Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Erdogan aiita Israel "shirika la kigaidi la Kiyahudi"

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdoğan katika ukosoaji wake wa mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon na Gaza ameitaja nchi hii kuwa ni "shirika la kigaidi la Kiyahudi".

Muhtasari

  • Maseneta Kenya waaswa kutokuwa na upendeleo katika kuamua suala la Gachagua
  • Wanne mbaroni Tanzania kwa kumuua mume wa mdaiwa mkopo
  • Erdogan aiita Israel "shirika la kigaidi la Kiyahudi"
  • Mapigano yaendelea Gaza, idadi ya waliouawa yafikia 42,000
  • Israel yasema imeshambulia maeneo 185 ya Hezbollah katika saa 24 zilizopita
  • Bunge la Seneti Kenya kusikiliza mashtaka dhidi ya Naibu wa rais Gachagua leo
  • Hezbollah inasema iliwarudisha nyuma wanajeshi wa Israel kwenye mpaka
  • Msumbiji yafanya uchaguzi huku chama tawala kikitarajiwa kudumisha uongozi
  • Brazil yaondoa marufuku dhidi ya X baada ya kampuni hiyo kulipa faini ya dollar milioni 5
  • Raia wa Afghanistan akamatwa kwa madai ya njama ya shambulizi siku ya uchaguzi wa Marekani
  • Urusi inadhamiria kusababisha ghasia katika maeneo ya Uingereza, inaonya MI5
  • Jimbo la Florida Marekani lajitayarisha kukabiliana na kimbunga Milton

Moja kwa moja

Na Asha Juma

  1. Cameroon yasisitiza kuwa rais yuko vizuri licha ya kutoonekana hadharani

    Rais wa Cameroon yuko katika hali "nzuri", maafisa wakuu wamesisitiza baada ya kutokuwepo kwa muda mrefu kulilokozua uvumi ulioenea kuhusu hali ya kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 91.

    Rais Paul Biya hajaonekana hadharani tangu tarehe 8 Septemba, alipohudhuria kongamano la China na Afrika mjini Beijing.

    Tangu wakati huo amekosa matukio ambayo ilipangwa awepo, kama vile Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa huko New York.

    Lakini katika taarifa yake, mkuu wa baraza la mawaziri la kiraia la Cameroon alisema Biya yuko vizuri na kulaani "watu waovu" wanaokisia kuhusu afya ya rais na "kifo".

    Kauli hiyo imekuja baada ya siku kadhaa za vyama vya upinzani na mashirika ya kiraia kutaka taarifa kuhusu afya ya Biya na mahali alipo.

  2. Tunachojua kufikia sasa kuhusu mgogoro kati ya Hezbollah na Israel

    Waisrael wawili waliuawa wakati wa shambulio la roketi kwenye mji wa mpaka wa Kiryat Shmona, Hezbollah ilisema ilirusha makombora katika eneo hilo.

    Mapigano yameripotiwa na Israel na Hezbollah mpakani. Hezbollah inasema iliirudisha nyuma IDF magharibi mwa Lebanon.

    IDF ilisema asubuhi ya leo kuwa imepiga maeneo 185 ya Hezbollah katika saa 24 zilizopita. Milipuko imeonekana karibu na Tiro na katika eneo la Khiam.

    Umoja wa Mataifa unasema robo ya eneo la Lebanon iko chini ya amri ya kuhamishwa, na watu waliokimbia makazi yao wanaishi mitaani na fukwe za Beirut.

    Simu ya Biden-Netanyahu: Rais wa Marekani Biden na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu wanatarajiwa kuzungumza na baadaye leo.

    Mapigano ya Gaza: Huko Gaza, vikosi vya Israeli vinapigana huko Jabalia, na wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas ilitangaza kuwa idadi ya vifo imepita 42,000 katika mwaka uliopita, na 45 waliuawa katika saa 24 zilizopita.

    Unaweza kusoma;

  3. Maseneta Kenya waaswa kutokuwa na upendeleo katika kuamua suala la Gachagua

    Kuondolewa kwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kunawapa maseneta fursa ya kuonesha uaminifu wao kwa Katiba, Spika wa Seneti Amason Kingi amesema.

    Katika ujumbe wake kwa Bunge, Kingi alisema hoja ya kumwondoa madarakani ni ya kipekee na haijawahi kutokea kwani ni ya kwanza kabisa nchini kupendekeza kuondolewa kwa Naibu Rais.

    "Wakati huu unahitaji kutafakari kwa kina juu ya jukumu muhimu la Seneti katika kuchunguza kuondolewa kwa maafisa wa serikali," alisema.

    Alibainisha kuwa mchakato wa kumfungulia mashtaka ni chombo cha msingi cha uangalizi wa kisheria na chombo muhimu kuhakikisha kuwa katiba inafuatwa.

    Kingi aliendelea kubainisha kuwa Bunge la Seneti limepewa dhamana na Katiba kuketi na kuchunguza pendekezo lolote la kuondolewa ofisini kwa kuondolewa kwa Rais, Naibu Rais, magavana wa kaunti na naibu magavana wa kaunti.

    "Hii ni fursa nyingine kwa seneti kuonesha uaminifu wake kwa Katiba na kuishi kulingana na sifa yake," Kingi aliongeza. Alisema Seneti, kama baraza la kesi, lazima idumishe uadilifu na kutoegemea upande wowote katika usimamizi wa haki.

    Unaweza kusoma;

  4. Wanne mbaroni Tanzania kwa kumuua mume wa mdaiwa mkopo

    Jeshi la polisi nchini Tanzania linawashikilia wafanyakazi wanne wa kampuni ya kutoa mikopo ya kifedha ya OYA kwa tuhuma za mauaji ya Juma Mfaume kwa kumshambulia sehemu mbalimbali za mwili mume wa mdaiwa wa mkopo.

    Taarifa ya Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani, Muhudhwari Msuya inasema tukio hilo limetokea Jumatatu katika wilaya ya kipolisi Mlandizi ambapo wafanyakazi hao walifika nyumbani hapo kwa lengo la kudai fedha za marejesho ya mkopo kwa mke wa Mfaume.

    Kwa mujibu wa polisi, baada ya kufika nyumbani kwa Mfaume aliwaelekeza kuwa mkewe hakuwepo lakini watuhumiwa hao walilazimisha kuingia ndani kwa nguvu huku wakimshambulia kwa kumchapa na fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake na kupelekea kuanguka chini na kupoteza fahamu.

    Kamanda Msuya alisema kutokana na hali hiyo watuhumiwa walimbeba Mfaume kwenye gari lao kwaajili ya kumpeleka hospitali lakini alifariki akiwa anapewa matibabu.

    Alisema, "Mwili wa marehemu umefanyiwa uchunguzi na daktari kisha kukabidhiwa ndugu kwa taratibu za mazishi.”

    Hata hivyo, Jeshi la Polisi linatoa wito kwa makampuni na taasisi za kifedha kufuata taratibu za kisheria katika kudai fedha kutoka kwa wateja wao ili kuepusha usumbufu na madhara yanayoweza kutoka ikiwemo uharibifu wa Mali, kujeruhi na vifo.

    Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya OYA ya nchini Tanzania, Alpha Peter ameiambia BBC kuwa waliodaiwa kusababisha kifo ni watumishi wa taasisi yao na kwamba kitendo hicho hakikuwa maelekezo ya kampuni hiyo.

    Peter alisema, “Kilichofanyika, si maelekezo wala utaratibu wa taasisi yetu pale tunapoenda kudai marejesho kwa wateja wetu. Kwasasa tuko karibu na familia kuifariji lakini pia tunaendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi la Polisi wakati huu wakiendelea na uchunguzi wa tukio hilo.”

    Kampuni ya OYA ya nchini Tanzania ilisajiliwa mwaka 2020 na kwasasa inatoa huduma kwenye mikoa nane.

    Imeandikwa na Alfred Lasteck

  5. Erdogan aiita Israel "shirika la kigaidi la Kiyahudi"

    Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdoğan katika ukosoaji wake wa mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon na Gaza ameitaja nchi hii kuwa ni "shirika la kigaidi la Kiyahudi".

    Bwana Erdoğan ambaye alikuwa akizungumza mbele ya wabunge wa chama tawala cha Justice and Development, kwa mara nyingine tena alikosoa madola ya Magharibi hasa Marekani kwa kuiunga mkono Israel.

    Rais wa Uturuki pia alionya kwamba mzozo kati ya Iran na Israel umeongeza hatari ya vita vya kikanda.

    Bwana Erdogan, ambaye ana historia ndefu ya ukosoaji mkali wa Israel, hapo awali alimwita Benjamin Netanyahu "mchinjaji wa Gaza" na kumlinganisha yeye na serikali yake na Hitler na serikali ya Ujerumani ya Nazi.

  6. Mapigano yaendelea Gaza, idadi ya waliouawa yafikia 42,000

    Tumekuwa tukiangazia Lebanon asubuhi ya leo, lakini mapigano yanaendelea huko Gaza, ikiwa ni pamoja na Jabalia kaskazini, ambapo vifaru vya Israel na wanajeshi wanafanya operesheni ya ardhini.

    Katika taarifa yake asubuhi ya leo, jeshi la Israel limesema lilishambulia maeneo 45 ya Hamas huko Gaza katika muda wa saa 24 zilizopita, ikiwa ni pamoja na kambi za Hamas, kurusha roketi na maeneo ya kuhifadhi silaha.

    Wizara ya afya inayosimamiwa na Hamas huko Gaza imesema zaidi ya Wapalestina 42,010 wameuawa katika mashambulizi ya kijeshi ya Israel tangu yalipoanza mwaka mmoja uliopita.

    Hilo ni ongezeko la 45 kwa jumla ya siku iliyotangulia. Wizara haitofautishi kati ya vifo vya wapiganaji kutoka Hamas na raia, inapochapisha takwimu hizo.

    Israel imetoa amri ya kuhama kwa watu kaskazini mwa Gaza, lakini Philippe Lazzarini kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) anasema watu 400,000 wamenaswa katika mapigano.

    Unaweza kusoma;

  7. Israel yasema imeshambulia maeneo 185 ya Hezbollah katika saa 24 zilizopita

    Jeshi la Israel leo asubuhi lilitoa taarifa kuhusu mapigano katika muda wa saa 24 zilizopita, likisema yalipiga takribani maeneo 185 ya Hezbollah nchini Lebanon.

    Katika taarifa, Vikosi vya Ulinzi vya Israel vinasema wanajeshi wake walijihusisha katika "makabiliano ya karibu" na wapiganaji wa Hezbollah waliokuwa ardhini kusini mwa Lebanon, pamoja na kufanya mashambulizi zaidi ya anga.

    Wakati wa mapigano ya ardhini, kamanda wa Israel aliuawa kwa kurushiana risasi, IDF inasema.

    Hezbollah hapo awali ilidai kuwa imezuia uvamizi wa Israel katika maeneo ya mashariki na magharibi mwa mpaka wa Lebanon.

    IDF pia inasema ililenga maeneo 45 ya Hamas katika Ukanda wa Gaza katika muda wa saa 24 zilizopita.

    Unaweza kusoma;

  8. Kitabu kinadai Trump alituma kwa siri mashine za kupima Covid kwa Putin

    Kitabu kipya cha mwandishi mkongwe wa Watergate Bob Woodward kinasema Donald Trump alituma kwa siri mashine za kupima Covid-19 kwa Vladimir Putin kwa matumizi ya kibinafsi wakati zilikuwa na uhaba, madai ambayo yalikataliwa kwa hasira na kambi ya kampeni ya Trump.

    Kitabu hicho kwa jina ‘War’- pia kinajumuisha madai kwamba Trump amekuwa akiwasiliana kwa siri na Putin tangu alipoondoka madarakani, kwa mujibu wa nukuu zilizotajwa na vyombo vya habari vya Marekani.

    Kambi ya Trump ilisema hakuna hata moja ya "madai hayo ya kubuni" ambayo ni ya kweli.

    "Rais Trump hakumpa idhini kabisa ya kufikia kitabu hiki kisicho na thamani kabisa ambacho ama kiko kwenye kasha la vitabu vyenye kuuzwa kwa bei ya chini au kinachotumika kama karatasi ya shashi," alisema msemaji wa kambi ya Trump Steven Cheung katika taarifa yake kwa BBC.

    Kitabu hicho kipya, kitakachotolewa wiki ijayo, kinahusisha kuendelea kwa mawasiliano kati ya rais huyo wa zamani na Putin na msaidizi mmoja wa Trump ambaye hajatajwa kwenye kitabu hicho.

    Soma zaidi:

  9. Kesi ya kumuondoa Gachagua madarakani yatua rasmi Bunge la Seneti

    Bunge la Seneti nchini Kenya litaanza kujadili hoja ya kumuondoa afisini Naibu wa rais Rigathi Gachagua siku za Jumatano na Alhamisi wiki ijayo.

    Seneti leo imefanya kikao kupokea hoja hiyo kutoka kwa Kiongozi wa walio wengi Aaron Cheruyot baada ya bunge la kitaifa kupifa kura ya kumuondoa afisini Gachagua siku ya Jumanne.

    Bunge zima la Seneti litachunguza mashtaka dhidi ya Gachagua na kusikiliza ushahidi kutoka pande zote .

    Gachagua alitimuliwa Jumanne baada ya wabunge 281 kupiga kura ya kuunga mkono kuondolewa kwake afisini.

    Kiwango kilichowekwa na katiba ni angalau wabunge 233.

    Soma pia

  10. Hezbollah inasema iliwarudisha nyuma wanajeshi wa Israel kwenye mpaka

    Hezbollah inasema iliwavizia wanajeshi wa Israel kwa kifaa cha kulipua usiku kucha, wakati wakijaribu kuelekea mji wa Blida, karibu na mpaka wa Israel-Lebanon upande wa mashariki.

    Vile vile, Hezbollah inasema ilirudisha nyuma kikosi cha Israel kilichojaribu kuingia katika eneo la Labouneh, karibu na pwani ya magharibi mwa Lebanon.

    Hezbollah ilirusha makombora kaskazini mwa Israel

    Wakati huo huo, Jeshi la Israel linasema limenasa makombora mawili yaliyorushwa kutoka Lebanon asubuhi ya leo kuelekea maeneo ya Carmel na Menashe, kusini mwa mji wa bandari wa Haifa.

    Ving'ora vya mashambulizi ya anga pia vilisikika katika mji wa Kaisaria, ulioko kwenye pwani kati ya Haifa na Tel Aviv.

    Siku ya Jumanne, Israel ilisema iligundua roketi 180 zilizorushwa kutoka Lebanon.

    Baadhi ya maeneo 100 yalilengwa katika eneo la Haifa - mengi yalinaswa, lakini mengine yalifika kwenye vitongoji vya Kiryat Yam na Kiryat Motzkin.

    Soma zaidi:

  11. Msumbiji yafanya uchaguzi huku chama tawala kikitarajiwa kudumisha uongozi

    Vituo vya kupiga kura vimefunguliwa nchini Msumbiji huku watu milioni 17 wakitarajiwa kupiga kura katika uchaguzi wa rais, pamoja na uchaguzi wa wabunge na majimbo.

    Katika uchaguzi huo chama tawala cha Frelimo kinatarajiwa kudumisha utawala wake.

    Rais Filipe Nyusi anajiuzulu baada ya mihula miwili na mgombea wa chama hicho Daniel Chapo anatarajiwa kuchukua nafasi yake.

    Frelimo imetawala Msumbiji tangu uhuru kutoka kwa Ureno mwaka 1975.

    Daniel Chapo atakuwa kinyang’anyironi na Venancio Mondlane, mgombea binafsi mwenye haiba ambaye amevutia umati mkubwa wa watu, kamanda wa zamani wa waasi Ossufo Momade, na kiongozi mdogo wa chama cha upinzani, Lutero Simango.

    Matokeo ya uchaguzi huo yanatarajiwa kutangazwa kabla ya Oktoba 24.

    Msumbiji imekuwa ikikabiliana na uasi wa Kiislamu katika eneo la kaskazini ambao umesababisha kusitishwa kwa miradi ya mabilioni ya dola ya gesi huku maelfu ya wakaazi wakihama makwao.

    Umaskini pia ni tatizo kwa idadi kubwa ya watu waliojiandikisha kupiga kura.

  12. Brazil yaondoa marufuku dhidi ya X baada ya kampuni hiyo kulipa faini ya dollar milioni 5

    Mahakama ya Juu Zaidi ya Brazil imesema kuwa inaondoa marufuku ya mtandao wa kijamii wa X, ambao zamani ulijulikana kama Twitter.

    Katika uamuzi wake, Jaji Alexandre de Moraes alisema kwamba aliidhinisha "kurudishwa mara moja" kwa shughuli za mtandao wa X nchini humo baada ya kulipa faini kubwa na kuzuia akaunti zinazotuhumiwa kueneza habari potofu.

    Kulingana na taarifa, jukwaa hilo limelipa faini ya jumla ya reais milioni 28 ($5.1m; £3.8m) na kukubali kuteua mwakilishi wa eneo hilo, kama inavyotakiwa na sheria ya Brazil.

    Moraes alikuwa amezuia ufikiaji wa jukwaa hilo linalomilikiwa na Elon Musk, baada ya kukataa kupiga marufuku wasifu kadhaa uliochukuliwa na serikali kueneza habari potofu kuhusu uchaguzi wa Rais wa Brazil wa 2022.

    Shirika la mawasiliano nchini Brazil, Anatel, limeagizwa kuhakikisha huduma imeanza tena kwa watumiaji zaidi ya milioni 20 nchini humo ndani ya saa 24.

    Baada ya miezi kadhaa ya kukaidi maagizo ya mahakama, Musk aliwafuta kazi wafanyakazi wa kampuni hiyo wa Brazil mwishoni mwa Agosti na kufunga ofisi ya X nchini Brazil.

    "Uamuzi wa kufunga ofisi za X nchini Brazil ulikuwa mgumu," Musk, ambaye pia ni mkuu wa kampuni ya kutengeneza magari ya umeme ya Tesla na kampuni ya roketi ya SpaceX, aliandika wakati huo.

    Aliyejitangaza kama "mtiifu wa uhuru wa kuzungumza", mfanyabiashara huyo bilionea alielezea hatua ya Jaji Moraes ya kupiga marufuku akaunti kadhaa kama matumizi mabaya ya mamlaka na ukiukaji wa uhuru wa kujieleza.

    Siku kadhaa baadaye, Jaji Moraes aliamuru jukwaa zima kuzuiwa kote nchini humo.

    Watumiaji wengi walihamia kwenye majukwaa mbadala kama vile Bluesky, na mahitaji ya VPN (Virtual Proxy Networks) nchini Brazili yaliongezeka.

    Soma zaidi:

  13. Raia wa Afghanistan akamatwa kwa madai ya njama ya shambulizi siku ya uchaguzi wa Marekani

    Wizara ya Sheria ya Marekani imemkamata mtu anayedaiwa kupanga shambulizi siku ya Uchaguzi na anahusishwa na kundi la Islamic State.

    Mshukiwa, Nasir Ahmad Tawhedi, 27, ni raia wa Afghanistan anayeishi katika mji wa Oklahoma, kulingana na waendesha mashtaka.

    Mkurugenzi wa FBI Christopher Wray alisema katika taarifa ya Jumanne kwamba: "Mshtakiwa huyu, akichochewa na ISIS, alikula njama ya kufanya shambulio la kikatili, Siku ya Uchaguzi, hapa nchini kwetu."

    FBI ilisema alikuwa akijaribu kuhifadhi silaha, na alikuwa amechukua hatua kuuza mali za familia yake na kuwahamisha wanafamilia wake nje ya nchi.

    Bw Tawhedi anashtakiwa kwa kutoa, kujaribu kutoa, na kula njama ya kusaidia au kutoa rasilimali kwa shirika la kigeni la kigaidi; na kwa kujaribu kununua bunduki na risasi za kutumia kufanya uhalifu au kitendo cha kigaidi.

    FBI ilisema Bw Tawhedi alifanya kazi na mwenzake ambaye jina lake halikutajwa, jamaa wake mwenye umri mdogo na pia ni raia wa Afghanistan.

    Inamtuhumu kwa kutumia propaganda za Islamic State kupitia mtandao, kulingana na rekodi za Google zilizopatikana na vyombo vya sheria, na kutoa michango kwa shirika la kutoa msaada linalotumika na IS.

    "Tutaendelea kupambana na tishio linaloendelea ambalo ISIS na wafuasi wake wanaleta kwa usalama wa taifa wa Marekani, na tutawatambua, kuwachunguza na kuwafungulia mashtaka watu wanaotaka kuwatisha watu wa Marekani,'' alisema Mwanasheria Mkuu Merrick Garland.

    Bw Tawhedi alitafuta bunduki aina ya AK-47 ili kutumia katika shambulio hilo, mamlaka zinadai.

    Mnamo tarehe 7 Oktoba, yeye na mwanzilishi mwenza walikutana na watu ambao kwa kweli walifanya kazi kwa siri kwa FBI kununua silaha na risasi.

    Baada ya ununuzi huo, Bw Tawhedi na mshiriki mwenzake walikamatwa.

    Bw Tawhedi aliwasili Marekani mnamo Septemba 2021 kwa visa maalum ya wahamiaji pamoja na mkewe na mtoto wake mdogo.

    Alikuwa anaishi katika mji wa Oklahoma wakati wa kukamatwa kwake.

    Haijabainika mara moja ikiwa ana uwakilishi wa kisheria.

    Pia unaweza kusoma:

  14. Urusi inadhamiria kusababisha ghasia katika mitaa ya Uingereza, inaonya MI5

    Shirika la kijasusi la Urusi limekuwa likifanyia kazi suala la kuhakikisha kuna "ghasia endelevu katika mitaa ya Uingereza na Ulaya", mkuu wa MI5 amesema.

    Akitoa taarifa yake ya kila mwaka kuhusu vitisho vya usalama vinavyoikabili Uingereza, Ken McCallum alisema maafisa wa ujasusi wa GRU waliendeleza vitendo vya "uchomaji moto, hujuma na vingine vya hatari zaidi pamoja na kuongezeka kwa uzembe" nchini Uingereza baada ya nchi hiyo kuunga mkono Ukraine katika vita vyake na Urusi.

    MI5 pia imejibu njama 20 zilizoungwa mkono na Iran tangu 2022, alisema, ingawa aliongeza kuwa kazi zake nyingi bado zinahusisha itikadi kali za Kiislamu na kufuatiwa na ugaidi uliokithiri wa mrengo wa kulia.

    Mchanganyiko wa vitisho vinavyohusiana na ugaidi kutoka kwa mataifa ulimaanisha MI5 ilikuwa na "kazi moja walioyoipa kipaumbele", alionya.

    Katika hotuba yake ya wigo mpana, alisema:

    • Vijana walikuwa wakivutiwa zaidi na itikadi kali mtandaoni, huku 13% ya wale waliochunguzwa kwa kuhusika na ugaidi walikuwa na umri wa chini ya miaka 18.
    • Jumla ya njama 43 zilizofanywa dakika za mwisho zilihusisha bunduki na vilipuzi kwa nia ya kutekeleza "mauaji ya watu wengi" nchini Uingereza zilizuiliwa tangu 2017
    • Uchunguzi wa vitisho dhidi ya serikali uliofanywa na MI5 uliongezeka kwa 48%
    • Kazi ya kukabiliana na ugaidi imesalia katika pande mbili kati ya "asilimia 75 ya Waislamu wenye msimamo mkali, na 25% ni ugaidi uliokithiri wa mrengo wa kulia"

    Pia kulikuwa na "imani na itikadi mchanganyiko" na ilibidi MI5 kukabiliana nazo, aliambia mkutano huo katika kituo cha oparesheni za kukabiliana na ugaidi cha MI5 huko London.

    Pia unaweza kusoma:

  15. Jimbo la Florida Marekani lajitayarisha kukabiliana na kimbunga Milton

    Wakazi wa eneo la Florida wanaharakisha kumaliza maandalizi ya dharura - au waondoke tu - huku Kimbunga Milton kikielekea kwa haraka kwenye Ghuba ya Tampa iliyo na watu wengi.

    Milton kwa sasa ni dhoruba ya aina ya tano, yenye upepo mkali wa hadi 165mph (270km/h).

    Kinatarajiwa kupiga kwa nguvu zote Jumatano usiku, chini ya wiki mbili baada ya jimbo hilo kukumbwa na kimbunga cha Helene.

    Rais Joe Biden alionya watu huko Florida Jumanne kuondoka makwao na kulichukulia suala hilo kwa uzito mkubwa kama lenye kuhusisha "maisha au kifo" wakati jimbo hilo likijitahidi zaidi kwenye uhamishaji.

    Kimbunga hicho kikiwa kimewekwa "kitengo cha tano, ni kama kimbunga kikubwa," mkazi mmoja wa jiji la Ghuba la Bradenton aliambia BBC kutoka hoteli ambayo amehamia Kissimmee.

    "Nisingependa kuwa huko," alisema Gerald Lemus. "Hii itakuwa dhoruba isiyokifani haijalishi itakumba wapi."

    Bw Lemus, ambaye ameishi Bradenton maisha yake yote, alisema hajawahi kuhama kutokana na dhoruba zilizotangulia. Lakini aliamua kufanya hivyo kwa ajili ya usalama wa binti yake wa miaka minane.

    "Nilimtazama tu na sikuweza kumtia mashaka kwa kitu kama hiki," alisema Jumanne usiku.

    "Ni hatua ya hatari ambayo hatukutaka kuichukua."

    ML Ferguson amekuwa akihangaika kujenga upya nyumba yake huko Anna Maria, Florida, baada ya kuharibiwa vibaya mwezi uliopita na kimbunga Helene, ambacho kilikuwa kikali kilichowekwa kwenye kitengo cha nne.

    "Hiki kitakuwa kibaya zaidi kuliko Helene," alisema kwenye simu akiwa katika barabara kuu nje ya jiji.

    "Gari langu limeharibika kiasi cha kutoweza kutengenezeka tena, sote tulifutwa kazi, na mali [zangu] ziliharibiwa. Baada ya dhoruba hii kupiga, itakuwa rasmi sasa sina makazi."

    Soma zaidi:

  16. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 09/10/2024