Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Watoto waliokuwa wakishikiliwa kwenye magereza yenye hali mbaya mjini Texas waondolewa
Watoto wahamiaji takribani 250 wameondolewa kwenye kituo kilicho kwenye mpaka jimboni Texas nchini Marekani, kituo ambacho kilikuwa kimewaweka watoto hao kwa majuma kadhaa.
Wanasheria walipewa ruhusa na Jaji wamesema watoto hao waliachwa wakiwa na hali mbaya.
Mmojawapo ameiambia BBC kuwa watoto wahamiaji ''walifungiwa kwenye magereza yaliyo katika hali mbaya yenye choo cha wazi katikati ya chumba'' ambapo walikula na kulala hapo.
Wazazi wengi wanavuka kwenye mpaka wa Marekani, wengi wao kutoka Amerika ya Kati, walitengana na watoto wao mwaka 2018.
Mbali na hayo, doria mjini Texas zimeripoti vifo vya wahamiaji saba wiki hii ambao wakiwemo watoto wawili na mtoto mchanga mmoja.
Hali ilikuwaje?
''Hakuna mtu aliyekuwa akiwatunza watoto hawa...walikuwa hawaogeshwi, Profesa Warren Binford wa chuo kikuu cha Williamette ameiambia BBC baada ya kutembelea eneo hilo.
''Mamia ya watoto waliwekwa mahali pamoja wakiwa wamejazana, kuna chawa, kuna mlipuko wa homa ya mafua. Watoto wamekuwa wakiwekwa bila uangalizi wa watu wazima, watoto ambao wanaumwa sana,wakiwa wamelala chini.
Flora Mukherjee mwanasheria mwingine aliyetembelea kituo hicho amekiambia kituo cha habari cha CBS kuwa '' watoto hao walikuwa wamevaa nguo zilezile walizovaa wakati walipokuwa wakivuka mpaka''.
''Ni jambo linalohuzunisha,lisilo la kibinaadamu na halipaswi kufanyika nchini Marekani.''
Wakati simulizi kuhusu hali ya kituo kilichowaweka watoto zikiendelea kuibuka, baadhi ya watu wamejitokeza kutoa msaada kwa watoto, lakini walirudishwa na maafisa wa mpakani.
Kundi moja lilisema lilitumia pauni 267 kununua nepi, sabuni,wanasesere kwa ajili ya watoto lakini walipuuzwa na maafisa waliokuwa kazini kwenye kituo hicho.
Mamlaka zimesema nini?
Katika taarifa yao, mamlaka ya mpakani hapo ilisema kuwa kituo hicho hakina uwezo wa kuhudumia watoto inavyostahili wakisema kuwa wanahitaji msaada wa kibinaadamu haraka sana kuondokana na hali hiyo.
Shirika hilo limesema kuwa wamewapeleka watoto kwenye vituo vingine mara walipoona kuwa kuna nafasi.
Wabunge wanafanya nini?
Wabunge wa chama cha Democrats wamekuwa wakijaribu kusukuma hoja ya kupeleka kiasi cha dola bilioni 5 kwenye eneo la mpaka, lakini suala hilo limepata pingamizi.
Baadhi ya wabunge wamesema kupeleka fungu hilo kutafanya kuendelea kwa vitendo vya uvamizi na kuwafunga watu.
Tayari Ikulu ya Marekani imetishia kupiga kura ya turufu dhidi ya mswada huo ikisema haipeleki fedha kutatua matatizo ya sasa.
Serikali ya Trump imeomba fedha zaidi kusaidia idara ya uhamiaji na masuala ya ulinzi na usalama.
Wazazi wako wapi?
Kutengana kwa watoto wahamiaji na wazazi wao kulianza mwaka 2018, chini ya sera ya rais Donald Trump ya kupiga vita wahamiaji kuingia Marekani, sera iliyofanya watoto 3,000 kutengana na wazazi wao.
Chini ya sera, iliyotangazwa mwezi Mei mwaka 2018, ikisema kuwa wanaovuka mpaka kinyume cha sheria watashtakiwa-sheria iliyotaka watoto wabaki wakitunzwa vituoni.
Pamoja na kuwepo kwa sera hiyo, mamlaka za usalama wa ndani, huduma za afya nchini humo zilisema kuwa hawakuwa na taarifa kuhusu sera hiyo kabla ya kutangazwa, hivyo hazikuwa zimejiandaa kwa ongezeko la watoto waliowaweka kwenye vituo.
Pia kumekuwa na idadi maalumu iliyowekwa na mamlaka za Marekani kuhusu idadi ya watu wanaoomba hifadhi kila siku, hali inayofanya, muda wa kusubiri kuwa mrefu zaidi.
Baadhi ya wahamiaji na familia zao badala yake hujaribu kupita njia za hatari mbali na vituo halali vya kuingilia, au huwatumia wasafirishaji binaadamu kuwawezesha kuingia nchini Marekani.