Jinsi wahamiaji kutoka Afrika wanavyohatarisha maisha kuingia Ulaya

Chanzo cha picha, EPA
"Nilisema kwaheri kwa familia yangu na nikaondoka bila kitu chochote," anaeleza Mohamed, mwenye umri wa miaka 30 kutoka Morocco.
Akizungumza na chombo cha utangazaji cha Uhispania RTVE, alitoa maelezo juu ya jinsi alivyojiunga na wahamiaji wengine wengi ambao waliingia kwa njia haramu katika eneo la Uhispania linalozungukwa na Afrika la Ceuta tangu Jumatatu.
Sawa na wahamiaji wengi, alisema ajira ni tatizo kuu lililomfanya ajaribu kuvuka.
"Ninataka kufanya kazi na kusaidia familia yangu. Mimi na marafiki zangu wote, tunataka kufanya kazi."

Chanzo cha picha, Guardia Civil
Mohamed aliiambia televisheni ya Uhispania kuwa alichukua teksi na binamu yake na marafiki wake kadhaa kabla ya kuogelea kwa muda wa dakika 30 kulifikia eno hilo la Uhispania.
Wakiwa njiani kuelekea kwenye mpaka walisimamishwa na Maafisa wa Morocco, alisema , lakini wakatuacha tuendelee, ilikuwa ni kama ndio na hapana ".
Zaidi ya wahamiaji 5,600 kati ya wahamiaji 8,000 walioingia wamerudishwa makwao, maafisa wa Uhispani wanasema.
Makumi kadhaa ya vijana walipanga mistari kwa ajili ya kurejeshwa tena Morocco Jumatano wiki hii.
Kwa mujibu wa Shirika la habari la Uhispania Efe, polisi wa Moroccan sasa wamefunga eneo la mpaka ili kuzuia jaribio lolote la watu kuvuka mpaka na kuingia nchini humo.

Maeneo ya Uhispani ya Ceuta na Melilla yanayozingirwa na eneo la Afrika Magharibi yamekuwa kivutio kukubwa cha wahamiaji Waafrika wanaojaribu kuingia Ulaya .
Waziri wa serikali ya Morocco, ameeleza kuwa nchi yake imekuwa ikilegeza udhibiti wa mipaka yake na wiki hii imeamua kuimarisha udhibiti huo kujibu hatua ya afisa wa ngazi ya juu wa kijeshi anayepinga utawala wa Morocco wa Sahara Magharibi kuruhusiwa kupata matibabu hospitalini nchini Uhispania mwezi uliopita.
Nini kilichotokea wiki hii?
Wahamiaji wengi wao wakitumia maboya ya kuogelea-walianza kuwasili Ceuta Jumatatu mapema.
Huku wengi wao wakiwa ni vijana, familia nzima na watoto wapatao 1500 pia waliingia Uhispania.
Takriban mtu mmoja alikufa alipokuwa akijaribu kuvuka kuingia Uhispania wiki hii.
Jumanne, Uhispania iliwapeleka wanajeshi kusaidia kuimarisha ulinzi wa polisi kwenye mpaka wa Ceuta.

Chanzo cha picha, AFP
Tukio la vuta ni kuvute lilishuhudiwa katika mwambao huku familia zikiogelea ndani ya maji na wanajeshi wa Uhispania walionekana kwenda ndani ya bahari kuwaokoa watoto wadogo.
Kufikia Jumanne jioni, ripoti zilisema kuwa idadi ya watu waliojaribu kuingia kwa njia ya bahari sasa imepungua. Baadhi ya wahamiaji walirejea kwa hiari, Morocco na wengine walishuhudiwa wakirejeshwa na wanajeshi.

Chanzo cha picha, Reuters
Katika eneo jingine la Uhispania, Melilla, Waafrika kutoka maeneo ya kusini mwa jangwa la Sahara wapatao 86 waliingia Jumanne wakitokea eneo la kusini . Melilla ina uzio (fensi) mkubwa na wahamiaji wengine mamia kadhaa walizuiwa na vikosi vya usama, kulingana na taarifa za shirika la habari la Efe
Maafisa wa Uhispania walinukuliwa na Efe wakisema kuwa walinzi wa Morocco walivisaidia vikosi vya Uhispania ndani ya eneo la Melilla.
Vyombo vya habari vya uhispania vilisema kuwa ilikuwa ni tofauti na Ceuta, ambako wazinzi wa mpaka wa Moroccan walisimama tu na kuangalia huku wahamiaji wakiingia baharini kujaribu kuingia katika eneo hilo.
'Morocco jinsi ilivyo'
Akiwa na begi lake dogo la vitu vyake begani mwake, Moktar Gonbor mwenye umri wa miaka 30 alielezea kwa ufupi kwa nini vijana wengi sasa wanaelekea nyumbani.
"Hatuna chakula, hatuna fedha, na tulilala barabarani usiku uliopita ." Alikuwa akirejea Morocco-hata kama maisha yake kule sio yale aliyoyataka.
Mitaa michake mbali kutoka mahala alipokuwa, wenyeji katika baa kwa jina Fernando walikua wakinywa kahawa na kutazama televisheni kuu picha za kipekee za rekodi ya wahamiaji waliowasili kwa saa 24 zilizopita.

Mwanamke mwenye umri wa miaka zaidi ya sitini kwa jina Mercedes, alielezea kuwa anajihisi mwenye kuwahurumia watoto wa wahamiaji ambao hata hawakuwa wamevaa nguo.
Lakini aligonga meza kwa hasira wakati alipotuambia kuwa wahamiaji waliruhusiwa kuingia kupitia mpakani kila wakati Morocco ilipotaka pesa au kitu fulani kutoka kwa Uhispania.
Rafiki yake, Maria Jesus, aliingilia kati mazungumzo akasema: "Waziri Mkuu anapaswa kuiambia Morocco jinsi ilivyo na kuwarejesha katika mahali pao ."













