Mataifa 5 tajiri na masikini zaidi barani Afrika 2025

Chanzo cha picha, Getty Images
- Author, Abdalla Seif Dzungu
- Nafasi, BBC Swahili
- Akiripoti kutoka, Nairobi Kenya
- Muda wa kusoma: Dakika 5
Shirika la Fedha Duniani IMF limetoa orodha ya mwaka 2025 ya nchi tajiri zaidi na masikini barani Afrika.
Kiwango hiki, ambacho kinajumuisha mataifa madogo kama vile Mauritius na Libya, kinatokana na usawa wa uwezo wa kununua (PPP), ambao hurekebisha mfumuko wa bei na tofauti za gharama ili kutoa ulinganisho sahihi wa hali ya maisha.
Ulinganisho wa utajiri wa kitaifa pia hufanywa mara kwa mara kwa msingi wa usawa wa nguvu ya ununuzi (PPP), kurekebisha tofauti za gharama ya maisha katika nchi tofauti.
Hizi hapa ni nchi 5 tajiri na 5 masikini Barani Afrika mwaka 2024 Kulingana na Shirika la Fedha Ulimwenguni (IMF)
1. Ushelisheli
Taifa la Ushelisheli, lenye Pato la taifa-PPP kwa kila mtu mmoja la $43,070, ina uchumi dhabiti unaoendeshwa na utalii, uvuvi, na huduma za kifedha.
Serikali ya nchi hiyo imeweka sera zinazozingatia utalii endelevu na mseto wa kiuchumi, kuhakikisha ukuaji na utulivu wa muda mrefu.
Ushelisheli inajivunia Pato la Taifa la juu kiasi kwa kila mtu, na kuifanya kuwa mojawapo ya nchi tajiri zaidi barani Afrika.
Sekta za utalii na uvuvi ni vichochezi vikuu vya uchumi wa Ushelisheli, kuvutia uwekezaji mkubwa wa kigeni na kuchangia ukuaji wa uchumi.
Mbali na utalii na uvuvi, Seychelles inanufaika kutokana na uchumi mseto unaojumuisha huduma za kifedha na tasnia zingine.
Taifa hilo linafurahia maisha ya hali ya juu kiasi, liikiwa na huduma bora za afya na mifumo ya elimu.
Ushelisheli inashika nafasi ya 56 duniani kwa Pato la Taifa kwa kila mtu
2. Mauritius
Mauritius, yenye Pato la taifa-PPP kwa kila mtu moja la $33,954, imeendelea kuwa kitovu cha kifedha barani Afrika.
Uchumi wa nchi unasaidiwa na huduma za kifedha, utalii, na utengenezaji.
Sera za serikali huvutia uwekezaji wa kimataifa na kuongeza fursa za biashara.
Mauritius inamiliki jumla ya utajiri unaoweza kuwekezwa wa takriban dola bilioni 48.
Utajiri wa wastani kwa kila mtu nchini Mauritius unakaribia $37,500.
Taifa hilo limepata ongezeko kubwa la mamilionea, na ukuaji wa 69% katika miaka 10 iliyopita.
Kufikia Desemba 2022, Mauritius ilikuwa na watu 4,900 wenye thamani ya zaidi ya dola milioni moja na watu 10 wenye thamani ya kuzidi $100 milioni.
3. Gabon
Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.
Bonyeza hapa kujiunga
Mwisho wa Whatsapp
Gabon, yenye Pato la taifa-PPP kwa kila mtu la $24,682, inafaidika kwa kiasi kikubwa kutokana na rasilimali zake za mafuta.
Serikali imechukua hatua za kuleta mseto wa uchumi kwa kuwekeza kwenye miradi ya madini, kilimo na miundombinu ili kupunguza utegemezi wa hidrokaboni.
Gabon ni mzalishaji mkuu wa mafuta na muuzaji wa bidhaa hiyo muhimu, huku mafuta yakichangia sehemu kubwa ya mapato yake.
Pia ina amana kubwa ya manganese, mbao, na rasilimali nyingine muhimu.
Idadi ndogo ya watu nchini Gabon na mapato makubwa ya mafuta yanachangia Pato la Taifa kwa kila mtu ikilinganishwa na nchi nyingine za Kiafrika.
Licha ya utajiri wake, Gabon inakabiliwa na ukosefu wa usawa wa mapato na umaskini.
Sehemu kubwa ya wakazi wanaishi chini ya dola 2.15 kwa siku, na kiwango cha ukosefu wa ajira ni kikubwa, hasa miongoni mwa vijana.
Uchumi wa Gabon unategemea sana mapato ya mafuta, na kuifanya nchini hiyo iwe hatarini kwa kushuka kwa bei ya mafuta duniani.
4. Misri
Misri, yenye Pato la taifa-PPP kwa kila mtu moja la $21,608, ina uchumi tofauti unaoungwa mkono na utalii, kilimo, fedha zinazotumwa na kutoka nje na viwanda.
Nchi inaendelea kuwekeza katika miundombinu na kuvutia wawekezaji kutoka nje, kuimarisha msingi wake wa kiuchumi.
5. Botswana
Botswana, yenye Pato la taifa-PPP kwa kila mtu la $20,311, inatambulika kwa ukuaji wake thabiti wa uchumi na mikakati yenye mafanikio ya kuleta mseto.
Nchi imesimamia ipasavyo rasilimali zake za almasi na kuwekeza katika sekta kama vile utalii na kilimo, na kuchangia katika uimara wake wa kiuchumi.
Mataifa 5 maskini zaidi barani Afrika

Chanzo cha picha, Getty Images
Mtazamo wa kiuchumi wa 2025 unaonyesha tofauti ya utajiri wa kimataifa, huku baadhi ya nchi zikiwa na Pato la taifa la chini kwa kila mwananchi.
Changamoto za kiuchumi, ukosefu wa utulivu wa kisiasa na migogoro huathiri mataifa haya.
Ifuatayo ni orodha ya mataifa masikini zaidi barani Afrika 2025
1. Sudan Kusini
Sudan Kusini inasalia kuwa nchi yenye Pato la taifa la chini zaidi kwa kila mwananchi barani Afrika.
Migogoro ya ndani inayoendelea, kuyumba kwa uchumi, na kutegemea mauzo ya mafuta nje ya nchi kumezuia maendeleo ya kiuchumi.
Upungufu wa miundombinu na changamoto za kibinadamu huathiri maendeleo.
Mafuta huchangia sehemu kubwa ya Pato la Taifa la Sudan Kusini, mauzo ya nje na mapato ya serikali.
Licha ya utajiri wake wa mafuta, sehemu kubwa ya wakazi wanaishi chini ya mstari wa umaskini, na kuangazia "laana ya rasilimali" ambapo utajiri hautafsiriwi ipasavyo katika maendeleo.
Kukosekana kwa utulivu na migogoro kumekwamisha maendeleo ya kiuchumi hasa katika sekta ya mafuta kwani miundombinu imeharibika na uzalishaji kushuka.
Uchumi unategemea sana mafuta na hauna mseto katika sekta zingine kama kilimo au utengenezaji.
Asilimia kubwa ya watu wa taifa hilo wanaishi katika umaskini uliokithiri, na ukosefu wa usawa wa kipato.
Sudan Kusini inakabiliwa na uhaba wa miundombinu, ikiwa ni pamoja na barabara na mitandao ya usafiri, ambayo inazuia shughuli za kiuchumi.
Ukosefu wa utawala bora, ikiwa ni pamoja na rushwa na ufisadi, unazidi kuzorotesha maendeleo ya uchumi na usimamizi wa rasilimali.
2. Burundi
Burundi inaendelea kupambana na Pato la taifa la chini kwa kila mtu.
Ukuaji mdogo wa viwanda na kutegemea kilimo cha kujikimu huchangia matatizo ya kiuchumi.
Kutokuwa na uhakika wa kisiasa na uwekezaji dhaifu wa kigeni huathiri ukuaji.
Kilimo ndiyo sekta inayoongoza, ikichangia sehemu kubwa ya Pato la Taifa na kuajiri asilimia kubwa ya watu, wengi wao wakiwa katika kilimo cha kujikimu.
Sehemu kubwa ya watu wanaishi chini ya mstari wa umaskini, huku data ikionyesha kuwa 71.8% ya watu nchini Burundi wanaishi chini ya $1.90 kwa siku, kulingana na Benki ya Dunia.
Ingawa kumekuwa na ukuaji wa uchumi katika miaka ya hivi karibuni, mara nyingi inatajwa kuwa hautoshi kutatua changamoto za nchi, kulingana na Benki ya Dunia.
3. Jamhuri ya Afrika ya Kati CAR
Jamhuri ya Afrika ya Kati inakabiliwa na matatizo ya kiuchumi kutokana na mizozo ya muda mrefu na changamoto za utawala.
Nchi ina maliasili nyingi lakini haina miundombinu ya kujiendeleza.
Masuala ya usalama yanapunguza fursa za uwekezaji.
4. Malawi
Uchumi wa Malawi unategemea sana kilimo.
Hali ya hewa, uzalishaji mdogo, na ukuaji mdogo wa viwanda huathiri ukuaji wa uchumi.
Nchi inakabiliwa na changamoto katika kupanua sekta yake ya viwanda na kuboresha hali ya maisha.
5. Msumbiji
Msumbiji inaendelea kukumbwa na matatizo ya kiuchumi kutokana na changamoto za madeni na maendeleo duni ya miundombinu.
Nchi hyo inamiliki akiba kubwa ya gesi asilia lakini inakabiliwa na ugumu katika kubadilisha hilo kuwa faida kubwa za kiuchumi.















