudumisha uratibu wa usalama wa karibu.

    Soma zaidi:

  11. Idadi ya vifo katika mkasa wa moto Hong Kong inaongezeka mamlaka zinasema

    Zaidi ya watu arobaini wamethibitishwa kufariki katika moto mkubwa ulioteketeza majengo kadhaa ya ghorofa huko Hong Kong.

    Watu wengine 45 wako hospitalini katika hali mbaya huku wengine 279 wakiwa bado hawajulikani walipo.

    Watu watatu wamekamatwa kwa tuhuma za mauaji - wawili ni wakurugenzi wa kampuni ya ujenzi na mmoja ni mshauri wa uhandisi.

    Wakati chanzo cha moto huo kikiendelea kuchunguzwa, polisi wanasema wavu na makaratasi ya plastiki yalipatikana kwenye madirisha ya majengo hayo yaliyokuwa yakifanyiwa ukarabati. Polisi wanasema huenda vifaa hivi zilisababisha moto huo kuenea kwa haraka zaidi.

    Asubuhi ya leo, moshi bado unafuka kutoka kwa baadhi ya majengo ya ghorofa - lakini moto huo umedhibitiwa katika majengo manne kati ya nane.

    Idara ya zima moto inatarajia kuchukua siku nzima kudhibiti moto huo.

    Mamia ya wakaazi wamehamishwa hadi kwenye makazi ya muda na nyumba za dharura zinatengewa watu wanaohitaji kuhamishwa.

    Idara ya zimamoto ya Hong Kong imeainisha moto huo kama wa kiwango cha tano – ikimaanisha ni mkubwa zaidi.

    Imepita miaka 17 tangu moto wa kiwango cha tano ulipoikumba Hong Kong mara ya mwisho.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Wanajeshi wa Marekani wapigwa risasi karibu na Ikulu ya White House

    Wanajeshi wawili wa Ulinzi wa Kitaifa wamejeruhiwa vibaya baada ya kupigwa risasi huko Washington DC karibu na Ikulu ya White House, katika kile meya wa jiji hilo amekiita "shambulio la kulengwa".

    Polisi walisema mshukiwa mmoja aliwafyatulia risasi walinzi wawili siku ya Jumatano alasiri, kabla ya kuzingirwa na kukamatwa na Walinzi wengine wa Kitaifa waliokuwa karibu ambao walikuwa wamesikia milio ya risasi.

    Rais Donald Trump, ambaye alikuwa Florida wakati huo, alisema mtu aliyefanya shambulizi kwa kutumia bunduki alikuwa raia wa Afghanistan ambaye aliingia Marekani mnamo Septemba 2021.

    Aliapa kwamba utawala wake utahakikisha mshukiwa "analipa gharama kubwa zaidi" kwa "kitendo cha ugaidi".

    Vyanzo vingi vya utekelezaji wa sheria hapo awali vilimtaja mtu anayedaiwa kuwa na bunduki kwa mshirika wa BBC wa Marekani CBS kuwa ni Rahmanullah Lakanwal, raia wa Afghanistan mwenye umri wa miaka 29.

    "Lazima sasa tuchunguze upya kila raia wa kigeni ambaye ameingia nchini mwetu kutoka Afghanistan chini ya [Rais wa zamani Joe] Biden," Trump alisema katika hotuba ya moja kwa moja Jumatano usiku.

    Mshukiwa alipigwa risasi nne, vyanzo vya utekelezaji sheria viliiambia CBS.

    Haijulikani ni silaha gani ilitumika katika shambulio hilo wala nia haikubainika wazi mara moja.

    Mshukiwa hakuwa akishirikiana na mamlaka, vyanzo vya kutekeleza sheria viliiambia CBS Jumatano usiku.

  13. Hujambo. Karibu katika matangazo ya leo ikiwa ni tarehe 27/11/2025.