Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Rais Erdogan wa Uturuki 'aitupa pipani barua ya Trump kuhusu Syria '
Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan aliitupa barua ya rais wa Marekani Donald Trump katika "pipa la taka", BBC imefahamishwa.
Katika barua hiyo ilioandikwa Octoba tarehe 9 na kutumwa baada ya vikosi vya Marekani kuondolewa Syria, Bw. Trump alimuambia Erdogan: "Usijifanye kuwa na nguvu. Usiwe mpumbavu!"
Vyanzo vya ofisi ya rais wa Uturuki vimeiambia BBC kuwa barua hiyo "ilimkasirisha sana" Rais Erdogan.
Siku ambayo barua hiyo ilipokewa, Uturuki ilianza operesheni yake dhidi ya vikosi vya Kikurdi katika eneo la mpakani.
"Wacha tufikie mpango mzuri! Bilashaka hutaki kuhusika na mauaji ya maelfu ya watu, na mimi pia sitaki kuhusika na uharibifu wa uchumi wa Uturuki - na nitafanya hivyo," Bw. Trump alisema katika barua hiyo.
"Historia itakuhukumu kwa haki ukishughulikia suala hili kwa njia ya kibinadamu. Itakuhukumu daima kama shetani kwa maovu."
Katika majibu yake, vyanzo katika ofisi ya rais wa Uturuki vilisema: "Rais Erdogan alipokea barua, na kupinga vikali yaliomo na kuitupa kwenye pipa la taka."
Rais Trump amelaumiwa vikali kwa kuwaondoa wanajeshi wa Marekani nchini Syria huku wakosoaji wakisema kuwa hatua hiyo iliipatia Uturuki nafasi ya kuanzisha mashambulizi ya kijeshi nchini humo.
Ukosoaji mkubwa umetoka ndani ya chama chake Bw.Trump.
Katika hatua isiokuwa ya kawaida, wabunge 129 wa chama cha Republican katika bunge la uwakilishi waliungana na wenzao wa chama cha Democratic kupiga kura ya kupinga uamuzi huo siku ya Jumatano.
Azimio hilo la pamoja ambalo pia lilimtaka rais Erdogan kukomesha mara moja oparesheni ya kijeshi dhidi ya vikosi vinavyoongozwa na wapiganaji wa Kikurdi, lilipitishwa kwa kura 354 - 60.
Spika wa bunge la Marekani, Nancy Pelosi pia alikutana na rais Trump, kujadili suala hilo katika mkutano uliokumbwa na majibizano makali yaliyochangia yeye na kiongozi wa wachache katika bunge la Seneti, Charles Schumer, kuondoka katika chumba cha mkutano huo.
Viongozi wa Republican walisema hatua ya Bi Pelosi ni ukosefu wa "nidhamu", na kumkosoa kwa "kuondoka katika mkutano huo".
Bi. Pelosi na Bw.Trump pia walilaumiana kwa kile "kilichotokea", na baadae Trump akaweka kwenye Twitter picha ya majibizano kati yao.
Lakini picha hiyo imesifiwa na Wanachama wa Democrats, ambao walisema ni ya "kishujaa" na ilimuonesha Bi. Pelosi akiwa "katika ubora wake". Bi Pelosi pia aliifanya picha hiyo kuwa picha yake kuu katika mtandao wa Twitter.
Mapema siku ya Jumatano Rais Trump, alisema Marekani haitaingilia kati oparesheni ya kijeshi ya Uturuki nchini Syria, kwasababu nchi hiyo "sio mpaka wake", na kuongeza kuwa Wakurdi ambao walikuwa washirika wao wa zamani "sio malaika".