Majaribio ya makombora ya Korea Kaskazini: Picha kutoka angani zatolewa

Muda wa kusoma: Dakika 3

Vyombo vya Habari vya serikali nchini Korea Kaskazini vimetoa picha zinazosema kuwa zilichukuliwa kutokana na majaribio ya kombora lake kubwa zaidi kutoka mwaka 2017.

Picha hizo zinaonesha sehemu za rasi ya Korea na maeneo yaliyo karibu yaliyonekana kutoka angani.

Korea Kaskazini ilisema kuwa kombora hilo lilikuwa la masafa la kati ya Hwasong-12.

Korea Kusini na Japan zilisema lilifikia umbali wa kilomita 2,000 (maili 1,242) kabla ya kuanguka kwenye maji kutoka Japan. Nchi zote mbili zimeshutumu jaribio hilo, ambalo ni la saba mwezi huu.

Picha hizo, zilizotolewa na shirika la kitaifa la habari la Korea Kaskazini, KCNA, ziliripotiwa kupigwa kwa kutumia kamera zilizowekwa kwenye kichwa cha kombora lililofanyiwa majaribio.

Picha mbili kati ya hizo zinaonyesha wakati wa kurushwa na nyingine inaonyesha kombora likiwa katikati ya safari, iliyopigwa kutoka juu.

Maafisa wa Japan na Korea Kusini wanakadiria kuwa kombora hilo lilipaa kwa dakika 30kwa umbali wa kilomita 800.

Umoja wa Mataifa unapiga marufuku Korea Kaskazini kufanya majaribio ya silaha za balestiki na za nyuklia, na imeweka vikwazo vikali.

Nchi hiyo ya Asia Mashariki mara kwa mara inakiuka marufuku hiyo , na kiongozi wake Kim Jong-un ameapa kuimarisha ulinzi wa wa nchi yake.

Afisa mkuu wa Marekani alitoa wito kwa Korea Kaskazini kujiunga na mazungumzo ya moja kwa moja kuhusu mipango yake ya nyuklia na makombora bila masharti yoyote, Reuters iliripoti.

"Tunaamini ni wakati sahihi kabisa kuanza kuwa na mazungumzo haya makubwa," afisa huyo alisema.

Awali Marekani ilitoa wito kwa Koerea Kakazini "kujiepusha na vitendo hivyo vya kudhoofisha usalama zaidi".

Majaribio ya makombora ya Korea Kaskazini huwa yanatangazwa siku inayofuata na shirika la habari la kitaifa.

Siku ya Jumatatu, KCNA ilisema kuwa kombora hilo lilikuwa limerushwa ili "kuthibitisha usahihi wake". Inasemekana Bw Kim hakuwepo.

Ilirushwa kwa kutumia "mfumo wa juu zaidi wakurusha kombora kutoka eneo la kaskazini-magharibi hadi Bahari ya Mashariki ya Korea kwa kuzingatia usalama wa nchi jirani", shirika hilo liliongeza.

Mchanganuzi wa Korea Kaskazini Ankit Panda alisema kutokuwepo kwa Bw Kim, na lugha iliyotumiwa kwenye vyombo vya habari kuelezea uzinduzi huo, zinaonyesha kuwa jaribio hili lilinuiwa kuthibitisha kwamba mfumo wa makombora ulifanya kazi inavyopaswa, badala ya kuonyesha teknolojia mpya.

KCNA iliripoti kuwa kombora lililojaribiwa lilikuwa masafa ya kati ya Hwasong-12. Ni mara ya kwanza kwa kombora lenye uwezo wa nyuklia la ukubwa huo kurushwa tangu mwaka 2017.

Mwaka huo, kombora hilo lilijaribiwa mara sita ikiwa ni pamoja na kurushwa mara mbili kwenye kisiwa cha Japan cha Hokkaido, Hali iliyosababisha king'ora kulia na kutoa arifa za kielektroniki kwa wakazi wa eneo hilo.

Korea Kaskazini imesema hapo awali kuwa Hwasong-12 inaweza kubeba "kinu kikubwa cha silaha za nyuklia."

Jaribio la saba mwezi huu

Jaribio la Jumapili lilikuwa ni la saba la kombora la Korea Kaskazini tangu kuanza kwa mwaka huu, na kuifanya Januari kuwa moja ya miezi yenye shughuli nyingi zaidi kwa programu ya makombora ya nchi hiyo.

Wataalamu wanasema kuna sababu kadhaa zinazochochea mfululizo huo wa uzinduzi, ikiwa ni pamoja na kuashiria nguvu ya kisiasa kwa jamii ya kimataifa na za kikanda, hamu ya Kim Jong-un ya kuishinikiza Marekani irudi kwenye mazungumzo ya nyuklia ambayo yamekwama kwa muda mrefu na pia hitaji la vitendo la kujaribu uhandisi mpya na mifumo ya amri za kijeshi.

Muda pia unaonekana kuwa muhimu, unakuja kabla tu ya Michezo ya Olimpiki ya Majira ya baridi nchini Uchina, na kabla ya uchaguzi wa rais wa Korea Kusini mnamo Machi.

Majaribio hayo yameongezeka guku uchumi wa Korea Kaskazini ikiendelea kuzorota kutokana na vikwazo vinavyoongozwa na Marekani, changamoto zinazohusiana na majanga na miongo kadhaa ya usimamizi mbaya.