Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Wapiganaji wa Urusi kuondoka Burkina Faso, kuelekea Ukraine

Urusi inawaondoa maafisa wake 100 wa kijeshi kutoka Burkina Faso kusaidia katika vita nchini Ukraine.

Muhtasari

  • Mwanamume afungwa kwa njama aliompangia mkewe ili apewe hukumu ya kifo
  • DR Congo yatishia kujiondoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki
  • Rais wa Rwanda awafuta kazi zaidi ya wanajeshi 200
  • Thai: Wafanyikazi walionaswa chini ya njia ya treni wapatikana wamefariki
  • Rais wa Senegal aitaka Ulaya kusaidia kukabili ugaidi eneo la Sahel
  • Jeneza la kale la Misri laundwa upya baada ya miongo kadhaa
  • Harris atetea utendakazi wa White House katika mahojiano ya kwanza
  • Israel yakubali kusitisha mapigano kuruhusu utoaji wa chanjo ya polio
  • Ndege ya Ukraine F-16 yadunguliwa katika shambulizi la Urusi - BBC

Moja kwa moja

Asha Juma

  1. Mongolia inalazimika kumkamata Putin ikiwa atazuru nchini humo - ICC

    Maafisa wa Mongolia "wana wajibu" wa kumkamata Vladimir Putin ikiwa atazuru nchi hiyo wiki ijayo, Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) imesema.

    Safari hiyo, inayotarajiwa kufanyika Jumanne, itakuwa mara ya kwanza kwa kiongozi huyo wa Urusi kutembelea nchi wanachama wa ICC tangu mahakama hiyo iamuru akamatwe Machi 2023.

    Mahakama inadai Bw Putin anahusika na uhalifu wa kivita, ikisema alishindwa kuzuia ufurushwaji kinyume cha sheria wa watoto kutoka Ukraine hadi Urusi tangu mzozo huo uanze.

    Licha ya maafisa nchini Ukraine kutaka Mongolia wamkamate Bw Putin mara tu atakapowasili nchini humo, Kremlin ilisema "haina wasiwasi" kuhusu ziara hiyo.

    "Tuna uhusiano mzuri na washirika wetu kutoka Mongolia," msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov aliwaambia waandishi wa habari huko Moscow. "Bila shaka, vipengele vyote vya ziara ya Rais vimetayarishwa kwa makini." Dkt Fadi el-Abdallah, msemaji wa ICC, aliambia BBC siku ya Ijumaa kwamba mahakama hiyo inategemea Nchi Wanachama wake, ikiwa ni pamoja na Mongolia, "kutekeleza maamuzi yake".

    Alisema Mongolia, kama watia saini wengine wa ICC, ina "wajibu wa kushirikiana". Hii ni pamoja na kufuata vibali vya kukamatwa kama vile mahakama ilivyotoa kukamatwa kwa Bw Putin mnamo 2023.

    Mahakama hiyo ilidai kuwa rais wa Urusi anahusika na uhalifu wa kivita, ikilenga kuwafukuza kinyume cha sheria watoto kutoka Ukraine hadi Urusi.

    Pia imetoa kibali cha kukamatwa kwa kamishna wa haki za watoto wa Urusi, Maria Lvova-Belova, kwa uhalifu huohuo.

    Ilisema uhalifu huo ulifanyika nchini Ukraine kuanzia tarehe 24 Februari 2022, wakati Urusi ilipoanzisha uvamizi wake.

    Hapo awali Moscow ilikanusha madai hayo na kutaja hati hizo kuwa za "kuudhi". Dk Abdallah alisema majaji wa ICC watachunguza kesi za "kutoshirikiana" na watia saini wake na kuliarifu Bunge la Nchi Wanachama, ambalo linaweza "kuchukua hatua yoyote inayoona inafaa".

    ICC haina mamlaka ya kuwakamata washukiwa, na inaweza tu kutumia mamlaka ndani ya nchi wanachama wake.

  2. Wapiganaji wa Urusi kuondoka Burkina Faso, kuelekea Ukraine

    Urusi inawaondoa maafisa wake 100 wa kijeshi kutoka Burkina Faso kusaidia katika vita nchini Ukraine.

    Wao ni sehemu ya wanajeshi wapatao 300 kutoka Bear Brigade - kampuni ya kijeshi ya binafsi ya Urusi, ambao waliwasili katika taifa hilo la Afrika Magharibi mwezi Mei kusaidia jeshi la kijeshi la nchi hiyo.

    Katika chaneli yake ya Telegram, kundi hilo lilisema vikosi vyake vitarejea nyumbani kusaidia ulinzi wa Urusi dhidi ya mashambulizi ya hivi karibuni ya Ukraine katika eneo la Kursk.

    Kuna hofu kwamba kujiondoa kunaweza kuwatia moyo wapiganaji wa Kiislamu nchini Burkina Faso, ambao hivi karibuni waliwaua hadi watu 300 katika moja ya mashambulizi makubwa kuwahi kutokea katika miaka ya hivi karibuni.

    Burkina Faso tangu mwaka 2015 imekuwa ikikabiliwa na mashambulizi ya mara kwa mara ya wanajihadi, huku zaidi ya watu milioni mbili wakilazimika kuyahama makazi yao katika kile ambacho mashirika ya misaada yanaita janga "lililopuuzwa zaidi" duniani.

    Kikosi cha kijeshi chini ya Rais wa mpito Kapteni Ibrahim Traoré, ambaye aliingia madarakani kwa mapinduzi mnamo Septemba 2022, aliahidi kumaliza mashambulizi lakini amejitahidi, hata baada ya kutafuta ushirikiano mpya wa usalama na Urusi.

    Huku karibu nusu ya nchi ikiwa nje ya udhibiti wa serikali, makundi ya wanajihadi yanazidi kuwalenga raia na vitengo vya kijeshi.

    Walionusurika wanasema takribani watu 300 waliuawa siku ya Jumamosi katika mji wa kaskazini wa Barsalogho, katika shambulio ambalo lilidaiwa na kundi la wanamgambo wenye mafungamano na al-Qaeda, Jamaat Nusrat al-Islam wal-Muslimin (JNIM).

    Wanaripotiwa kuwa raia na wanajeshi wakisaidia kuchimba mitaro kusaidia kulinda mji dhidi ya mashambulizi ya wanajihadi.

    Mamlaka haijasema ni watu wangapi waliuawa lakini Waziri wa Mawasiliano Rimtalba Jean Emmanuel Ouedraogo aliliita shambulizi hilo kuwa la kinyama.

  3. Mgonjwa wa tatu mwenye maradhi ya Homa ya Nyani agunduliwa Kenya

    Wizara ya Afya imethibitisha kuwepo mgonjwa wa tatu wa Homa ya Nyani {Mpox} nchini, huku mgonjwa wa kike mwenye umri wa miaka 30 jijini Nairobi akipimwa na kukutwa na maradhi hayo .

    Mkurugenzi Mkuu wa Afya Dk.Patrick Amoth amesema kuwa mgonjwa, huyo ambaye ana historia ya kusafiri kuelekea Uganda hivi karibuni , kwa sasa yuko katika hali nzuri na anapatiwa matibabu katika sehemu aliyotengwa katika mji mkuu.

    Kisa hiki cha hivi punde kinafanya jumla ya watu waliothibitishwa kuwa na Mpox nchini Kenya kufikia watatu, baada ya wagonjwa wengine kugunduliwa katika kaunti za Taita Taveta na Busia.

    Hadi sasa, Wizara imepima jumla ya sampuli 89 za Mpox, huku 79 zikiwa hazina huku saba zikiwa zinaendelea kufanyiwa uchunguzi.

    Dkt. Amoth amesisitiza kuwa Wizara imekuwa ikifuatilia kwa karibu hali hiyo na imeongeza kwamba juhudi za kudhibiti kuenea kwa ugonjwa huo zinaendelea.

    Ufuatiliaji unaoendelea unajumuisha ukaguzi wa wasafiri katika Bandari maalumu za kuingia nchini, na zaidi ya watu 582,000 wamekaguliwa kufikia sasa.

    Wizara ya Afya inawataka wananchi kuwa watulivu, ikihakikisha kuwa mfumo wa huduma za afya umejipanga kikamilifu kukabiliana na ugonjwa huo.

    “Tunapenda kuwahakikishia wananchi kuwa vituo vyetu vya kutolea huduma za afya vimejiandaa kikamilifu kupima na kudhibiti ugonjwa huu na hakuna haja ya kuwa na hofu... Tunaendelea kujitolea kulinda afya na ustawi wa wananchi wote na tutaendelea kukabiliana na maradhi hayo," alisema Dk Amoth.

    Unaweza kusoma;

  4. Mtekaji nyara wa Kiitaliano aliyetoroka akamatwa nchini Argentina

    Polisi mjini Buenos Aires wamemkamata mwanaume aliyesakwa kwa miongo kadhaa nchini Italia kwa utekaji nyara unaotekelezwa na kundi la wanamgambo wa mrengo mkali wa kushoto la Red Brigades.

    Leonardo Bertulazzi, ambaye kwa miaka mingi alikuwa mkimbizi nchini Argentina, anakabiliwa na kifungo cha miaka 27 jela nchini Italia baada ya takribani miaka 44 ya kutoroka.

    Sasa akiwa na umri wa miaka 72, Bertulazzi alihukumiwa akiwa hayupo nchini Italia katika miaka ya 1970 kwa kumteka nyara Pietro Costa, mhandisi wa jeshi la maji kutoka kwenye familia tajiri inayomiliki meli huko Genoa.

    Alikamatwa kwa mara ya kwanza na polisi wa Buenos Aires mwaka 2002, baada ya kuripotiwa kuingia nchini kutoka Chile kwa hati ya kusafiria ya uongo, lakini aliachiliwa miezi michache baadaye na kurejeshwa kwake kulizuiwa.

    Leonardo Bertulazzi alipewa hadhi ya ukimbizi miaka miwili baadaye lakini hilo lilibatilishwa wakati rais wa mrengo wa kulia wa Argentina, Javier Milei, alipoingia madarakani.

    "Bertulazzi anahusika na uhalifu ambao ulidhoofisha maadili ya kidemokrasia na maisha ya waathirika wengi," ilisema taarifa kutoka kwenye serikali huko Buenos Aires.

    Red Brigades lilikuwa kundi la wapiganaji wa Kimaksi ambao waliwateka nyara na kuwaua maafisa kadhaa wa serikali katika miaka ya 1970 na 80, akiwemo waziri mkuu wa zamani, Aldo Moro.

    Kipindi hicho cha vurugu za kisiasa kilijulikana kama "Miaka ya Uongozi" kwa sababu ya mlolongo wa uhalifu wa mrengo wa kushoto na wa kulia.

  5. Nyumba zabomolewa Timor-Mashariki kabla ya ziara ya Papa Francis

    Nyumba za familia zinabomolewa karibu na Dili, mji mkuu wa Timor-Mashariki, katika eneo ambalo Papa Francis ataadhimisha misa mwezi ujao.

    TakribanI watu 90 wameambiwa na serikali kwamba lazima watafute mahali pengine pa kuishi kabla hajafika, kulingana na wakazi waliofukuzwa waliozungumza na BBC.

    Serikali ya nchi hiyo inakanusha kuwa kuondolewa kunahusishwa na ziara ya Papa, ikisisitiza kuwa wakazi hao wanaishi huko kinyume cha sheria.

    Mamlaka zimetumia takribani $18m (£13.6m) katika ziara ya siku tatu ya papa, itakayoanza tarehe 9 Septemba.

    "Tuna huzuni sana," Zerita Correia, mkazi wa eneo hilo, aliiambia BBC News. "Hata walibomoa vitu vyetu ndani ya nyumba. Sasa inabidi tupange karibu kwa sababu watoto wangu bado wako shuleni katika eneo hili," aliongeza.

    Msemaji wa wakazi hao alisema kuwa familia 11 zitakuwa zimehamishwa kabla ya Papa Francis kuwasili Timor-Mashariki.

    Serikali imewalipa kati ya $7,000 na $10,000 kwa ajili ya nyumba zao. "Kiasi hicho hakitoshi kwa kila kaya kukidhi mahitaji yake," alisema Venancio Ximenes, akizungumza na BBC.

    “Hatua inayofuata ya kufukuzwa itakuja baada ya Papa Francis kuondoka na hiyo itahusisha zaidi ya familia 1,300,” aliongeza.

    Nyumba hizo ziko Tasitolu, eneo oevu nje kidogo ya Dili. Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, mamia ya watu walihamia huko kutoka sehemu za vijijini.

    Wengi walikuja kutafuta kazi katika mji mkuu na kujenga nyumba katika eneo hilo. Serikali inasema wanachuchumaa na hawana haki ya kuishi kwenye ardhi hiyo.

  6. Israel yasema kiongozi wa Hamas aliuawa siku ya tatu ya operesheni Ukingo wa Magharibi

    Jeshi la Israel limesema limemuua mkuu wa kundi la wapiganaji la Palestina Hamas huko Jenin na wapiganaji wengine wawili, huku operesheni kubwa ikiendelea kwa siku ya tatu kaskazini mwa Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu.

    Vikosi vya usalama vya Israel "vilikutana na kumuondoa" Wissam Hazem kwenye gari na kisha kufanya mashambulizi ya anga dhidi ya "magaidi wawili walipokuwa wakijaribu kukimbia", taarifa ilisema.

    Wizara ya afya ya Palestina ilisema watu hao watatu waliuawa usiku karibu na mji wa Zababdeh, kusini-mashariki mwa Jenin. Vyombo vya habari vya Palestina pia vimeripoti kuwa wanajeshi wa Israel wameondoka Tulkarm baada ya kusababisha uharibifu mkubwa wa majengo na miundombinu katika kambi za wakimbizi za mji huo.

    Hakukuwa na kauli yoyote kutoka kwa jeshi la Israel, ambalo lilisema Alhamisi kuwa limewaua wafuasi watano wa vikundi vyenye silaha huko Tulkarm, akiwemo kiongozi wao wa eneo hilo.

    Jeshi lilitangaza, hata hivyo, kwamba vikosi viliondoka kwenye kambi ya wakimbizi ya al-Faraa karibu na Tubas baada ya kukamilisha kile ilichokiita "lengo la kuzuia ugaidi, kufichua miundombinu ya kigaidi na kuwaangamiza magaidi wenye silaha".

    Takribani Wapalestina 19 wameuawa tangu kuanza kwa operesheni ya Israel, ambayo ni moja kati ya operesheni kubwa zaidi katika Ukingo wa Magharibi katika miongo miwili, kulingana na wizara ya afya ya Palestina.

    Unaweza kusoma;

  7. Mawaziri wa Ulinzi wa EU wajadili utoaji wa silaha, mifumo ya ulinzi wa anga kwa Ukraine

    Mawaziri wa ulinzi wa Umoja wa Ulaya wanakutana mjini Brussels kujadili kuharakisha usambazaji wa mifumo ya ulinzi wa anga iliyoahidiwa hapo awali kwa Ukraine, mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell alisema.

    Kama ilivyoripotiwa na shirika la Ukrinform, alitoa maoni yake juu ya taarifa za jana na mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Ukraine, Dmytro Kuleba, ambaye wakati wa mazungumzo huko Brussels alilalamika kuhusu uwasilishaji polepole wa risasi na silaha nyingine kwa Vikosi vya Wanajeshi vya Ukraine, vilivyoahidiwa na washirika wa Magharibi.

    "Ahadi nyingi zimetolewa tangu Juni mwaka huu, hasa katika eneo la ulinzi wa anga. Kwa kuzingatia mashambulizi makubwa ya miji ya Ukraine, ambayo yamekuwa mashambulizi makubwa zaidi dhidi ya raia, ni wazi kwamba lazima tujibu," Borrell alisema.

    "Tutaangalia masuala haya yote, ambapo sasa tuko katika kutimiza wajibu wetu. Ni wazi, ikiwa Waukraine wana msaada huo, wanaweza kupigana kwa mafanikio," Borrell alisema.

    Aliongeza kuwa "operesheni katika eneo la Kursk ni mfano mzuri wa hili." "Hii ni hatua ya kimkakati ya kuamua na yenye mafanikio ambayo inaonesha kuwa wako tayari kupigana na kuendelea kupigana wakati wana msaada wa nyenzo ambao unategemea sisi,"

    Mikutano isiyo rasmi ya mawaziri wa mambo ya nje na ulinzi wa Umoja wa Ulaya inafanyika mjini Brussels, ingawa ilipaswa kufanyika nchini Hungary, ambayo kwa sasa inashikilia urais wa zamu wa EU.

    Uamuzi huo ulifanywa kuahirisha mikutano hiyo kutokana na nafasi ya Waziri Mkuu wa Hungary, Viktor Orban, ambaye alikwenda Moscow kwa mazungumzo na Vladimir Putin.

    Unaweza kusoma;

  8. Mwanamume afungwa kwa njama aliompangia mkewe ili apewe hukumu ya kifo

    Mwanamume mmoja nchini Singapore ambaye alijaribu kumpangia njama mke wake waliyeachana, kwa kuweka bangi kwenye gari lake amehukumiwa kifungo cha karibu miaka minne jela.

    Tan Xianglong, 37, aliweka kile alichofikiri ni zaidi ya nusu kilo ya bangi kati ya viti vya nyuma vya gari la mwanamke huyo, akidhani ilitosha kutoa hukumu ya kifo kwa kosa la ulanguzi wa dawa za kulevya.

    Singapore ina baadhi ya sheria kali zaidi duniani za kupambana na dawa za kulevya, ambazo serikali inasema ni muhimu kuzuia uhalifu unaohusiana na dawa za kulevya.

    Chini ya nusu ya kile kilichowekwa na Tan iligeuka kuwa bangi.

    Tan "alinuia kumweka matatani aliyekuwa mke wake na sheria," kulingana na hati za mahakama.

    "Alielewa kuwa mhusika angekamatwa kimakosa na kushtakiwa kwa uhalifu mkubwa ikiwa mpango wake utafaulu."

    Alihukumiwa siku ya Alhamisi kifungo cha miaka mitatu na miezi 10 jela kwa kupatikana na bangi.

    Mahakama pia ilizingatia shtaka la pili la kuweka ushahidi kinyume cha sheria.

    Tan na mkewe walifunga ndoa mnamo mwaka 2021 na kutengana mwaka mmoja baadaye.

    Hawakuweza kuwasilisha talaka kwa sababu Singapore inaruhusu talaka kwa wenzi tu ambao wameoana kwa takriban miaka mitatu.

    Tan aliamini kuwa anaweza kuondolewa sheria hiyo ikiwa mke wake alikuwa na rekodi ya uhalifu.

    Katika mazungumzo ya jukwaa la Telegram na mpenzi wake mwaka jana, alisema alikuwa ameanzisha "uhalifu usioepukika" kumsingizia mke wake.

    Soma zaidi:

  9. DR Congo yatishia kujiondoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki

    Jamhuri ya Kidemokrasi a Kongo imetishia kujiondoa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) iwapo jumuiya hiyo itashindwa kuiwajibisha Rwanda kwa madai ya unyanyasaji katika eneo la Mashariki lililokumbwa na ghasia.

    Tishio hilo lilitolewa baada ya Mahakama ya Haki ya EAC kuripotiwa kukubali kuanza kesi dhidi ya Rwanda kuhusu kuhusika kwake na ghasia mashariki mwa DR Congo.

    Naibu Waziri wa Sheria wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Samuel Mbemba aliutaja kuwa "ushindi wa mahakama kwa nchi yetu".

    Mbemba pia aliitaka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kuanzisha uchunguzi kuhusu madai ya ukatili wa Rwanda mashariki mwa DR Congo.

    Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo limekuwa likipambana na kundi la waasi la M23 - linalodaiwa kuuungwa mkono na Rwanda.

    Taifa hilo la Afrika Mashariki limekuwa likipinga madai hayo ya Congo.

    Soma pia:

  10. Rais wa Rwanda awafuta kazi zaidi ya wanajeshi 200

    Rais wa Rwanda Paul Kagame amewafuta kazi takriban wanajeshi 214 wakiwemo maafisa kadhaa wakuu wa kijeshi.

    Taarifa fupi ya Wizara ya Ulinzi ya Rwanda, iliyowekwa kwenye ukurasa wake rasmi wa X asubuhi ya leo, ilisema kuwa maafisa waliofutwa kazi ni pamoja na Meja Jenerali Martin Nzaramba na Kanali Dkt Etienne Uwimana.

    "Pia ameidhinisha kufutwa na kubatilishwa kwa maafisa 195 wa vyeo vingine vya Jeshi la Ulinzi la Rwanda," ilisema taarifa hiyo.

    Hakuna sababu iliyotolewa kwa hatua hiyo, lakini ilitangazwa saa chache baada ya Kagame kukutana na maafisa wakuu wa kijeshi, akiwemo Mkuu wa Majeshi Jenerali Mubarakh Muganga.

    Tovuti inayounga mkono serikali ya New Times, iliripoti kwamba Kagame na maafisa wa kijeshi walijadili vipaumbele vya amani na usalama vya Rwanda.

    Pia unaweza kusoma:

  11. Thai: Wafanyikazi walionaswa chini ya njia ya treni wapatikana wamefariki

    Wafanyakazi watatu raia wa kigeni waliokuwa wamekwama chini ya njia ya treni iliyoporomoka wamefariki dunia licha ya juhudi za uokoaji zilizodumu kwa muda wa siku tano, mamlaka ya Thailand imesema.

    Wanaume hao, wawili kutoka China na mmoja kutoka Myanmar, bado walidhaniwa kuwa hai hadi siku ya Alhamisi.

    Walinaswa chini ya njia ya treni waliyokuwa wakijenga ilipoporomoka siku ya Jumamosi katika wilaya ya Pak Chong, yapata kilomita 200 kaskazini-mashariki mwa mji mkuu Bangkok.

    Siku ya Ijumaa, mamlaka ilitangaza kwamba wote watatu walikuwa wamefarikidunia, huku uchunguzi wa awali ukionyesha kuwa hii ilitokana na ukosefu wa hewa.

    Njia ya treni iliyokuwa inajengwa ni sehemu ya mradi wa reli ya kasi ya Thailand-China, ilioporomoka kutokana na maporomoko ya ardhi mwendo wa saa 23:40 kwa saa za nchini humo Jumamosi iliyopita.

    Waokoaji, wanaojumuisha maafisa kutoka Shirika la Reli la Thailand na timu ya kukabiliana na maafa ya China, walikuwa wakifanya kazi usiku kucha kwa wiki nzima kwa matumaini ya kuwaokoa waathiriwa.

    Walikuwa wamejaribu kusukuma oksijeni kwenye njia ilioporomoka ili kuwasaidia wafanyikazi kuwa hai, lakini haijulikani ikiwa mirija waliyotumia iliwafikia wafanyikazi hao hata kidogo.

    Siku ya Alhamisi, waokoaji walipata mwili wa dereva wa lori raia wa Myanmar ukiwa umezikwa chini ya rundo la udongo na mawe.

    Miili ya wafanyikazi wawili wa Kichina, msimamizi na mchimbaji, ilipatikana karibu 06:00 saa za eneo siku ya Ijumaa, Shirika la reli lilisema.

    Miili yote mitatu ilipatikana takriban mita 25 kutoka mahali ambapo njia hiyo iliporomoka, maafisa waliongeza.

    Vichanganuzi na mbwa wa kunusa pia walikuwa wamegundua ishara muhimu, ikiwa ni pamoja na mapigo ya moyo, na kutoa matumaini kwamba wafanyakazi hao bado wangali hai.

  12. Rais wa Senegal aitaka Ulaya kusaidia kukabili ugaidi eneo la Sahel

    Rais wa Senegal, Bassirou Diomaye Faye ameitaka Ulaya kusaidia kukabiliana na tishio la usalama linaloongezeka huko Sahel, eneo tete ambalo limekabiliwa na mfululizo wa mashambulizi mabaya katika siku chache zilizopita.

    Ametoa wito huo wakati wa mkutano na waandishi wa habari akiwa na Waziri Mkuu wa Uhispania Pedro Sanchez, ambaye alikuwa anamaliza ziara yake Afrika Magharibi.

    "Hali katika eneo la Sahel inataka uhamasishaji wa kimataifa wa jumuiya ya kimataifa," alisema Rais Faye, ambaye pia anahudumu kama mwezeshaji katika juhudi za ECOWAS kurejesha Mali, Niger, na Burkina Faso katika umoja huo. Alisisitiza haja ya Ulaya kuzidisha uungaji mkono wake kwa Sahel, ikizingatiwa kwamba "Afrika na Ulaya zina hatima iliyounganishwa ya usalama."

    Ombi lake linawadia siku chache baada ya Burkina Faso kushuhudia moja ya mashambulizi yake mabaya zaidi.

    Makumi ya raia na vikosi vya usalama waliuawa na wanamgambo katika eneo la Kaskazini la Barsalogho mnamo Agosti 24.

    Kundi la wanajihadi lenye uhusiano na Al-Qaeda, Jama'at Nusrat al-Islam wal-Muslimin (JNIM) lilidai kuhusika na shambulio hilo la kikatili, ripoti zikidokeza kuwa watu 200 waliuawa kwa jumla wakati wakichimba mitaro ili kulinda kijiji chao dhidi ya wanamgambo.

    Mamlaka za Burkina Faso, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, EU, Marekani na hata ECOWAS walilaani shambulio hilo.

    Bado haifahamiki jinsi Burkina Faso, Mali, na Niger zitatafsiri wito wa kiongozi wa Senegal wa kuingilia kati kwa Ulaya katika mgogoro wa Sahel, kwani walivunja uhusiano na vikosi vya Magharibi na kuwaamuru watoke katika eneo hilo hilo la Sahel wakati bado hali ikiwa tete.

    Nchi hizo tatu ziliunda muungano wa kijeshi ili kukabiliana na uasi na kuendelea kuwa na uhusisano wa kiusalama na Urusi ambayo huwapa silaha na wale inaowaita kama "wakufunzi wa kijeshi."

    Soma zaidi:

  13. Jeneza la kale la Misri laundwa upya baada ya miongo kadhaa

    Jeneza la kale la Misri limeundwa upya baada ya kuhuishwa kwa miongo kadhaa.

    Ubunifu huo unaoaminika kuwa wa mwaka 650 KK, sasa umerejeshwa tena katika Chuo Kikuu cha Swanseacha Misri baada ya kuundwa upya kwa saa elfu kadhaa katika Chuo Kikuu cha Cardiff.

    Jeneza, ambalo awali lilitengenezwa kwa ajili ya mtu anayeitwa Ankhpakhered katika mji wa Thebes nchini Ugiriki, lilisafirishwa na kurudishwa chini ya uangalizi wa mtunza wa kituo hicho Dk Ken Griffin.

    Wafanyikazi walielezea kazi hio iliyomalizika kama "zaidi ya ndoto".

    Dk Griffin alisema: "Jeneza lilipaswa kusafishwa kwa uangalifu, kujengwa upya na kuunganishwa ili kuzuia kuharibika zaidi na tunafurahi kuwa tuko nayo tena.

    "Tulipewa zawadi na Chuo Kikuu cha Aberystwyth mnamo 1997 lakini maelezo juu ya historia yake ni kidogo sana.

    Pia unaweza kusoma:

  14. Harris atetea utendakazi wa White House katika mahojiano ya kwanza

    Makamu wa Rais wa Marekani Kamala Harris alitetea mabadiliko yake ya sera, Rais Joe Biden, na muda wake katika Ikulu ya White House katika mahojiano yake ya kwanza tangu kuwa mgombea wa chama cha Democratic.

    Bi Harris alisema kuwa utawala wa Biden uliweza "kuokoa uchumi" baada ya janga hilo na umepunguza uhamiaji haramu katika miezi ya hivi karibuni.

    Aliziita sera za Ikulu ya Marekani "mafanikio", akiashiria kupungua kwa gharama za dawa na kiwango cha ukosefu wa ajira: "Hiyo ni hatua nzuri. Kuna nafasi ya kufanya vizuri zaidi."

    Bi Harris alionekana kwenye mahojiano yaliyorekodiwa ya CNN na mgombea mwenza wake, Gavana wa Minnesota Tim Walz. Ilikuwa ni mara yake ya kwanza kama kufanya mahojiano ya aina hiyo kama mgombea urais.

    Makamu huyo wa rais alilazimika kutetea rekodi ya uchumi ya Ikulu ya Marekani, huku mfumuko wa bei na gharama ya juu ya maisha ikiendelea kuumiza vichwa Wamarekani.

    Kura za maoni zimependekeza mara kwa mara kwamba wapiga kura wangependelea mgombea wa Republican Donald Trump kushughulikia suala la uchumi.

    Lakini majibizano makali zaidi kati ya Bi Harris na mwandishi wa CNN Dana Bash yalijikita katika madai kwamba nafasi za sera za mgombeaji huyo wa Demokratic "zimebadilika" wakati akiwa makamu wa rais na sasa kama mgombeaji wa urais.

    Maelezo zaidi:

  15. Israel yakubali kusitisha mapigano kuruhusu utoaji wa chanjo ya polio

    Israel imekubali "kusitisha mapigano" huko Gaza ili kuruhusu utoaji wa chanjo ya watoto dhidi ya polio, Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema.

    Kampeni hiyo italenga kutoa chanjo kwa watoto 640,000 kote katika ukanda wa Gaza na itaanza Jumapili, afisa mkuu wa WHO Rik Peeperkorn alisema.

    Itatolewa katika hatua tatu tofauti, sehemu za kati, kusini na kaskazini za ukanda huo.

    Katika kila hatua, mapigano yatasitishwa kwa siku tatu mfululizo kati ya 06:00 na 15:00 saa za eneo hilo.

    Makubaliano hayo yanafikiwa siku chache tu baada ya maafisa wa Umoja wa Mataifa kusema mtoto wa miezi 10 alikuwa amepooza kwa kiasi fulani baada ya kisa cha kwanza cha maambukizi ya polio huko Gaza katika kipindi cha miaka 25.

    Takriban dozi milioni 1.26 za chanjo ya polio yenye kutolewa kwenye mdomo aina ya 2 (nOPV2) tayari iko Gaza, na dozi 400,000 za ziada zinatarajiwa kuwasili hivi karibuni.

    Kampeni hiyo itasimamiwa na "Wizara ya Afya ya Palestina, kwa ushirikiano na WHO, UNICEF, UNRWA".

    Zaidi ya wafanyakazi 2,000 wa afya na jamii wamefunzwa namna ya kutoa chanjo hiyo.

    WHO inalenga kufikia 90% ya wale watakaochajwa katika eneo lote, kiwango kinachohitajika kukomesha maambukizi ya virusi ndani ya Gaza.

    Makubaliano yanafanywa kwa siku ya nne ya ziada ya utoaji chanjo na ikiwa kutakuwa na haja ya kufanya hivyo kufikia kiwango cha chanjo kinacholengwa.

    Virusi vya polio huambukiza sana na mara nyingi huenezwa kupitia maji taka na maji machafu.

    Soma zaidi:

  16. Ndege ya Ukraine F-16 yadunguliwa katika shambulizi la Urusi - BBC

    Moja ya ndege za kivita za F-16 zilizotolewa na washirika wa Nato kwa Ukraine imedunguliwa, chanzo cha kijeshi cha Ukraine kimeiambia BBC.

    Ndege hiyo ilianguka katikati ya msururu wa mashambulizi ya makombora ya Urusi siku ya Jumatatu, na kumuua rubani Oleksiy Mes, jeshi la Ukraine lilisema.

    Tukio hilo ni hasara ya kwanza ya aina yake tangu ndege hizo ziwasilishwe mapema mwezi huu.

    Sababu ya ajali hiyo haikuwa matokeo ya moja kwa moja ya shambulio la kombora la adui, jeshi la Ukraine linadai.

    Ilisema rubani alitungua makombora matatu ya cruise na droni moja katika shambulio kubwa zaidi la anga la Urusi kufikia sasa.

    "Oleksiy aliwaokoa raia wa Ukraine kutoka kwa makombora hatari ya Urusi," Jeshi la Wanahewa la Ukraine liliandika katika taarifa kwenye mtandao wa kijamii. "Kwa bahati mbaya, ilimgaharimu maisha yake mwenyewe."

    Taarifa hiyo haikubainisha aina ya ndege iliyohusika, lakini chanzo cha kijeshi kiliiambia BBC kuwa rubani alikuwa akiendesha F-16.

    Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alithibitisha rasmi Jumanne kwamba ndege za F-16 zinazotengenezwa Marekani zinatumwa kutungua ndege zisizo na rubani na makombora ya Urusi.

    Wiki hii, aliomba washirika kuruhusu Ukraine kutumia makombora ya masafa marefu kulenga shabaha zaidi hadi Urusi.

    Hakutakuwa na vizuizi kwa matumizi ya ndege hizo mbali na kuzingatia sheria za kibinadamu, aliuambia mkutano huko Washington siku ya Jumatano - akimaanisha kwamba Kyiv inaweza kuanzisha mashambulizi zaidi katika eneo la Urusi.

    Soma zaidi:

  17. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya kila siku ikiwa ni tarehe 30/08/2024