Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
Bunge Kenya laidhinisha mapendekezo ya Uhuru Kenyatta katika mswada wa fedha
Spika wa bunge la Kenya, Justin Muturi, ameidhinisha uamuzi wa awali wa wabunge waliopigia kura pendekezo la rais Uhuru Kenyatta kupunguza kodi ya mafuta kutoka 16% hadi 8%.
Hii ni baada purukushani kuzuka bungeni kuhusu idadi kamili ya wabunge waliyoshiriki kura ya kuidhinisha hoja hiyo.
Spika alilazimika kusitisha kwa muda kikao hicho ili kuchunguza madai yaliotolewa na baadhi ya wabunge kwamba shughuli ya upigaji kura ilikumbwa na udanganyifu.
Hesabu ya wabunge kuidhinisha hoja
Kwa mujibu wa katiba, thuluthi tatu ya wabunge wanahitajika kuwa bungeni ili kuidhinisha au kupinga hoja.
Ni wabunge 213 kati ya 349 waliyokuwa wakati wa shughuli ya kupiga kura bungeni leo.
Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanasema suala hilo la kodi limegubikwa kisiasa.
Kumekuwa na madai kwamba wabunge wamekasirishwa na hatua ya raisi kupunguza bajeti yao.
Kumekuwa na hisia kwamba raisi pia amepunguza hazina ya maeneo bunge (CDF), bila kutilia maanani bajeti ya serikali kuu.
Mapendekezo mengine ya rais Kenyatta kwa bunge
- Kupunguza fedha zilizotengewa miradi ya maendeleo katika serikali za kaunti kwa Sh9 bilioni.
- Kupunguza fedha za kumarisha huduma katika serikali za kaunti kwa Sh3.8 bilioni.
- Rais Kenyatta amependekeza kupunguzwa kwa bajeti ya usafiri na shughuli zingine zisizo muhimu kwa taifa.
- Kuongeza kodi ya VAT kwa watumiajiwa simu kutoka 10% hadi 15%
- Kuongeza fedha katika idara za utekelezaji wa sheria ili kukusanya mapato zaidi kupitia mahakama ya nchini.
Mapendekezo hayo yote yakiidhinishwa na bunge, kila mfanyikazi anayepokea mshahara wa kuanzia shilingi 100,000 atatozwa kodi ya 1.5% na muajiri wake atachangia 2%.
Fedha hizo zitatumiwa kuchangia mradi wa nyumba ya gharama nafuu.
Mradi huo ni sehemu ya ajenda nne kuu za raisi Kenyatta.
Baadhi ya wakenya wamenukuliwa na vyombo vya habari wakilalamikia hali ngumu ya maisha itakayowakabili siku za usoni.
Wengine wao wamekashifu muafaka uliofikiwa kati ya kiongozi wa upinzani Raila Odinga na Rais Uhuru Kenyatta.
Wanasema kuwa muafaka huo umezima makali ya upinzani kuzungumza dhidi ya maovu ya serikali.