Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Kwanini 'jeans' zilizochanika magotini na mapajani zazuwa gumzo India
Denimu - mavazi ya vitambaa vyenye nyuzi za asili kama vile jeans zilizochanika kwenye magoti na mapajani zimeanza tena kuwa gumzo la utovu wa nidhamu kwa vijana.
Wa hivi karibuni kabisa kukasirishwa na vazi hilo ni waziri Tirath Singh Rawat wa kaskazini mwa India jimbo la Uttarakhand aliyeteuliwa hivi karibuni.
Mapema wiki hii, waziri huyo alilaumu "jeans zilizochanika" kama moja ya kile kinachosumbua vijana.
Akizungumza katika warsha iliyoandaliwa na Tume ya Taifa ya Kulinda Haki za Watoto, Bwana Rawat alimkosoa mwanamke ambaye hakutajwa aliyekutana naye ndani ya ndege.
Alisema, mwanamke huyo alikuwa akisafiri na watoto wake wawili na alikuwa amevaa viatu aina ya "boots, suruali ya jeans iliyochanika kwenye magoti na bangili kadhaa mkononi".
"Unaendesha shirika lisilokuwa la kiserikali, umevaa jeans iliyochanika kwenye magoti, unatembea na watoto, utawafunza maadili gani?" waziri alimuuliza.
Waziri huyo alikaripia raia wa India kwa "kutembea uchi" na kudai kuwa "wakati watu nchini India wanavaa jeans zilizochanika, wale walio nje ya nchi wanafunika miili yao na kufanya yoga".
Matamshi ya Bwana Rawat yamesababisha shutuma kali nchini India.
Chama cha upinzani cha Congress party kilitoa taarifa na kumtaka "aombe msamaha kwa wanawake wote India" - au ajiuzulu.
Alhamisi, kiongozi mwandamizi Priyanka Gandhi Vadra alishirikisha wengine picha za Waziri Mkuu Modi na mmoja wa mawaziri wenzake "wakionesha magoti yao":
Mkuu wa tume ya Delhi kwa wanawake Swati Maliwal aliandika ujumbe kwenye Twitter akimshutumu Bwana Rawat kwa "kuendeleza chuki dhidi ya wanawake":
Katika ujumbe wake kwenye Twitter, Maliwal alisema kuna tatizo sio tu vile alivyosema Bwana Rawat - lakini pia alivyokubali "kudharau wanawake".
Matamshi yake yamewafanya maelfu ya wanawake wa India katika mtandao wa Twitter na baadhi ya wanaume kuweka picha zao wakiwa wamevaa jeans zilizochanika. Na hashtag za #RippedJeansTwitter na #RippedJeans zikisambaa mtandaoni kwa muda.
Ijumaa, Bwana Rawat aliomba msamaha kwa matamshi yake kwa aliowakera. Alisema nia haikuwa kuwadharau na kuwa kila mmoja yuko huru kuvaa anachotaka.