Moja kwa moja, Netanyahu aonya Israel itaendelea kuishambulia Hezbollah, Iran ikisema mashambulizi yanakiuka usitishaji mapigano

Iran inaonya kuwa itajibu ikiwa Israel haitasitisha mara moja mashambulizi dhidi ya Lebanon, ambapo takriban watu 182 wamethibitishwa kuuawa, idadi ikihofiwa kuwa kubwa zaidi.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Asha Juma & Ambia Hirsi

  1. Marekani yawaonya raia wake kuhusu kusafiri kwenda Nigeria kwa sababu za usalama

    Nigeria ina ushirikiano wa muda mrefu na Marekani katika masuala ya ujasusi, usalama na kupambana na ugaidi.

    Chanzo cha picha, AFP via Getty Images

    Maelezo ya picha, Nigeria ina ushirikiano wa muda mrefu na Marekani katika masuala ya ujasusi, usalama na kupambana na ugaidi.

    Marekani imewataka raia wake kufikiria upya kuhusu kusafiri kwenda Nigeria, ikitaja hatari kama vile ugaidi, machafuko ya kiraia na utekaji nyara.

    Tahadhari ya usafiri ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani iliyotolewa Jumatano iliongeza kuwa majimbo fulani ya Nigeria ambayo yana hatari kubwa yamewekwa chini ya tahadhari kali zaidi linaloshauri kutoenda kabisa katika maeneo hayo.

    Washington pia imeidhinisha kuondoka kwa wafanyakazi wake “wasio wa dharura” pamoja na familia zao kutoka ubalozi wa Marekani mjini Abuja, kufuatia kile inachokiita “kuzorota kwa hali ya usalama” kote nchini.

    Tahadhari hiyo inatolewa wakati kukiwa na ongezeko jipya la mashambulizi katika baadhi ya maeneo ya nchi, licha ya ushirikiano unaokua wa kiusalama kati ya mataifa hayo mawili.

    Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Washington imekuwa ikishirikiana na Abuja katika kupambana na ugaidi, usalama wa baharini, kubadilishana taarifa za kijasusi na mafunzo ya kijeshi.

    Ushirikiano wa hivi karibuni umejumuisha msaada wa ufuatiliaji na uchunguzi wa anga, pamoja na matumizi ya ndege na helikopta zilizotolewa na Marekani na kutumiwa na vikosi vya Nigeria dhidi ya wanamgambo wa Kiislamu na makundi yenye silaha.

    Uamuzi wa kupunguza wafanyakazi wa ubalozi unaonesha pengo lililopo kati ya ushirikiano wa kimkakati wa kijeshi na hali halisi ya ukosefu wa usalama wa kila siku unaowakabili raia katika maeneo mengi ya nchi.

    Katika tahadhari hiyo ya usafiri, raia wa Marekani walionywa kuwa mashambulizi yanaweza kutokea bila onyo katika maeneo ya umma ikiwemo masoko, hoteli, maeneo ya ibada, shule na vituo vya usafiri.

    Unaweza kusoma;

  2. Rais wa Iran aonya kuwa wako tayari 'kunyanyua tena silaha' akishutumu Israel kwa kukiuka makubaliano ya kusitisha mapigano

    .

    Chanzo cha picha, Iran's Presidential website/WANA (West Asia News Agency)/Handout via REUTERS

    Rais wa Iran anayataja mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon kuwa ni "ukiukaji wa wazi" wa makubaliano ya kusitisha mapigano, na anasema ni "kiashiria hatari" cha ukosefu wa utashi wa utekelezaji wa makubaliano.

    Matamshi hayo yanakuja siku moja baada ya jeshi la Israel kusema kuwa limeipiga Lebanon kwa zaidi ya mashambulizi 100 ya anga, kwa kile inachoeleza kuwa ni malengo ya Hezbollah.

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu anasema Israel itaendelea kuishambulia Hezbollah "inapobidi".

    Katika chapisho kwenye X, Masoud Pezeshkian anasema ''haina maana'' kufanya mazungumzo huku mashambulizi yakiendelea upande mwingine na kuonya kwamba Iran "haitasita kurejea vitani".

    Huku hayo yakijiri, spika wa Bunge la Iran anaonya kuwa "ukiukaji wa makubaliano ya kusitisha vita utasababisha hasara na utajibiwa vikali".

    Mohammad-Bagher Ghalibaf anasema Lebanon ni "sehemu ya makubaliano ya usitishaji mapigano", na kwamba hakuna "nafasi ya kupinga hilo au kubadili msimamo".

    "Komesheni mashambulizi mara moja," anasema.

  3. Zaidi ya watu 3,000 wameuawa nchini Iran tangu kuanza kwa vita, vyombo vya habari vya ndani vinaripoti

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Vyombo vya habari vya Iran, vinamnukuu mkuu wa Shirika la Tiba ya Uchunguzi nchini humo Abbas Masjedi Arani, vikiripoti kuwa zaidi ya watu 3,000 wameuawa nchini humo tangu mzozo huo uanze tarehe 28 Februari.

    Kufikia tarehe 7 Aprili, Shirika la Habari la Wanaharakati wa kutetea Haki za Binadamu lenye makao yake nchini Marekani (HRANA) linasema kuwa raia 1,701 wamefariki, wakiwemo watoto wasiopungua 254.

    HRANA pia inaripoti kuawa kwa wanajeshi 1,221 wameuawa na vifo vingine 714 ambavyo havikuwekwa bayana tangu mzozo huo uanze.

    Ni vigumu kwa mashirika ya habari kupata taarifa kutoka Iran.

    Mashirika ya habari ya kimataifa mara nyingi huzuiwa viza ya kuingia Iran, jambo ambalo linafanya kuwa kukusanya habari.

    Mtandao wa intaneti pia umepotea kwa muda mrefu (siku yake ya 41) sasa kulingana na tovuti ya ufuatiliaji wa mtandao wa NetBlocks.

    Maelezo zaidi:

  4. Balozi wa Iran afuta ujumbe kuhusu mazungumzo ya Marekani na Iran nchini Pakistan

    Balozi wa Iran nchini Pakistan amefuta aliyokuwa ameuchapisha kwenye mtandao wa X ambapo alisema wajumbe wa Iran walikuwa wakielekea Islamabad leo kuanza mazungumzo na Marekani.

    Mazungumzo hayo yanatarajiwa kufanyika Jumamosi na chini ya uongozi wa Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance.

    Katika ujumbe huo, Reza Amiri Moghadam alisema mazungumzo "yatazingatia vipengele 10 zilivyopendekezwa na Iran".

    Kama tulivyoripoti hapo awali, Marekani na Iran zina misimamo inayokinzana kuhusu vipengelei hivyo.

    Balozi huyo hakueleza ni kwa nini wujumbe huo umefutwa.

    Soma pia:

    '

    Chanzo cha picha, Reza Amiri Moghadam/X

  5. Netanyahu aonya Israel itaendelea kuishambulia Hezbollah 'itakapolazimika kufanya hivyo'

    Benjamin Netanyahu

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Maelezo ya picha, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu anasema Israel itaendelea kuishambulia Hezbollah "popote inapobidi", kufuatia makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Marekani na Israel.

    Hapo awali Israel ilieleza kuwa usitishaji vita huo haujumuishi Lebanon, hata hivyo Iran inasema kuendelea kwa mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon ni sawa na "ukiukaji mkubwa" wa makubaliano hayo.

    Netanyahu anasema: "Ujumbe wetu uko wazi: Yeyote anayefanya vitendo viovu dhidi ya raia wa Israel atakabiliwa." "Tutaendelea kuishambulia Hezbollah popote inapobidi, hadi tutakapoimarisha usalama kwa wakazi wa kaskazini."

    Kaulii yake inakuja baada ya Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) kutangaza kuuawa kwa Ali Yusuf Harshi, katibu na mpwa wa katibu mkuu wa Hezbollah Naim Qassem.

    Maelezo zaidi:

  6. Kenya yapinga ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu madai ya ubakaji Haiti

    Maafisa wa Kenya

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Kenya imepinga rasmi ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu tuhuma za ubakaji dhidi ya maafisa wake wanaohudumu nchini Haiti chini ya Ujumbe wa Kimataifa wa Usaidizi wa Usalama wa Kimataifa.

    Katika barua iliyotumwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Gutteres tarehe 7 Aprili, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Kenya Musalia Mudavadi alielezea wasiwasi wake kuhusu madai ya unyanyasaji wa kingono na dhuluma ambayo yaliripotiwa Agosti 2025.

    Mudavadi alisema madai hayo yalichunguzwa mara moja kupitia Bodi ya Uchunguzi na kupatikana kuwa hayana uthibitisho. "Hakuna malalamiko rasmi yaliyowasilishwa kwa mamlaka yoyote, na matokeo yaliwekwa wazi na mashirika ya Haiti na Umoja wa Mataifa" alisema.

    Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni aliongeza kuwa wafanyakazi wa MSS walifuata kikamilifu mifumo yote ya uendeshaji na kwamba hakuna ripoti zilizobainisha utovu wa nidhamu.

    Ripoti ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kutoka Februari na kuwekwa hadharani mwezi Aprili inaeleza maafisa chini ya ujumbe unaoongozwa na Kenya nchini Haiti walihusishwa katika visa vinne vya unyanyasaji wa kingono na unyanyasaji wa aina nyingine. Moja ikihusisha mtoto wa miaka 12.

    Ripoti hiyo inasema madai hayo yalithibitishwa na uchunguzi uliofanywa na Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa. Kulingana na Umoja wa Mataifa madai hayo yanachunguzwa. Haijabainika iwapo maafisa hao ni raia wa Kenya.

    Ujumbe unaoongozwa na Kenya, uliotumwa Haiti mwaka 2024 kusaidia kukabiliana na ghasia za magenge, kufuatia idhini ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, sasa nafasi yake imechukuliwa na Kikosi cha Kukakabiliana na Magenge.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Bei ya mafuta yapanda huku wasiwasi juu ya usitishaji mapigano

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Bei ya mafuta duniani imepanda huku wasiwasi ukiongezeka kuhusu iwapo makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Marekani na Iran yatadumu baada ya Israel kuanzisha wimbi la mashambulizi dhidi ya Lebanon.

    Mashambulizi hayo yalisababisha Iran kuonya kuhusu "vitendo vyake vyenye kuchochea hatua za kujibu kuchukuliwa" ikiwa mashambulizi yataendelea, huku Rais wa Marekani Donald Trump akisema vikosi vya nchi hiyo vitabaki katika eneo hilo hadi Iran itakapokubaliana na kuafikiwa kwa makubaliano "halisi" ya kusitisha mapigano.

    Wasiwasi unaendelea kuongezeka kuhusu kama njia muhimu ya meli ya Mlango Bahari wa Hormuz itafunguliwa.

    Siku ya Jumatano mara tu baada ya kutangazwa kwa usitishaji mapigano, bei ya mafuta ghafi ilipanda kwa 2.7% siku ya Alhamisi kwa $97.23 kwa pipa.

    Masoko ya hisa barani Asia yalishuka.

    "Nadhani kuna wasiwasi kidogo katika masoko ya kimataifa," Victoria Scholar, mkuu wa uwekezaji katika kampuni ya Interactive Investor, aliambia kipindi cha BBC Today.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon yalikuwa 'ukiukaji mkubwa' wa makubaliano - Iran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Saeed Khatibzadeh ameambia kipindi cha BBC Today katika mahojiano maalum kwamba mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon siku ya Jumatano yalikuwa "ukiukaji mkubwa" wa makubaliano ya kusitisha mapigano kati ya Marekani na Iran.

    Saeed Khatibzadeh anasema Iran ilituma ujumbe Ikulu ya Marekani jana usiku: "Huwezi kufanya vitu viwili vya kipekee kwa wakati mmoja."

    Aliongeza: "Huwezi kuomba kusitisha mapigano kisha ukubali masharti na sheria, ukubali maeneo yote yanayohusu kusitisha mapigano, na kutaja Lebanon, hasa Lebanon katika hili, na kisha mshirika wako anaanze mauaji ya halaiki."

    Khatibzadeh amesema mashambulizi ya Israel ni sawa na "aina ya mauaji ya halaiki".

    Israel inasisitiza kuwa inashambulia kundi la wanamgambo wa Hezbollah, ambalo lenyewe linarusha makombora nchini Israel.

    Marekani lazima ichague kati ya vita na kusitisha mapigano, Waziri amesema

    Katika mahojiano yake na BBC Today, naibu waziri wa mambo ya nje wa Iran aliendelea kusema, Marekani "lazima ichague" kama inataka vita au amani.

    "Hawawezi kuvipata vyote viwili kwa wakati mmoja. Ni vya kipekee kwa pande zote, na hilo liko wazi kabisa."

    Anasema Iran inawaomba "kila mtu Mashariki ya Kati kufuata makubaliano haya...na tunatarajia Wamarekani kufanya vivyo hivyo na washirika wake."

    Alipoulizwa na Nick Robinson kuhusu kama Iran itajiondoa kwenye mazungumzo ikiwa mashambulizi ya Israel yataendelea, alisema: "Tunazingatia sana ustawi wa Mashariki ya Kati nzima."

    Soma zaidi:

  9. Wapatanishi wa Iran waelekea Pakistan

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Balozi wa Iran nchini Pakistan amethibitisha kuwa ujumbe wa Iran unaelekea Pakistan hii leo kuanza mazungumzo na Marekani kuhusu kukomesha vita hivyo.

    Wanatarajiwa kukutana na Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance mjini Islamabad siku ya Jumamosi.

    Reza Amiri Moghadam, balozi wa Iran nchini Pakistani, anachapisha ujumbe kwenye X kwamba mazungumzo hayo "yatategemea vipengele 10 vilivyopendekezwa na Iran". Kama tulivyoripoti, kuna mkanganyiko kuhusu vipengele hivyo.

    Moghadam amesema mazungumzo hayo yatafanyika "licha ya kutiliwa shaka maoni ya umma wa Iran kutokana na ukiukwaji wa mara kwa mara wa kusitisha mapigano unaofanywa na utawala wa Israel ili kuhujumu mpango wa kidiplomasia".

    Soma zaidi:

  10. Vikosi vya Marekani vitasalia 'IRAN' hadi 'MAKUBALIANO HALISI' yatakapofikiwa - Trump

    .

    Chanzo cha picha, Kevin Lamarque / Reuters

    Rais wa Marekani Donald Trump ameandika ujumbe hivi karibuni kwenye jukwaa la mtandao wake wa Truth Social, akiionya Iran kwamba "'Ufyatuaji Risasi' Unaanza,' wa kiwango kikubwa, kwa njia bora zaidi, na wenye nguvu mno kuliko ambacho kimewahi kushuhudiwa na mwingine yeyote hapo awali" ikiwa "MAKUBALIANO HALISI" hayataafikiwa kikamilifu.

    Huu ndio ujumbe wake kamili:

    Meli zote za Marekani, Ndege, na Wanajeshi, pamoja na Risasi za ziada, Silaha, na kitu kingine chochote kinachofaa na muhimu kwa ajili ya kufunguliwa mashtaka ya kuua na kuangamiza Adui ambaye tayari amedhohofishwa vibaya, vitasalia ndani na karibu na Iran, hadi wakati ambapo MAKUBALIANO HALISI yataafikiwa na kutekelezwa kikamilifu. Ikiwa kwa sababu yoyote ile hayataafikiwa, jambo ambalo haliwezekani, basi "Ufyatuaji Risasi Unaanza," wa kiwango cha juu zaidi, bora zaidi, na wenye nguvu zaidi kuliko ambacho kimewahi kushuhudiwa na mwingine yeyote hapo awali. Ilikubaliwa, muda mrefu uliopita, na licha ya maneno yote ambayo yamekuwa kinyume chake - HAKUNA SILAHA ZA NYUKLIA na, Mlango wa Hormuz UTAFUNGULIWA NA UTAKUWA SALAMA. Wakati huo huo Jeshi letu kubwa litasalia huko, likitarajia, Ushindi unaofuata. MAREKANI IMEREJEA TENA!

    Trump anamaanisha nini kwa Iran kuafikia 'MAKUBALIANO HALISI'?

    Taarifa za kusitisha mapigano kwa wiki mbili kati ya Marekani na Iran zimekuwa zikikinzana.

    Kutokubaliana huko kunahusu vipengele vyenye kuzingatia masuala 10 mbadala ambayo yameibuka.

    Trump anasema "kuna kundi moja tu la "vipengele" vyenye maana vinavyokubalika na Marekani".

    Ameweka wazi anachotaka chini ya kile anachokiita makubaliano halisi: "HAKUNA SILAHA ZA NYUKLIA na, Mlango wa Hormuz UTAFUNGULIWA NA UTAKUWA SALAMA."

    Kumekuwa na matoleo kadhaa kutoka upande wa Iran.

    Vyombo vya habari vya serikali ya Iran vilifichua moja ya mipango yake uliojumuisha kukomesha mapigano nchini Iran, Iraq, Yemen na Lebanon, kufungua tena Mlango-Bahari wa Hormuz, na kujitolea kikamilifu kwa Marekani kuondoa vikwazo.

    Baadaye, mpango wa vipengele 10 wa Baraza Kuu la Usalama wa Taifa la Iran ulionekana kuongeza urutubishaji wa madini ya urani na kwa IRAN kuendelea kudhibiti Mlango-Bahari wa Hormuz.

    Madai kuhusu urutubishaji yaliondolewa baadaye kutoka kwa tafsiri ya Kiingereza ya taarifa ya Baraza la Usalama.

    Hakukuwa na kutajwa kwa usitishaji mapigano ikiwemo Lebanon katika ujumbe uliochapishwa na Trump, jambo ambalo pia limezua sintofahamu kuhusu masharti ya makubaliano ya usitishaji mapigano.

    Soma zaidi:

  11. Iran yaziambia meli jinsi ya kuepuka mabomu Baharini

    .

    Chanzo cha picha, Islamic Revolutionary Guard Corps

    Meli zinazopanga kupita katika Mlango-Bahari wa Hormuz zinapaswa kuchukua njia mbadala, ili "kuzingatia kanuni za usalama wa baharini na kulindwa kutokana na mashambulizi ya mabomu yanyaoweza kutokea baharini", Walinzi wa Mapinduzi wa Iran walisema katika taarifa iliyonukuliwa katika vyombo vya habari vya serikali ya Iran.

    Taarifa hiyo inaendelea kuelezea njia mbadala, pamoja na ramani ya kuwaelekeza. Meli zinazoingia kutoka Bahari ya Oman zinapaswa kusafiri kuelekea kaskazini mwa Kisiwa cha Larak, kisha kuendelea kuelekea Ghuba ya Uajemi.

    Meli zinazoelekea upande mwingine zinapaswa kutoka Ghuba ya Uajemi, kupita kusini mwa Kisiwa cha Larak na kuendelea kuelekea Bahari ya Oman.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Israel yafungua tena maeneo matakatifu ya Yerusalemu

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Polisi wa Israel wanasema maeneo matakatifu ya Yerusalemu yatafunguliwa tena kwa wageni na waumini kufuatia mpango wa muda wa kusitisha mapigano uliofikiwa katika mzozo wa Mashariki ya Kati.

    Maeneo hayo, ikiwa ni pamoja na eneo la msikiti wa Al-Aqsa, Ukuta wa Magharibi unaojulikana kama Western Wall, na Kanisa la Kaburi Takatifu, yote yakiwa kwenye Jiji la Kale, ni miongoni mwa maeneo matakatifu zaidi duniani katika Uislamu, Uyahudi na Ukristo.

    Kwa sababu ya vita dhidi ya Iran vilivyoanzishwa na Marekani na Israeli wiki sita zilizopita, maeneo hayo yamefungwa wakati wa sikukuu muhimu za kidini, ikiwa ni pamoja na wakati wa Pasaka huku idadi ndogo sana ya makasisi ikikubaliwa.

    Jiji la Kale, ambapo maeneo yake kwa kawaida huwa na shughuli nyingi za wakazi, wanaoenda sokoni, watalii na waumini, limekuwa kimya sana, huku wamiliki wengi wa maduka na vibanda wakishindwa kufungua kabisa.

    Polisi walisema kwamba maeneo matakatifu yatafunguliwa tena kuanzia Alhamisi asubuhi, huku mamia ya maafisa wengine wakipelekwa ili kuhakikisha usalama, na umma unahimizwa kuwa na subira ikiwa kutakuwa na msongamano.

    Pia unaweza kusoma:

  13. Trump asema, 'Nato haikuwepo tulipowahitaji'

    .

    Chanzo cha picha, Reuters

    Muda mfupi uliopita, Rais wa Marekani Donald Trump alichapisha kwenye mtandao wa Truth Social kwa mara ya kwanza tangu alipokutana na mkuu wa Nato Mark Rutte katika Ikulu ya White House.

    "NATO HAIKUWEPO TULIPOWAHITAJI, NA HAWATAKUWAPO IKIWA TUTAWAHITAJI TENA. KUMBUKA GREENLAND, KIPANDE KILE KIKUBWA CHA BARAFU, KINACHOSIMAMIWA VIBAYA!!!"

    Inaonekana Trump amerejelea lengo lake lililotajwa hapo awali la kujumuisha eneo la Denmark kuwa Marekani, hatua ambayo ilipingwa na washirika wengi wa Marekani katika Nato.

    Hapo awali Rutte aliiambia CNN kwamba mkutano wao ulikuwa wa kuambiana "ukweli", na kwamba anaamini "kabisa" kwamba dunia iko salama zaidi baada ya mashambulizi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran.

    Awali, Katibu Mkuu wa Nato, Mark Rutte alikutana na Donald Trump, na kuelezea mkutano wao kama wa kuambiana "ukweli" wenye uwazi, licha ya kutokubaliana.

    Rutte alikuwa Ikulu ya White House kwa zaidi ya saa mbili.

    Hata hivyo, kilicho wazi ni kwamba Trump bado ana mashaka makubwa kuhusu muungano huo na nchi wanachama ambazo anaamini hazikuisaidia Marekani vya kutosha kabla na wakati wa Operesheni ya Epic Fury iliyofanyika Iran.

    Uhusiano kati ya utawala na muungano wa Nato ulikuwa tayari katika hali mgumu kabla ya vita na Iran, hasa kutokana na kutokubaliana kuhusu mipango ya Trump kwa Greenland.

    Hata hivyo, mzozo nchini Iran umeongeza malalamiko ya Trump na Nato katika viwango vipya na kusababisha kile ambacho labda ni changamoto kubwa zaidi ambayo imekabiliana nayo katika historia yake.

    Soma zaidi:

  14. Israel yashambuliana na Hezbollah nchini Lebanon

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Ni zaidi ya saa 24 tangu Rais wa Marekani Donald Trump atangaze kusitisha mapigano kwa wiki mbili nchini Iran, jambo ambalo Israel, Iran na wapatanishi wa Pakistan walilithibitisha.

    Lakini tayari makubaliano ya amani yanaonyesha kuyumba.

    Israel imeanzisha wimbi kubwa la mashambulizi nchini Lebanon, na kuua watu wasiopungua 182.

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ameelezea mashambulizi hayo kama "pigo kubwa zaidi" kwa Hezbollah tangu kuanza kwa vita, akisema Israel itaanza tena kupigana na Iran kukiwa na haja ya "kufanya hivyo".

    Wakati huo huo, Iran imesema ikiwa mashambulizi nchini Lebanon hayatakoma mara moja huenda yakachochea "hatua kuchukuliwa".

    Siku ya Jumamosi, Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance atashiriki katika mazungumzo na Iran mjini Islamabad, Pakistan.

    Jambo la msingi litakuwa usafiri wa meli katika Mlango-Bahari wa Hormuz, njia ya baharini katika Ghuba ya Uajemi ambayo ni muhimu kwa usambazaji wa mafuta duniani.

    Iran imesema meli "zitalengwa na kuharibiwa" ikiwa zitapita bila ruhusa.

    Spika wa bunge la Iran pia anasema mambo matatu ya kusitisha mapigano kwenye mapendekezo yenye masuala 10 "yamekiukwa waziwazi", huku Vance akisema kila mara kuna "mapungufu" katika makubaliano kama hayo.

    Hezbollah yasema imeshambulia kaskazini mwa Israel

    Vile vile, Hezbollah imesema imerusha makombora kaskazini mwa Israeli.

    Wanamgambo hao wanaoungwa mkono na Iran wanasema ilikuwa ni kujibu ukiukwaji wa mapigano, katika taarifa iliyochapishwa kwenye mitandao ya kijamii.

    Pia wametishia kuendelea na mashambulizi hadi "uchokozi wa Israel na Marekani" dhidi ya Lebanon utakapokoma.

    Bado kuna kutokubaliana kuhusu kama nchi hiyo imejumuishwa katika usitishaji mapigano.

    Soma zaidi:

  15. Hujambo msomaji wetu. Karibu katika matangazo ya moja kwa moja ya tarehe 09/04/2026.