Maalim Seif Sharif Hamad na viongozi wa zamani wa CUF wapewa uanachama ACT

Chama cha ACT Wazalendo, leo kimemtambulisha rasmi kwa umma na kumkabidhi kadi NAMBA MOJA ya uanachama aliyekuwa katibu mkuu wa Chama cha wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad.
Pamoja na Maalim Seif, ambaye alitangaza siku ya Jumatatu kukihama chama cha CUF, aliyekiasisi na kukiongoza kwa zaidi ya miaka 20, viongozi wengine waandamizi zaidi ya 20 wa CUF nao wamekabidhiwa kadi za uanachama.


Maalim Seif ameeleza kwamba ameamua kujiunga na ACT yeye na viongozi wenzake kwa sababu ya siasa nzuri inayofanywa na chama hicho.


Kwa upande wao wanachama wa ACT Wazalendo, wanauona mwanga mpya wa chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2020.

Ismail Jussa Ladhu ambaye alikua Mkurugenzi wa mambo ya nje ya CUF, ni miongoni mwa viongozi waliokabidhiwa uanachama.

Baadhi ya viongozi waliotambulishwa leo na kupewa kadi za uanachama wa ACT ni pamoja na Joran Bashange (aliyekuwa naibu katibu mkuu wa CUF, Tanzania bara), Nassoro Ahmed Marzui (Naibu katibu mkuu Zanzibar), Abubakar Khamis Bakary (Jaji mstaafu na mjumbe wa baraza kuu la Uongozi, CUF) na Makam mwenyekiti mstaafu na mgombea mwenza wa Urais , katika uchaguzi mkuu uliopita wa Tanzania, Juma Duni Haji.

Akiwakaribisha viongozi hao, Mwenyekiti wa ACT Wazalendo , Yeremia Maganja, amesema, kwa mazingira ya sasa ya deomkrasia, kuungana ndiyo njia pekee ya kusaidia kujenga demokrasia ya kweli, hivyo kujiunga kwa Maalim Seif kwenye chama cha ACT Wazalendo, ni hatua muhimu kuelekea huko.

Swali kuu wachambuzi wanahoji katika mazingira haya, Je hatua zinazoshuhudiwa zitasaidia kwa kiasi gani kukiimarisha chama hicho cha upinzani katika siasa Tanzania

Sherehe zilikuwa kubwa katika ofisi za chama cha ACT wazalendo zilizo jijini Dar es salaam.
Tangu saa 12 alfajiri mamia ya wanachama wa ACT na wafuasi wa Maalim Seif walianza kukusanyika, kushuhudia, kiongozi huyo akipatiwa kadi mpya ya uanachama ya ACT.


Pamoja na wasiwasi wa wananchi wengi kuhusu hama hama ya viongozi wa vyama vya siasa hasa wenye ushawishi mkubwa kama wa Maalim Seif, mwenyekiti wa chama cha Ukombozi wa Umma. (CHAUMMA), Hashim Rungwe anasema huo ni utamaduni wa wananchi unapaswa kupewa uhuru.












