Maandamano ya kupinga ongezeko la bei ya mafuta yashika kasi Kenya, mgomo wa usafiri ukiendelea

Chanzo cha picha, Getty Images
Ghasia zimeripotiwa katika maeneo mbalimbali nchini Kenya huku maandamano dhidi ya ongezeko la bei ya mafuta na mgomo wa usafiri wa umma ukiendelea kushika kasi.
Katika eneo la Makavazi yaliyoko Jijini Nairobi, maafisa wa polisi wamerusha mabomu ya kuwasha ili kuwatawanya waandamanaji waliokuwa wamekusanyika nje ya eneo hilo.
Katika mji wa Meru, waandamanaji wamefunga baadhi ya barabara na kuzuia magari kupita, hali inayosababisha usumbufu mkubwa wa usafiri wa umma.
Huko Kaunti ya Murang'a, kundi la vijana linaripotiwa kufanya vurugu na kuwashinikiza wafanyabiashara kufunga maduka yao wakati wa maandamano hayo.
Katika mji wa Mombasa, vijana wamejaribu kuweka vizuizi barabarani katika eneo la stendi ya magari ya Lights wakitekeleza mgomo wa usafiri wa umma. Hata hivyo, polisi wamewatawanya baadhi ya wahudumu wa matatu waliokuwa wamekusanyika eneo hilo.
Katika kaunti ya Makueni, waandamanaji wanaripotiwa kuteketeza ofisi za chama cha UDA zilizoko Wote wakilalamikia ongezeko la bei ya mafuta.
Wakati huo huo katika kaunti ya Kisii, maafisa wa polisi wamewataka madereva wa malori kuondoa magari yaliyokuwa yakizuia barabara ya Kisii kuelekea Oyugis huku mgomo wa matatu ukiendelea kushuhudiwa eneo hilo.
Katika eneo la Kitengela, baadhi ya waandamanaji wanadaiwa kugeuza maandamano hayo na kuanza kupora maduka yaliyokuwa yamefunguliwa. Hata hivyo, milio ya helikopta za polisi zimeanza kusikika angani huku maafisa wa usalama wakijaribu kudhibiti hali.
Haya yakijiri Waziri wa nishati Opiyo Wandayi amewataka wakenya kuvuta subira akiwaahidi kuwa serikali inashughulia suala la mafuta.
''Naomba wakenya wawe na subira.Serikali inashughulikia suala la mafuta'', anasema Waziri Opiyo.
Soma zaidi:









