Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Moja kwa moja, Mapigano kati ya Israel na Hezbollah nchini Lebanon yaua mamia

Iran inaonya kuwa itajibu ikiwa Israel haitasitisha mara moja mashambulizi dhidi ya Lebanon, ambapo takriban watu 182 wamethibitishwa kuuawa, idadi ikihofiwa kuwa kubwa zaidi.

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Iran yaziambia meli jinsi ya kuepuka mabomu katika Mlango Bahari wa Hormuz

    Meli zinazopanga kupita katika Mlango-Bahari wa Hormuz zinapaswa kuchukua njia mbadala, ili "kuzingatia kanuni za usalama wa baharini na kulindwa kutokana na mashambulizi ya mabomu yanyaoweza kutokea baharini", Walinzi wa Mapinduzi wa Iran walisema katika taarifa iliyonukuliwa katika vyombo vya habari vya serikali ya Iran.

    Taarifa hiyo inaendelea kuelezea njia mbadala, pamoja na ramani ya kuwaelekeza. Meli zinazoingia kutoka Bahari ya Oman zinapaswa kusafiri kuelekea kaskazini mwa Kisiwa cha Larak, kisha kuendelea kuelekea Ghuba ya Uajemi.

    Meli zinazoelekea upande mwingine zinapaswa kutoka Ghuba ya Uajemi, kupita kusini mwa Kisiwa cha Larak na kuendelea kuelekea Bahari ya Oman.

    Pia unaweza kusoma:

  2. Israel yafungua tena maeneo matakatifu ya Yerusalemu

    Polisi wa Israel wanasema maeneo matakatifu ya Yerusalemu yatafunguliwa tena kwa wageni na waumini kufuatia mpango wa muda wa kusitisha mapigano uliofikiwa katika mzozo wa Mashariki ya Kati.

    Maeneo hayo, ikiwa ni pamoja na eneo la msikiti wa Al-Aqsa, Ukuta wa Magharibi unaojulikana kama Western Wall, na Kanisa la Kaburi Takatifu, yote yakiwa kwenye Jiji la Kale, ni miongoni mwa maeneo matakatifu zaidi duniani katika Uislamu, Uyahudi na Ukristo.

    Kwa sababu ya vita dhidi ya Iran vilivyoanzishwa na Marekani na Israeli wiki sita zilizopita, maeneo hayo yamefungwa wakati wa sikukuu muhimu za kidini, ikiwa ni pamoja na wakati wa Pasaka huku idadi ndogo sana ya makasisi ikikubaliwa.

    Jiji la Kale, ambapo maeneo yake kwa kawaida huwa na shughuli nyingi za wakazi, wanaoenda sokoni, watalii na waumini, limekuwa kimya sana, huku wamiliki wengi wa maduka na vibanda wakishindwa kufungua kabisa.

    Polisi walisema kwamba maeneo matakatifu yatafunguliwa tena kuanzia Alhamisi asubuhi, huku mamia ya maafisa wengine wakipelekwa ili kuhakikisha usalama, na umma unahimizwa kuwa na subira ikiwa kutakuwa na msongamano.

    Pia unaweza kusoma:

  3. Trump asema, 'Nato haikuwepo tulipowahitaji'

    Muda mfupi uliopita, Rais wa Marekani Donald Trump alichapisha kwenye mtandao wa Truth Social kwa mara ya kwanza tangu alipokutana na mkuu wa Nato Mark Rutte katika Ikulu ya White House.

    "NATO HAIKUWEPO TULIPOWAHITAJI, NA HAWATAKUWAPO IKIWA TUTAWAHITAJI TENA. KUMBUKA GREENLAND, KIPANDE KILE KIKUBWA CHA BARAFU, KINACHOSIMAMIWA VIBAYA!!!"

    Inaonekana Trump amerejelea lengo lake lililotajwa hapo awali la kujumuisha eneo la Denmark kuwa Marekani, hatua ambayo ilipingwa na washirika wengi wa Marekani katika Nato.

    Hapo awali Rutte aliiambia CNN kwamba mkutano wao ulikuwa wa kuambiana "ukweli", na kwamba anaamini "kabisa" kwamba dunia iko salama zaidi baada ya mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

    Awali, Katibu Mkuu wa Nato, Mark Rutte alikutana na Donald Trump, na kuelezea mkutano wao kama wa kuambiana "ukweli" wenye uwazi, licha ya kutokubaliana.

    Rutte alikuwa Ikulu ya White House kwa zaidi ya saa mbili.

    Hata hivyo, kilicho wazi ni kwamba Trump bado ana mashaka makubwa kuhusu muungano huo na nchi wanachama ambazo anaamini hazikuisaidia Marekani vya kutosha kabla na wakati wa Operesheni ya Epic Fury iliyofanyika Iran.

    Uhusiano kati ya utawala na muungano wa Nato ulikuwa tayari katika hali mgumu kabla ya vita na Iran, hasa kutokana na kutokubaliana kuhusu mipango ya Trump kwa Greenland.

    Hata hivyo, mzozo nchini Iran umeongeza malalamiko ya Trump na Nato katika viwango vipya na kusababisha kile ambacho labda ni changamoto kubwa zaidi ambayo imekabiliana nayo katika historia yake.

    Soma zaidi:

  4. Israel yashambuliana na Hezbollah nchini Lebanon

    Ni zaidi ya saa 24 tangu Rais wa Marekani Donald Trump atangaze kusitisha mapigano kwa wiki mbili nchini Iran, jambo ambalo Israel, Iran na wapatanishi wa Pakistan walilithibitisha.

    Lakini tayari makubaliano ya amani yanaonyesha kuyumba.

    Israel imeanzisha wimbi kubwa la mashambulizi nchini Lebanon, na kuua watu wasiopungua 182.

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ameelezea mashambulizi hayo kama "pigo kubwa zaidi" kwa Hezbollah tangu kuanza kwa vita, akisema Israel itaanza tena kupigana na Iran kukiwa na haja ya "kufanya hivyo".

    Wakati huo huo, Iran imesema ikiwa mashambulizi nchini Lebanon hayatakoma mara moja huenda yakachochea "hatua kuchukuliwa".

    Siku ya Jumamosi, Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance atashiriki katika mazungumzo na Iran mjini Islamabad, Pakistan.

    Jambo la msingi litakuwa usafiri wa meli katika Mlango-Bahari wa Hormuz, njia ya baharini katika Ghuba ya Uajemi ambayo ni muhimu kwa usambazaji wa mafuta duniani.

    Iran imesema meli "zitalengwa na kuharibiwa" ikiwa zitapita bila ruhusa.

    Spika wa bunge la Iran pia anasema mambo matatu ya kusitisha mapigano kwenye mapendekezo yenye masuala 10 "yamekiukwa waziwazi", huku Vance akisema kila mara kuna "mapungufu" katika makubaliano kama hayo.

    Hezbollah yasema imeshambulia kaskazini mwa Israel

    Vile vile, Hezbollah imesema imerusha makombora kaskazini mwa Israeli.

    Wanamgambo hao wanaoungwa mkono na Iran wanasema ilikuwa ni kujibu ukiukwaji wa mapigano, katika taarifa iliyochapishwa kwenye mitandao ya kijamii.

    Pia wametishia kuendelea na mashambulizi hadi "uchokozi wa Israel na Marekani" dhidi ya Lebanon utakapokoma.

    Bado kuna kutokubaliana kuhusu kama nchi hiyo imejumuishwa katika usitishaji mapigano.

    Soma zaidi:

  5. Hujambo msomaji wetu. Karibu katika matangazo ya moja kwa moja ya tarehe 09/04/2026.